Breaking News

Your Ad Spot

Nov 14, 2016

WASIWASI WA VIONGOZI WA AFRIKA KUTOKANA NA USHINDI WA TRUMP KATIKA UCHAGUZI WA RAIS MAREKANI

Ushindi wa Donald Trump katika uchaguzi wa rais nchini Marekani umezusha wimbi na wasiwasi mkubwa na hali ya kutokuwa na imani kuhusu siasa za kigeni za kiongozi huyo mkabala wa nchi za Afrika.
Mkurugenzi wa Kituo cha Habari cha Cape Town nchini Afrika Kusini, Rayan Cummings anaamini kuwa, kushika madaraka kwa Trump huko Marekani kunazua maswali mengi kuhusu mabadiliko ya siasa za nje za nchi hiyo katika masuala ya kupambana na ugaidi, biashara, misaada ya kifedha na makubaliano ya kimataifa ya mabadiliko ya hali ya hewa.
Japokuwa katika kampeni zake za uchaguzi Donald Trump hakugusia moja kwa moja suala la uhusiano wa siku zijazo kati ya Marekani na nchi za bara la Afrika, lakini swali linajitokeza kwamba, je, sisitizo lake la kupambana na ugaidi lina maana ya kushirikiana na nchi kama Nigeria na Kenya kwa ajili ya kuyaangamiza makundi ya Boko Haram na al Shabab? Rayan Cummings anaamini kuwa, iwapo tutayazingatia matamshi ya Trump katika kampeni za uchaguzi kuwa ndiyo dira ya sera na siasa za serikali yake, basi ni wazi kuwa rais mteule wa Marekani anaamini sana suala la kutumia mabavu na nguvu za kijeshi.
Kwa sasa Marekani imetuma majeshi katika nchi za Afrika kama wale waliotumwa Uganda kwa kile kinachosemekana ni kuisaidia serikali ya Kampala kupambana na waasi wa kundi la Lord's Resistance Army (LRA). Maafisa wa serikali ya Marekani wanaunga mkono suala la kutuma majeshi ya nchi hiyo barani Afrika; hata hivyo askari hao wanatumiwa kama wenzo wa kuingilia masuala ya ndani ya nchi za bara hilo. Suala hilo linaonekana wazi kwa kutilia maanani kwamba, nchi zinazolengwa zaidi barani Afrika ni zile zenye utajiri mkubwa wa maliasili kama almasi, dhahabu, urani na kadhalika.
Trump na Clinton
Kwa sasa wengi wanauliza kwamba, Donald Trump ambaye katika kampeni zake za uchaguzi alijikita zaidi katika matatizo ya ndani ya wananchi wa Marekani ataendeleza siasa na sera hizo baada ya kuapishwa rasmi na kushika hatamu za uongozi au la? Wachambuzi wa mambo wanasema, sisitizo la Trump na kujiepusha na siasa za kuingilia masuala ya ndani ya nchi kama Iraq na Syria lina maana ya Marekani kujitenga na masuala mengi ya kimataifa katika kipindi cha miaka minne ijayo. Wanasisitiza kuwa, iwapo hali itakuwa hivyo kutajitokeza mgongano wa kustaajabisha kati ya siasa za rais mteule wa Marekani na wanadharia wa siasa za kigeni mjini Washington hasa juu ya suala la kutuma majeshi ya nchi hiyo katika nchi zenye utajiri na maliasili nyingi kama zile za Afrika. 
Wakati huo huo misimamo mikali ya Trump kuhusu majukumu ya Marekani mkabala wa mkataba wa hali ya hewa wa Paris, inatia wasiwasi. Trump amekuwa akipinga vikali mkataba huo. Katika upande wa pili wasomi wanasema kuwa, bara la Afrika ndilo linalopatwa na madhara makubwa zaidi yanayosababishwa na mabadiliko ya hali hewa kuliko maeneo mengine ya dunia. Mkataba wa Paris unasisitiza kuwa, nchi za Afrika zinapaswa kupata misaada ya kifedha kutoka kwa Marekani na nchi nyingine zilizostawi ili kufidia madhara yanayosababishwa na nchi hizo kwa mazingira ya dunia.
Donald Trump
Donald Trump anaamini kuwa, mikataba ya kibiashara na uwekezaji wa moja kwa moja wa Wamarekani barani Afrika unasababisha kukosa ajira na kazi raia wengi wa Marekani. Hapa linakuja swali kwamba, vipi kiongozi mwenye mitazamo kama hiyo ataruhusu wamiliki wa viwanda, wafanyabiashara na matajiri wa Marekani kuwekeza barani Afrika na kutayarisha kazi na ajira kwa Waafrika maskini? Kwa msingi huo inatabiriwa kuwa, katika kipindi cha utawala wa Trump kutashuhudiwa kupungua sana kwa misaada ya kifedha ya Marekani kwa nchi za Afrika.  
Viongozi wa nchi za Afrika pia wana wasiwasi kwamba, katika kipindi cha utawala wa Trump, yumkini Marekani ukakiuka au kutengua Mkataba wa Biashara kati ya Mataifa ya Afrika na Amerika wa AGOA. Kwa mujibu wa mkataba huo nchi 39 za Afrika zinaweza kupeleka bidhaa zao za kilimo na kuziuza Marekani bila ya kulipa ushuru, ingawa baadhi ya viongozi wa Afrika kwa upande wao wamekuwa wakilalamika kuwa mkataba wa biashara huru wa AGOA unaifaidisha zaidi Marekani.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages