Breaking News

Your Ad Spot

Jul 10, 2012

WALIODAI KUUAWA CHADEMA KUHOJIWA NA POLISI

Seikali itachukua hatua za kuwahoji viongozi wa Chadema waliodai kutaka kuuawa, licha ya chama hicho kukataa kupeleka tuhuma zao hizo kwenye vyombo vya dola kwa madai ya kukosa imani na vyombo hivyo.
  Pia, imewataka viongozi wa kisiasa  kuacha tabia ya kukurupuka kutoa taarifa za kuogopesha wananchi kwani umaarufu wa kisiasa hauletwi kwa kuchonganisha raia na vyombo vya dola au serikali  wakati kuna sehemu husika wanakoweza kupeleka malalamiko yao.
    Hayo yalielezwa na Waziri wa Ulinzi na na Usalama, Dk Emmanuel Nchimbi, wakati akitoa tamko la serikali kwa waandishi wa habari jana mjini Dodoma, juu ya tuhuma za baadhi ya viongozi wa juu wa Chadema kudai wapo hatarini kuuawa.
   Dk Nchimbi alieleza kwamba viongozi wa kisiasa wanatakiwa kuachana na tabia ya kutuhumu vyombo vya ulinzi kwani kufanya hivyo ni kuvifanya vyombo hivyo kukata tama wakati kuna mambo mengi vyombo hivyo vinafanya kwa ulinzi wa raia na nchi kwa jumla.
   Alisema kwamba kitendo cha viongozi wa Chadema kupiga kelele za kutaka kuuawa ni kuonyesha udhaifu wa kiuongozi, maana hata wananchi watashangaa aina ya viongozi wanaotaka kuwapa nchi wanaishia kuzusha hofu badala ya kuhamaisha maendeleo.
   Dk Nchimbi alieleza kwamba kazi ya vyombo vya usalama ikiwemo Jeshi la Polisi ni kulinda raia na mali zao na ni jambo la kisheria, hivyo amewagiza viongozi wa Jeshi la Polisi kuwahoji nani anataka kuwaua na kwa namna gani ili hatua zichukuliwe.
    Alieleza kwamba tuhuma zinazotolewa na Chadema ni nzito, hivyo serikali haiwezi kukaa kimya kwa hoja kwamba chama hicho hakina imani na jeshi la polisi na badala yake itawahoji kwa kuwa wamepewa dhamana ya kulinda raia wakimo Chadema .
    ‘Nimeamuru jeshi la polisi liwahoji maana kazi ya polisi ni kulinda raia na mali zao, hivyo hatuwezi kukaa kimya kwa hoja kwamba hawana imani na jeshi hilo’alieleza.
     Dk Nchimbi alisema kwamba tabia inaliyoanza kujengeka kwa wanasiasa hususan chadema kukimbilia kutoa taarifa za kuuawa ni kulenga kuwaogopesha wananchi na kulazimisha umaarufu wa kisiasa, kitu ambacho hakiwezi kuwasaidia.
     Akitoa ufafanuzi juu ya kwa nini serikali haichukui hatua pamoja na viongozi wa chama hicho kulalamika mara kwa mara kwamba wanatishiwa kuuawa, Dk Nchimbi alieleza kwamba serikali haifanyi kazi kwa kukurupuka kwani ingefanya hivyo ingekwisha watia ndani viongozi wa chama hicho.
     ‘Mnakumbuka tuhuma za viongozi wa Chadema kuhusishwa na kifo cha Chacha Wangwe, kama serikali ingekuwa inafanya kazi kwa kukurupuka na kutafuta umaarufu ingewatia ndani viongozi hao lakini hatukufanya hivyo kwa kufahamu kwamba hizo ni tuhuma zisizo na ukweli’alieleza Dk Nchimbi.
    Aidha, alieleza kwamba viongozi wa chadema na wanasiasa wengine wafanye  mambo ya kuja kukumbukwa baadaye sio kuja kukumbukwa kwa kuzusha na kuogopesha wananchi, kitu ambacho hakina msaada kwa taifa,
    Alitolea mfano, Marekani  kwamba pamoja na nchi hiyo kutawaliwa na vyama viwili kwa awamu tofauti lakini viongozi na wananchi wake wamejenga uzalendo wa taifa lao na sio kila mtu anaweza kuamka na kuzusha la kwake.
    Katika hatua nyingine, Dk Nchimbi alivigeukia vyombo vya habari kwa kujenga tabia ya kuchagua kesi za kuandika na matokeo yake habari  zinazoonekana za maana ni zile zinazotolewa na chadema au chama kingine lakini zinazotolewa na chama cha mapinduzi na serikali yake sio habari kwao.
    ‘Tuache tabia hii, akifanya mtu wa chadema mnaona hizo ndio habari lakini akifanya mtu wa CCM mnaona hazina maana, lazima tujenge uzalendo wan chi yetu kwa kutekeleza wajibu wetu kwa haki,’alieleza Dk Nchimbi.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages