Mtaalamu
wa masuala ya vyombo vya habari jamii na Mkufunzi Bi Rose Haji Mwalimu
(aliyesimama) wakati wa ufunguzi kijiji cha Usagara, wilayani Misungwi
mkoani Mwanza hivi karibuni.
Na Modewjiblog team, Mwanza
Tabia
ya watu kukwepa kutoa ushahidi mahakamani ni sababu mojawapo ya
wahalifu wa mauaji ya albino kutotiwa hatiani na kuachiwa huru.
Hayo
yameelezwa katika warsha zilizoendeshwa mfululizo wilayani Misungwi,
Kahama na Bariadi za ushirikishwaji wa jamii katika kuzuia na kutokomeza
ukatili, unyanyasaji na unyanyapaa kwa watu wenye ulemavu wa ngozi
(albinism) nchini.
Wakichangia
mada kuhusu changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu wa ngozi,
washiriki wamesema kwamba imekuwa ni kawaida kwa watu kutokuwa tayari
kutoa ushahidi mara wanapoitwa mahakamani kwa sababu zisizokuwa na
mashiko.
Sababu hizo ni kuogopa kuuawa na wahusika na shinikizo kutoka kwa wanafamilia.
“Mara
nyingi tumeshuhudia watu wanaoitwa mahakamani kutoa ushahidi hawaendi
siku kesi inaposikilizwa hata kama aliandikiwa na mahakama kufanya
hivyo, wengine huamua kuhama kabisa eneo analoishi kwa kukwepa lawama
kutoka kwa jamii au familia na kuogopa kuuawa baada ya kugundulika kuwa
katoa ushahidi,” alisema mmoja wa washiriki.
Kuachiwa
kwa watuhumiwa wanaodaiwa kuhusika na ukatili hususan kukatwa viungo na
mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi kumezua mjadala mkubwa katika
jamii kwamba jeshi la polisi haliwajibiki kikamilifu au kuhisiwa kuwa na
ushirikiano wa namna fulani na watuhumiwa hao.
Afisa
mtetezi na ushawishi kutoka shirika linaloshughulika na watu wenye
Albinism la Under The Same Sun (UTSS), Kondo Seif akisisitiza jambo kwa
washiriki katika warsha ya siku tatu iliyofanyika katika kijiji cha
Nyakasungwa wilayani Sengerema mkoani Mwanza hivi karibuni.
“Mtuhumiwa
anapoachiwa huru wanajamii wanaona kama polisi imepewa rushwa kuwachia,
hawaelewi kwamba wao wenyewe wameshiriki kwa mtuhumiwa huyo kuwa huru
kwa sababu hawana ujasiri wa kujitokeza mahakamani kama walivyoweza
kutoa maelezo ya awali kwa polisi,” wamedai washiriki hao.
Tanzania imekumbwa na wimbi kubwa la ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu jambo ambalo limelitia doa taifa.
Kwa
mujibu wa Kamisheni ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa
Mashambulizi hayo ambayo yanahusishwa na matumizi ya viungo vya miili ya
watu wenye ulemavu wa ngozi kwa imani za kishirikina yamepoteza maisha
ya watu wapatao 73 wenye ulemavu huo nchini kuanzia mwaka 2000.
“Huku
kwetu imani za kishirikina zimeenea na waganga wa jadi ni wengi sana.
Ni kawaida kabisa kwa mtu wa sehemu hizi kwenda kwa mganga wa kienyeji
ili apigiwe ramli endapo kuna mtoto mgonjwa au kifo kimetokea katika
kaya badala ya kwenda kituo cha afya,” alisema Bahame Maduhu, mwenyekiti
Kata ya Nkololo wilayani Bariadi.
Maduhu
amesema kwamba watu wajanja wamechukua udhaifu wa wanajamii kutoka
kanda ya Ziwa kuamini ushirikina kiasi kwamba waganga wengine wenye
tamaa za kutajirika kutoka sehemu mbalimbali za nchi wamehamia katika
ukanda huo.
Washiriki
wakiandaa mpango kazi kwa ajili ya utekelezaji ili kudhibiti ukatili
dhidi ya ukatili ya watu wenye ulemavu wa ngozi katika kijiji cha
Nkololo, Kata ya Nkololo wilayani Bariadi.
“Waganga
hasa wanaotumia ramli na mapepo machafu ndio wenye kuendesha mauaji ya
watu wenye ulemavu wa ngozi ili kukamilisha huduma za wateja wao ambao
hutaka utajiri, kuchimba madini, uvuvi na biashara nyingine, alieleza
mwenyekiti huyo.
Kuzorota
kwa hali ya usalama kwa watu wenye ulemavu wa ngozi serikali
ililazimika kuwahamishia katika vituo maalum kwa ajili ya ulinzi.
Hata
hivyo kwa sababu za msongamano hali ya vituo hivyo imezorota kutokana
na kukosekana kwa huduma muhimu hususan za afya, chakula, mavazi na
malazi .
Vituo
hivyo ni Mitindo, Misungwi mkoani Mwanza, Buhangija mkoani Shinyanga,
Kabanga mkoani Kigoma na Shule ya Msingi Pongwe mkoani Tanga.
Hadi
sasa ni vigumu kuelewa sababu za ukatili huo lakini kwa mujibu wa
washiriki wa warsha hizo utamaduni uliojenga imani za ushirikina
zilizoota mizizi katika jamii, elimu duni, biashara za uvuvi, uchimbaji
wa madini, utapeli uliojipenyeza katika tiba asili na unyanyapaa zimetajwa kuwa miongoni mwa chanzo cha ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi.
Hali
hii imelisukuma Shirika la Kimataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni
(UNESCO) kuandaa warsha nne mfululizo zilizowakusanya wanajamii 160
kutoka vijiji 12 zenye lengo ya kubaini matatizo na kutafuta suluhisho
katika jamii kwa kuihusisha jamii yenyewe katika kupambana na ukatili
dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi.
Miongoni
mwa walioshirikiana na UNESCO kutoa elimu hiyo ni wataalamu kutoka
Shirika la Serikali la Haki za Binadamu (CHRAGG), Baraza la Tiba Asili
Muhimbili na shirika la kimataifa linaloshughulikia masuala ya watu
wenye ulemavu wa ngozi ‘Under The Same Sun’ (UTSS).
Wilaya
ya Sengerema mkoani Mwanza ilitoa vijiji vitatu ambavyo ni Nyanzenda,
Nyakalilo na Nyakasungwa; Mwanza kijiji cha Luchili, Idetemya na Fela.
Wilaya ya Bariadi ilishirikisha kijiji cha Nkololo, Nkindwabiye na
Gasuma wakati Msalala ilitoa vijiji vitatu ambavyo ni Ndala, Busungo na
Chela.
Mwenyekiti
wa Baraza la Tiba Asili na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Tiba Muhimbili
Dakta Edmund Kayombo akielezea umuhimu wa waganga wa jadi kujisajili
katika warsha ya siku tatu iliyofanyika katika kijiji cha Nyakasungwa
wilayani Sengerema mkoani Mwanza kuhusu ushirikishaji jamii katika
kuandaa na kutekeleza mikakati itakayochangia kuzuia na kutokomeza
unyanyasaji na dhulma zinazofanywa dhidi ya watu wenye albinism
iliyoshirikisha waganga wa asili, wauguzi na wakunga, viongozi wa dini,
walimu pamoja na watu maarufu iliyoandaliwa na Shirika la Umoja wa
Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO).
Mshiriki
wa warsha ya ushirikishwaji jamii kudhibiti ukatili dhidi ya watu wenye
ulemavu wa ngozi akiwasilisha mpango kazi wa kikundi kazi.
Baadhi
ya washiriki kutoka kata ya Nkololo wakifuatilia kwa makini maelezo ya
warsha ya siku tatu kuhamasisha ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu wa
ngozi.
Picha
ya pamoja ya washiriki wa warsha inayoshirikisha wanajamii kuandaa
mpango mkakati wa kudhibiti ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi
iliyofanyika Usagara wilayani Misungwi mkoa wa Mwanza.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269