Rais Robert Mugabe wa Zimbambwe amechaguliwa
tena kubeba bendera ya chama tawala cha Zanu-PF katika uchaguzi wa rais
uliopangwa kufanyika mwaka 2018.
Mugabe amechaguliwa tena
kupeperusha bendera ya chama hicho katika mkutano wa kila mwaka wa chama
cha Zanu-PF uliofanyika jana katika mji wa Masvingo nchini Zimbabwe.
Katika mkutano huo wajumbe wa chama tawala walitangaza himaya yao kwa
Mugabe kama mgombea pekee wa chama hicho katika uchaguzi ujao wa rais
hapo mwaka 2018.
Mugabe amechaguliwa tena kugombea urais
kwa tiketi ya chama tawala cha Zanu-pf mwaka 2018 katika hali ambayo,
juma lililopita alitangaza kuwa, juhudi za baadhi ya maafisa wa chama
hicho za kutaka kumchagua mrithi wake mtarajiwa zinakinzana na ada ya
chama hicho. Mugabe sambamba na kutangaza utayari wake wa kuwania tena
kiti cha urais katika uchaguzi ujao alilaani kile alichokitaja kuwa
siasa chafu katika chama hicho na kusisitiza kwamba, wajumbe wa chama
tawala hawana haki ya kuchukua hatua yoyote ile ya kumchagulia mrithi.
Kundi moja ndani ya chama tawala cha ZANU-PF lilikuwa likifanya juhudi
za kumtangaza Grace mke wa Mugabe kuwa mrithi wa baadaye wa mumewe huku
kundi jingine likiwa linamuunga mkono Emmerson Mnangagwa Makamu wa Rais
wa Zimbabwe.
Rais Mugabe mwenye umri wa miaka 92 amechaguliwa tena kuwania kiti
cha urais kwa tiketi ya chama tawala katika uchaguzi ujao katika hali
ambayo, akthari ya wananchi wa nchi hiyo na hata maveterani wenzake
wanamtaka aachie uongozi na kukabidhi jukumu hilo kwa mtu mwingine. Kwa
muktadha huo mivutano ya kisiasa itaendelea kushuhudiwa nchini Zimbabwe
kutokana na hatua ya Rais Mugabe ya kung'ang'ania kuendelea kubakia
madarakani huku mikusanyiko na malalamiko ya aina yoyote ile
yakikandamizwa vikali na vikosi vya usalama vya nchi hiyo.
Siku chache zilizopita, Shirika la
Msamaha Duniani Amnesty International, lilitangaza kuwa, radiamali ya
polisi dhidi ya malalamiko na maandamano katika mitaa na barabara za
nchi hiyo ni ukiukwaji wa wazi wa haki za raia. Pamoja na hayo, mbinu ya
kale ya kuwakandamiza wapinzani kwa kutumia mabavu na kuwatisha wafuasi
wa vyama vya upinzani ingali inaendelea katika nchi hiyo.
Wapinzani wengi sambamba na kukosoa sera
za Robert Mugabe wanaamini kwamba, kiongozi huyo kutokana na umri
mkubwa alionao hawezi tena kuiongoza nchi kama inavyotakiwa huku athari
yao wakikosoa siasa zake hususani katika miaka ya hivi karibuni.
Hata kama Zimbabwe kama zilivyo athari nchi za Kiafrika
inakabiliwa na matatizo ya kiuchumi, umasikini na ukosefu wa ajira,
lakini katika miaka ya hivi karibuni nchi hiyo imeshuhudia mgogoro wa
kiuchumi ukishadidi kiasi kwamba, wafanyakazi wa serikali hawajapokea
mishahara yao kwa miezi kadhaa. Aidha theluthi mbili ya wakazi milioni
14 wa nchi hiyo wanapitisha maisha yao kwa kufanya biashara ndogo ndogo
za mikononi.
Katika wiki za hivi karibuni serikali ya
Zimbabwe ikiwa na lengo la kukabiliana na mgogoro wa kifedha
inaokabiliwa nao, ilichapisha noti mpya na kuziingiza katika mzunguko wa
fedha. Viongozi wa Zimbabwe wanaamini kwamba, sera hizo mpya za kifedha
zitaweza kutatua tatizo la uhaba wa fedha naakidi. Hata hivyo wakosoaji
wa serikali ya Harare wanasema kuwa, hatua hiyo ya serikali itapunguza
thamamani ya akiba ya fedha ya nchi hiyo na kuporomosha thamani yake
kufikia kiwango cha chini kabisa katika kipindi cha muongo mmoja
uliopita.
Ukame ni tatizo jingine linaloiandama Zimbabwe. Zimbabwe ambayo
wakati fulani ikitambulika kama ghala la nafaka Afrika, hivi sasa
inakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula kutokana na mabadiliko ya
tabianchi yanayojulikana kama Elnino. Hali hiyo imemfanya Rais Mugabe
atangaze hali ya hatari na kuitaka jamii ya kimataifa iisaidie nchi hiyo
ili iweze kujidhaminia bidhaa za chakula.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269