Breaking News

Your Ad Spot

Oct 16, 2011

JAJI MKUU AMFAGILIA JK NEW YORK

* NI KWA KUONGEZA MAJAJI
 Jaji Mkuu, Mhe. Mohamed Chande Othman amempongeza na kumshukuru  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa  kuongeza Majaji.


Jaji Mkuu (watano kutoka kushoto katika picha) ametoa pongezi hizo mwishoni mwa wiki, wakati alipoutembelea Ubalozi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa na kupata fursa ya kubadilishana mawazo na maafisa wa Ubalozi huo (pichani).
Jaji Mkuu Mhe. Chande amesema, uamuzi wa Rais Jakaya Kikwete wa kuteua majaji wengi katika Mahakama Kuu ni kielelezo cha namna gani anavyojali utawala wa sheria na anastahili kushukuriwa.
Aidha Jaji Mkuu, amesema uamuzi wa serikali wa kuanzisha Mfuko wa Mahakama kama ilivyo kwa muhimili mwingine wa dola yaani Bunge, ni jambo jema kwa kuwa mfuko huo utasaidia sana katika si, tu uboreshaji wa kazi za mahakama lakini pia katika suala zima la kuwahudumia wananchi ikiwa ni pamoja na kupungunza mrundikano wa kesi.
“Mhe. Rais ametusaidia sana, ameteua majaji wengi katika Mahakama Kuu tena wengi wao wakiwa vijana, hawa watadumu kwa muda mrefu. Tunamshukuru sana kwa hili na ni matumaini yangu kuwa ataendelea na hatua hii ya kutuongeza majaji wengi zaidi” amesema.
Katika mazungumzo yake na maafisa hao, mazungumzo ambayo pia yaliwahusisha maafisa kutoka wizara mbalimbali ambao wapo hapa New York kuhudhuria mikutano ya Kamati za Baraza Kuu la 66 la Umoja wa Mataifa, Jaji Mkuu amebainisha kuwa mahakama nchini bado zinakabiliwa na changamoto nyingi.
Amezitaja baadhi ya changamoto hizo ambazo pia zina kwamisha ufanisi na ambazo baadhi zimeanza kufanyiwa kazi, ni pamoja na ile ya kujaribu kutenganisha kazi za kisheria na kazi za kiutawala.
“Kama nilivyosema, tunakabiliwa na changamoto nyingi, zikiwamo hizo za upungufu wa majaji na mlundikano wa kesi,lakini kuna hili la mahakimu kufanya kazi za utawala hasa huko mikoani, hili pia ni tatizo kubwa tumeanza kulifanyia kazi”
Amefafanua kwa kusema , mahakimu wengi wamekuwa wakifanya kazi za utawala kwa mazoea tu, na kwamba hiyo si sahihi na inawapunguzia muda wa kushughulikia kesi.
Akasisitiza kwamba kazi za utawala, za mipango, uhasibu, au uratibu wa raslimali watu ni kazi ambazo zina mafunzo yake, ni kazi za kitaalam.
“ Katika hili mahakimu wetu wanafanya kazi kwa mazoea tu ni mfumo ambao tumeurithi. Tumejipanga kuubadili utaratibu huu, ili mahakimu wafanye kazi za kisheria na watawala wafanye kazi za utawala na mengineyo.
Aidha ameongeza kuwa uongozi wake wake umejipanga pia katika kuboresha utendaji kazi katika mahakama za mwanzo ambako amesema asilimia zaidi ya 75 ya kesi ndiko ziliko
Akizungumzia kuhusu mlundikano wa kesi, Mhe. Jaji Mkuu amesema ingawa kumekuwapo na uboreshaji katika usikilizaji wa kesi na utoaji wa hukumu. Lakini bado kuna mlundikano mkubwa wa kesi ambazo hazijapata hata nafasi ya kusikilizwa .
Akatoa mfano wa Mahakama Kuu kitengo cha Ardhi ambako amesema kuna kesi nyingi sana ikilinganishwa na majaji waliopo ambao ni wanne tu.
“ Matatizo ya ardhi ni moja ya tatizo kubwa na lenye mlundikano mkubwa wa kesi. Ni kweli kwamba Wizara husika imejitahidi sana katika kupunguza baadhi ya matatizo yakiwamo ugawaji wa viwanja kwa mtu zaidi ya mmoja . Lakini bado mfumo wa wizara hiyo kushughulikia matatizo ya ardhi si mzuri sana. ”
Akasema mfumo wa kushughulikia matatizo ya ardhi unatatiza kwa kuwa matatizo hayo yanaanzia katika ngazi za chini kama vile ngazi za vijiji na kuendelea hadi wizarani. Lakini utatuzi wake wa kisheria unaishia mahakamani.

“Tumejipanga kulitatua tatizo hilo, jambo moja tunalotaka kufanya ni kuifanya Mahakama Kuu kitendo cha Ardhi, mfumo wake uwe kama Mahakama ya Biashara. Kwa kutumia mfumo wa Makahama ya Biashara tunaamini kwamba kasi ya kushughulia kesi za ardhi utaboreka na ufanisi utaongezeka”. Amesisitiza.
Akijibu swali kuhusu mchakato wa maandalizi ya Katiba mpya pamoja na hukumu ya kuyonga.
Jaji Mkuu alikuwa na haya ya kusema. Kuhusu Katiba, kazi ya maandalizi ikiwamo ya kuratibu ukusanyaji wa maoni, pamoja na utoaji wa elimu kwa wananchi inaendelea vizuri na kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pia imeshirikishwa kwa asilimia 100.
Akasisitiza kwamba licha ya mkanganyiko uliojitokeza mwanzoni mwa zoezi hilo, ana imani kubwa na serikali kwa kile alichosema imejipanga vizuri.
Kuhusu hukumu ya kunyonga, Jaji Mkuu amesema kwa Tanzania, kuendelea kuwepo au kutokuwapo kwa hukumu ya kunyoga bado ni mjadala unaoendelea.
Akasema huko nyuma iliwahi kufanyika kura ya maoni kuhusu suala hilo. Matokeo ya kura hiyo yalidhihirisha kwamba bado wananchi walio wengi wanataka hukumu hiyo iendelee , huku idadi kubwa pia ikitaka hukumu hiyo ifutwe.
“kwa upande wa Tanzania, uamuzi wa kuwapo au kuto kuwapo kwa hukumu ya kunyonga bado lina mjadala wa aina yake. Na kwa kweli si kazi ya mahakama kuifuta adhabu hiyo, ni jukumu la chombo kingine ambacho ni Bunge. Lakini pia bado kuna mawazo tofauti miongoni mwa wananchi” akasema Jaji Mkuu.
Hata hivyo akasema kutokana na namna ambavyo mwenendo wa kimataifa umekuwa ukiichukulia hukumu hii ya kunyonga kama utoa kipaumbele  uboreshaji na utendaji kazi wa Mahakama nchini Tanzania

ukiukwaji wa haki za binadamu.Ana uhakika kwamba baada ya miaka kadhaa  nchi nyingi zitakuwa zimeondokana na adhabu hii.
Akasema kuwa ingawa Tanzania inayo na   hii ya kunyonga, lakini utekelezaji wake ni mdogo sana. Kwa mfano akasema Rais wa awamu ya Tatu Benjamin Mkapa na Rais wa awamu ya nne  Jakaya Kikwete hawajawahi kusaini hati za watu kunyongwa.  
Katika hatua nyingine Jaji Mkuu Mhe. Mohamed Othman Chande amesifu uhusiano mzuri uliopo baina ya mihimili mitatu yaani, serikali, Bunge na Sheria na kwamba angalau hakuna muingiliano kati ya vyombo hivyo.
Katika  mazungumgo yake na Maofisa hao, Mhe. Jaji Mkuu amewapongeza maofisa hao wa Ubalozi, kwa kazi kubwa na nzuri ya kuendelea kupeperusha bendera ya  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, na kwamba utendaji wao wa kazi umeijenga  sifa kubwa Tanzania mbele ya  Jumuia ya Kimataifa.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages