Watu 14 wameuawa katika mashambulio yaliyofanywa na makundi yanayobeba silaha mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Hayo ni kwa mujibu wa duru za jeshi na maafisa wa mkoa wa Kivu Kaskazini yalikofanywa mashambulio hayo.
Msemaji wa jeshi katika eneo hilo Kapteni Guillaume Djike amesema
mashambulio kadhaa yalifanywa jana usiku dhidi ya maeneo ya raia
na ngome za vikosi vya serikali. Djike, amelituhumu kundi la waasi wa
Mai-Mai kuwa ndilo lililohusika na mashambulio hayo.
Msemaji huyo wa jeshi ameeleza kuwa askari mmoja na raia mmoja
waliuawa katika eneo la Kaunga, raia wanne waliuliwa kwa kupigwa risasi
na kwa silaha baridi katika eneo la Kashalira na raia wengine saba
waliuliwa katika eneo la Kibirizi katika shambulio lililofanywa na watu
waliobeba silaha.
Wakati huohuo Roger Bihango, mwakilishi wa Gavana wa jimbo la Kivu
Kaskazini ametangaza kuwa waasi wa Mai Mai walimpiga risasi na kumuua
raia mmoja katika eneo la Buleusa.
Guillaume Djike ameongeza pia kuwa nyumba 150 zilichomwa moto katika mashambulio hayo ya jana usiku.
Mamia ya raia wameuawa katika mwaka uliopita katika machafuko na
mauaji ya halaiki yaliyofanywa na makundi yanayobeba silaha katika mkoa
wa Kivu Kaskazini wa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya
Kongo unaopakana na nchi za Rwanda na Uganda.../
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269