MTANDAO wa Wanawake na Katiba na
Uchaguzi umeitaka Serikali ya Awamu ya Tano iliyopo chini ya Rais Dk.
John Pombe Magufuli ijenge misingi imara itakayoondoa mazingira
kandamizi kwa jamii ya chini hasa kwa akinamama. Aidha umeitaka serikali
kuhakikisha inasimamia ipasavyo suala zima la uwajibikaji na kupambana
na vitendo vya kifisadi ambavyo ndivyo vinavyowakandamiza wananchi.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini
Dar es Salaam na jopo la viongozi wanaounda mtandao huo likiongozwa na
Mwenyekiti wa Umoja wa Mtandao, Profesa Ruth Meena walipokuwa wakitoa
tathmini juu ya mtazamo wa mtandao huo baada ya Uchaguzi Mkuu na suala
zima la usawa wa jinsia kwa wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari.
Akizungumza katika mkutano huo,
Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Wanawake Tanzania, Mary Rusimbi ambaye
ni mjumbe wa Mtandao wa Wanawake na Katiba na Uchaguzi alisema serikali
ya awamu ya tano ina kila sababu ya kumjali mwanamke na kutambua kuwa
anamchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi.
Alisema Serikali hainabudi kujenga
misingi imara ya uwajibikaji wa kweli na kutambua makundi mbalimbali ya
jamii kwa jinsia zote. “…Tunataka haki yetu iwe haki kweli kweli na
itambulike huku ikiwa nautekelezaji wa vitendo na kwa uhakika,”
alisisitiza Bi. Rusimbi.
Alisema kuwa wangependa kushuhudia
idadi ya kutosha ya wanawake inaingia katika ngazi mbalimbali za
uongozi na vyombo vya maamuzi ili waweze kuingiza changamoto zao na
kuzisemea ipasavyo kwa lengo la kupatiwa ufumbuzi.
Kwa upande wake Prof. Meena
akizungumzia mtazamo wa mtandao baada ya Uchaguzi Mkuu juu ya
ushirikishwaji wa wanawake katika kugombea nafasi anuai za uongozi
alisema bado kuna changamoto kubwa kwa kundi hilo kwani kulingana na
matokeo ya sasa Tanzania itafikia usawa wa 50/50 mwaka 2055.
Alisema licha ya ongezeko la fursa
ya vitimaalum kupandishwa hadi kufikia asilimia 40 bado fursa hizo
zinachangamoto kubwa kwani viti hivyo ndani ya vyama hutolewa kwa
wanawake kama aina fulani ya zawadi jambo ambalo huwazuia wanawake hao
kusimamia ajenda zao za msingi kwa kuhofia kuonekana wasaliti. “…Viti
hivi maalum hutolewa na vyama na vyama ndio vyenye ushawishi na misimamo
hivyo wanawake hawawezi kusimamia hoja zao ipasavyo…,” alisema Prof.
Meena.
Aidha Profesa Meena alivitaka
vyombo vya habari kusaidia kubeba ajenda za wanawake na kukemea mfumo
dume ili kuibadili jamii ambayo bado inamtazamo hasi juu ya wanawake na
uwezo wao. Alisema wanawake walijitokeza kwa wingi katika uchaguzi huu
licha ya kwamba ndani ya vyama vyao bado kuna aina fulani ya ugumu
katika kuwapa nafasi kundi hilo.
Naye Mjumbe wa Mtandao huo, Dk
Ave-Maria Semakafu aliitaka serikali kuendelea kuondoa vikwanzo na
changamoto mbalimbali katika jamii ambazo bado zinamtesa mwanamke.
Alisema huduma za elimu bado mtoto wa kike anachangamoto jambo ambalo
linamnyima kufikia malengo yake huku huduma nyingine za maji na
utafutaji wa nishati ya kuni ikiwa ni mzigo kwa mwanamke.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269