Breaking News

Your Ad Spot

Nov 30, 2016

MADAKTARI NCHINI WAMETAKIWA KUITISHA MIKUTANO YA KIJAMII ILI KUJADILI MAGONJWA


Katibu Mtendaji wa Chama cha Afya ya Jamii Tanzania (TPHA), Fabian Magoma  (kulia), akizungumza katika Kongamano la 33 la siku tano la Chama cha Afya ya Jamii Tanzania (TPHA) linaloendelea Hoteli ya Kebby Mwenge jijini Dar es Salaam leo asubuhi. Kushoto ni  Mwenyekiti wa TPHA anayemaliza muda wake, Daktari Bingwa  Elihuruma Nangawe.
Dk. Manase Frank akitoa mada kwenye kongamano hilo.

 Profesa Andrew Swai akitoa mada.
 Wadau wa sekta ya afya wakifuatilia kwa karibu mada zilizokuwa zikitolewa katika kongamano hilo.
 Kongamano likiendelea.
 Dk. Andronicus Aloyce Rwelamila kutoka Hospitali ya Tumbi Kibaha (kushoto) na Muuguzi wa Hospitali hiyo, Mary Gowele wakiwa kwenye kongamano hilo.
 Kongamano likiendelea

Usikivu katika kongamano hilo. Kushoto ni Mwenyekiti wa TPHA, Dk. Elihuruma Nangawe

 Profesa Japhet Kileo (kulia), akiuliza maswali kwenye 
kongamano hilo.
 Dk. Mwanahamisi Magwangwara (kushoto), akizungumza wakati akijibu maswali mbalimbali kutoka kwa wadau wa sekta ya afya katika kongamano la 33 la siku tano la Chama cha Afya ya Jamii Tanzania (TPHA) linaloendelea Hoteli ya Kebby Mwenge jijini Dar es Salaam leo. Kulia ni mtoa mada, Profesa Andrew Swai. 
Dk.Chilolo Edward (katikati), akijibu maswali kuhusu changamoto ya waendesha bodaboda. Kushoto ni Profesa Andrew Swai na Dk. Manase Frank. 
Mkurugenzi wa Shirika la Wanawake katika Jitihada za Maendeleo (WAJIKI), Janeth Mawinza akielezea changamoto ya matumizi ya pombe katika Manispaa ya Kinondoni.

Na Dotto Mwaibale

MADAKTARI nchini wametakiwa kufanya mikutano ya kijamii au wananchi ili kuwapa fursa ya kujua magonjwa yanayo wakabili.

Hayo yalielezwa na Dk. Manase Frank wakati akitoa mada katika kongamano la 33 la siku tano la Chama cha Afya ya Jamii Tanzania (TPHA) linaloendelea Hoteli ya Kebby Mwenge jijini Dar es Salaam leo asubuhi.

"Changamoto kubwa tuliyonayo ni wananchi wengi kutojua magonjwa yanayowasumbua hivyo ni muhimu kwa madakatari kuitisha mikutano itakayowakutanisha na wananchi ili kuondoa changamoto hiyo" alisema Dk. Frank.

Alisema wagonjwa wengi wamekuwa wakikata tamaa kwa kuchangiwa na kauli za baadhi ya madaktari ambao wanashindwa kujua tatizo la mgonjwa husika hivyo wakati umefika wa madaktari kushirikiana kwa karibu na jamii, viongozi wa dini  ili kuondoa changamoto hiyo.

Akitolea mfano wa kijana mmoja ambaye alifiwa na ndugu zake wote wa karibu kutokana na ugonjwa wa ukimwi na kuishi kwa kunyanyapaliwa lakini baadaye afya yake ilikuja kuimarika kufuatia ushauri uliotolewa na daktari kwa  jamii iliyokuwa ikimzunguka wakati wa ugonjwa wake.

Mtoa mada mwingine Profesa Andrew Swai aliomba serikali wakati wa siku ya Jumamosi na Jumapili kufunga baadhi ya barabara ili zitumike kwa wananchi kufanya mazoezi ya kutembea ili kujenga afya za miili yako na kuepukana na magonjwa kama kisukari.

Akizungumzia changamoto ya matumizi ya bodaboda Dk.Chilolo Edward alisema kwa mwaka jana katika Hospitali za mikoa ya  Morogoro, Tumbi Pwani na Shinyanga kulikuwa na ajali 895 huku majeruhi wakiwa 4813.

Alisema majeruhi waliolazwa katika hospitali hizo walikuwa ni 4525, waliopewa rufaa kwenda hospitali za Bugando na Muhimbili walikuwa 71 na waliolazwa ni 702.

Alisema vifo vilikuwa 81 hivyo vilitokea baada ya kufikishwa Hospitalini ni 70 na vilivyotokea eneo la ajali vilikuwa 11.

Dk.Chilolo alisema ili kupunguza changamoto hiyo inapaswa watoa huduma za afya kutoa elimu kwa waendesha boda boda pale wanapofikishwa mahospitali kuhusu umuhimu wao katika familia na taifa kwa ujumla hivyo kuwa makini wanapoendesha vyombo hivyo vya moto badala ya kuacha kazi hiyo kufanywa na polisi au Sumatra.


No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages