Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akitoa maagizo
kwa Mhandisi Mshauri Eng. Domicus Mapunda wa Kampuni ya Ujenzi ya Mbutu
Bridge JV inayojenga barabara ya Makutano-Nata KM 50 kwa kiwango cha
lami mkoani Mara wakati alipokagua mradi huo.
Mhandisi
Mshauri Eng. Domicus Mapunda wa Kampuni ya Ujenzi ya Mbutu Bridge JV
akitoa ufafanuzi kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa
Makame Mbarawa kuhusu mradi wa ujenzi wa barabara ya Makutano-Nata KM 50
inayojengwa kwa kiwango cha lami mkoani Mara wakati alipokagua mradi
huo.
Ujenzi wa barabara ya Makutano-Nata KM 50 inayojengwa kwa kiwango cha lami, wilaya ya Butiama, mkoani Mara ukiendelea.
Kaimu
Meneja wa Kiwanja cha Ndege cha Musoma Bi. Faraja akimuonesha Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kushoto), ramani
ya eneo la kiwanja cha ndege hicho, alipokagua kiwanja hicho mkoani
Mara.
Muonekano wa barabara ya changarawe ya kuruka na kutua ndege katika Kiwanja cha Ndege cha Musoma.
Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akitoa maelekezo
kwa Kaimu Meneja wa Kiwanja cha Ndege cha Musoma Bi. Faraja kuhusu eneo
litaloongezwa kiwanja hicho, mkoani Mara.
Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amewapa miezi
minne Wakandarasi Wazawa wa Kampuni ya Ujenzi ya Mbutu Bridge JV
inayojenga barabara ya Makutano-Nata kukamilisha km 18 kati ya 50 za
barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
Agizo
hilo limetolewa na Waziri huyo, alipokuwa akikagua mradi huo wa barabara
inayoanzia makutano kupitia Butiama, Nyamuswa hadi Sanzate ambao upo
katika mkoa wa Mara, na kutoridhishwa na kasi ya ujenzi wake ambayo
imesuasua kwa takriban miaka 3 sasa.
“Nataka
mwezi Aprili mwakani sehemu ya barabara hii iwe imeshakamilika kwa
kiwango cha lami na wananchi waanze kufurahia matunda yake, hatuwezi
kusubiri kwa muda wote huo kuwavumilia kukamilisha mradi huu”, amesema
Prof. Mbarawa.
Amesisitiza
kuwa nia ya Serikali ya kuboresha barabara hiyo ni kupunguza gharama za
usafirishaji, kuboresha makazi, kukuza uchumi kwa maeneo yaliyo kando
ya Barabara hiyo na kuhamasisha utalii kwenye mbuga za Wanyama za
Serengeti na Ngorongoro.
Naye,
Meneja wa Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS), Mkoa wa Mara Eng.
Japherson Nnko amesema kuwa barabara hiyo itakapomalizika itakuwa na
njia ya magari yenye upana wa mita6.5, mabega ya barabara ya mita 1.5
kila upande na Daraja kubwa la Kyarano lenye urefu wa mita 37.5.
Katika
hatua nyingine, Serikali imesema itawapa kipaumbele makandarasi wazawa
kuweza kushiriki katika mradi wa ujenzi wa reli mpya ya kisasa (Standard
Gauge), inayotarajiwa kuanza hivi karibuni katika maeneo mbalimbali
nchini.
Aidha,
Serikali imewataka Makandarasi hao kujitokeza kwa wingi kuchangamkia
fursa kwa kuomba zabuni za ujenzi huo na kuziimarisha kampuni zao
ikiwemo kuwa na vifaa vilivyo bora ili kupambana na soko la kibiashara
na makandarasi wa nje.
Sambamba
na hayo, Waziri Prof. Mbarawa amekagua Uwanja wa Ndege wa Musoma na
kusema kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha inapanua na kujenga kwa
kiwango cha lami uwanja huo hususani njia ya kuruka na kutua ndege
kutoka KM 1.6 ya sasa hadi KM 1.8 ili kuruhusu ndege kubwa zenye uwezo
wa kubeba abiria 70 kutua katika uwanja huo.
Waziri
Prof. Mbarawa amemaliza ziara yake ya siku mbili mkoani Mara ambapo
amekukagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wizara yake katika Wilaya
ya Bunda, Butiama, Musoma Mjini na Serengeti.
Imetolewa na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, kitengo cha Mawasiliano Serikalini(P.T)
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269