Breaking News

Your Ad Spot

Jan 25, 2018

AGIZO LA RAIS DK MAGUFULI KUNUFAISHA KISARAWE

Na Frank Mvungi, MAELEZO- Dodoma
Mamlaka ya Maji Safi na Maji  Taka Dar es Salaam (DAWASA) imeanza kutekeleza kwa vitendo agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli la kuupatia maji mji wa Kisarawe uliopo Mkoani Pwani kutoka katika mtambo wa Ruvu Juu.

Kwa mujibu wa Taarifa kwa vyombo vya Habari iliyotolewa naDAWASA inaonyesha kuwa kazi zilizofanyika hadi sasa kabla ya zabuni kutangazwa ni pamoja na upembuzi yakinifu, usanifu wa kina wa mradi, kuandaa  makabrasha ya zabuni na kutangaza zabuni .

“Kwa sasa Kazi ya uchambuzi wa zabuni zilizowasilishwa na kufunguliwa mwishoni mwa wiki inaendelea ambapo Kampuni 12 za ndani na nje ya nchi zimejitokeza kuomba kutekeleza mradi huo” inasisitiza sehemu ya Taarifa hiyo.

Taarifa hiyo imebainisha kuwa mradi huo  mkubwa kwa awamu yakwanza utahusisha ujenzi wa kituo cha kusukuma maji kitakachokuwa na uwezo wa kusukuma maji kiasi cjha lita 60 kwa sekunde  na kujengwa kwa kituo chenye uwezo wa kuhifadhi lita 480,000 za maji.

Mradi huo utahusisha ununuzi na ulazaji wa mabomba makuu kwa umbali wa kilometa17 hadi Makao Makuu ya Wilaya ya Kisarawe.

Awamu ya Pili itahusisha ujenzi wa tenki la Vigungu ambalo litahudumia eneo lililotengwa kwa ajili ya makazi mapya na nyongeza ya maji kwa ajili ya Viwanda vitakavyojengwa.

Aidha DAWASA  imechukua hatua za muda mfupi kupunguza tatizo la maji katika mji huo  ikiwemo Wizara ya Maji na Umwagiliaji kupitia DAWASA kutekeleza mradi wa maji wa Vigama kwa kuchimba Kisima kipya,Kufunga Pampu, Kujenga mnara, kufunga tenki la kuhifadhia maji na kulaza mabomba ya kusambaza maji hayo ambapo mkandarasi wa kutekeleza mradi huo amepatikana na mradi utaanza mwezi Februari mwaka huu.

Hatua nyingine itakuwa DAWASA kukarabati kisima cha Shule ya Sekondari Manneromango ikiwa ni mchango wake katika mkakati wa kuboresha miundo mbinu ya shule ili kuongeza ufaulu katika Wilaya hiyo,mradi huo utaanza kutekelezwa machi mwaka huu

DAWASA imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya Maji katika Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kuondoa changamoto ya upatikanaji wa maji kwa wananchi wake .

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages