Kwa akali watu 12 wamepoteza maisha katika
ajali mbaya ya basi iliyotokea mkoani Tabora nchini Tanzania. Kwa
mujibu wa ripoti, ajali hiyo imelihusisha basi la Kampuni ya City Boys
lililogongana na lori aina ya Fuso katika eneo la Makomero wilaya ya
Igunga mkoani Tabora hapo na kwamba ajali hiyo imetokea usiku wa kuamkia
leo.
Aidha mbali na watu 12 kufariki dunia, wengine 46 wamejeruhiwa, baadhi wakiwa mahututi. Kaimu
Mkuu wa Usalama Barabarani wa Mkoa wa Tabora, Inspekta Hardson,
amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema kuwa chanzo cha ajali
hiyo ni tairi la kulia la gari ya Fuso kupasuka wakati dereva akijaribu
kukwepa shimo na kupoteza mwelekeo na hivyo kugongana na basi la City
Boys uso kwa uso.
Hardson
amesema miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Igunga huku
baadhi ya majeruhi wakiwa wamepelekwa katika hospitali ya Nkinga na
Bugando mkoani Mwanza kwa ajili ya matibabu. Ongezeko la ajali za
barabarani nchini tanzania linatajwa kusababishwa na madereva
kutoheshimu sheria za barabarani ambapo hivi karibuni pia, yaani tarehe
24 mwezi uliopita kulitokea ajali mbaya mkoani Pwani na kusababisha watu
26 kupoteza maisha. Takwimu zinaonyesha kuwa, kila mwaka mamia ya watu
hufariki dunia katika ajali za namna hiyo nchini Tanzania suala
lililoifanya polisi ya nchi hiyo kuweka sheria kali za barabarani
kukiwemo kuwatoza faini kubwa madereva.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269