Breaking News

Your Ad Spot

Aug 15, 2017

RIDHIWANI AWAFUMBUA MACHO MADIWANI WA CHALINZE KUHUSU MAPATO YA VIJIJI VINAVYOZUNGUKA HIFADHI


Mbunge wa jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete ,akizungumza kuhusiana na faida na changamoto zilizopo kwenye vijiji vinavyozunguka hifadhi katika kikao cha mwaka cha baraza la madiwani la halmashauri hiyo.
 Baadhi ya madiwani na watendaji wa halmashauri ya Chalinze wakimsikiliza mbunge wa jimbo la Chalinze Ridhiwan Kikwete alipokuwa akizungumza faida na changamoto za hifadhi zilizopo kwenye vijiji vinavyozunguka hasa Wamimbiki na hifadhi ya taifa ya Saadan katika kikao cha mwaka cha baraza la madiwani la halmashauri hiyo.
 Mwenyekiti wa halmashauri ya Chalinze, Saudi Zikatim akizungumza katika kikao cha mwaka cha baraza la madiwani la halmashauri hiyo.(picha na Mwamvua Mwinyi)
Na Mwamvua Mwinyi,Chalinze


MBUNGE wa jimbo la Chalinze ,Ridhiwani Kikwete amewataka madiwani wa halmashauri ya Chalinze ,kukaa na viongozi wa vijiji vinavyozunguka hifadhi ya Saadan na Wamimbiki ili kujua mapato wanayonufaika nayo kwa mwaka na changamoto zilizopo.
Amesema zipo sheria zinazojieleza kuwa kila kijiji kinachozunguka hifadhi hupata mapato kwa mwaka kama si mwezi ambapo madiwani na halmashauri hazitambui.
Akizungumza katika kikao cha mwaka cha baraza la madiwani Chalinze,Ridhiwani alieleza,ipo haja ya kujua sheria za maliasili zinazosaidia maeneo yao pamoja na kulinda hifadhi ili kujiongezea kipato.
Aidha alisema kamati ndogo ya bunge ya mazingira na maliasili iliyoketi hivi karibuni kwa lengo la kujiuliza juu ya matatizo yanayoendelea kwenye bunga za hifadhi ikiwemo Wamimbiki inatarajia kufanya kikao na madiwani hao wakati wowote kuanzia sasa.
Ridhiwani alieleza kwamba,kamati hiyo itakwenda kuzungumza na halmashauri na madiwani hao ili kujua changamoto zinazowakabili .
“Wamimbiki ndio njia kubwa ya kupita tembo na wanyama wengine wakali kwenda Saadan na ndio njia ya wanyama wanaotoka Saadan kwenda Ruvuma na Selou”
“Kamati itatakaizungumzie uhifadhi na kutenga mazingira yetu yakae vizuri na kutengeneza vivutio Wamimbiki ili tutengeneze fedha nyingi kwa watalii hasa wa picha”alisema Ridhiwani.
Hata hivyo Ridhiwani alisema,zipo sheria zinazoruhusu ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri kuwa mwanachama kwa jambo hilo ambapo pia kila kijiji kinachozunguka hifadhi kwa mwaka inatakiwa kupata sh milioni.12.
“Kata na vijiji vinavyozunguka Saadan na Wamimbiki lazima mjue hilo,mie ndio nilijua katika kikao hicho hivyo fuatilieni kwenye vijiji vyenu mjue kama huwa wakinufaika na mapato hayo” .
“Unaweza kukuta vijiji havisemi na wakati mwingine vinahitaji fedha hata za madaftari kwa madiwani.;kama kweli havijui suala hili basi kikao chetu na kamati ndogo ya bunge kitasaidia kuleta ufumbuzi wa changamoto zetu”alifafanua Ridhiwani.
Mbali na hayo  aliwataka madiwani hao kuendelea kushikamana,kuwa na ushirikiano na kupendana .
Mbunge huyo aliwaomba wachapekazi kwa kasi waliyoanza nao ili kuiinua halmashauri hiyo ambayo inatoka kwenye uchanga na kuinua mapato yake zaidi ya sasa.
Nae mwenyekiti wa halmashauri ya Chalinze,Saidi Zikatim alisema wamepokea taarifa za ujio wa kamati hiyo kwani itakuwa mwarubaini wa changamoto mbalimbali zinazowakabili.
Alisema bado kuna kero kubwa ya migogoro ya  mipaka baina ya hifadhi na wana vijiji na kusababisha mahusiano yasiyo mazuri.

Zikatimu alibainisha ,hifadhi zinapaswa kutoa elimu na kutatua changamoto zinazowagusa na jamii ili kuondoa migongano isiyo ya lazima.


Katika kikao hicho ,diwani wa kata ya Mandela Madaraka Mbonde,alichaguliwa kuwa makamu mwenyekiti kwa kipindi cha mwaka mmoja.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages