Breaking News

Your Ad Spot

Aug 18, 2012

TUPO WANGAPI? TULIZANA!


Na Anna Nkinda - Maputo, Msumbiji 
Takwimu zinaonyesha kuwa kwa mwaka 2011 zaidi ya watu milioni 34 ulimwenguni wanaishi na maambukizi  ya Virusi vya ugonjwa wa Ukimwi (VVU) kati ya hao  milioni 30.7  watu wazima, milioni 16.7 wanawake  na milioni 3.4 watoto wenye  umri wa chini ya miaka 15.
Hayo yamesemwa LEO na   Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Shirika la Kimataifa la Kupambana na Ugonjwa wa Ukimwi (UNAIDS) Dkt. Raul de Melo Cabral wakati akiongea na wake wa wakuu wa nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) waliohudhuria mkutano wa  kuzuia maambukizi ya virusi vya Ugonjwa wa Ukimwi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kwa maendeleo ya kanda unaofanyika Maputo nchini Msumbiji.
Dkt. Cabral alisema kuwa  ugonjwa wa Ukimwi utaendelea kuwa changamoto kwa nchi zote na kila mtu anatakiwa kupambana  nao ndiyo maana katika Azimio la  Kisiasa  lililofanyika mjini New York mwaka 2011 wakuu wa nchi zote wanachama wa Umoja wa Mataifa  (UN)  wakiwemo wa  SADC walipitisha malengo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua zaidi katika kupambana na ugonjwa huo.
“Walikubaliana kuwa  ifikapo  mwaka 2015 wawe wamepunguza nusu ya maambukizi  ya ugonjwa huo katika nchi zao, kupunguza maambukizi mapya kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto,  kutoa matibabu kwa watu milioni 15 katika nchi zote wanachama wa umoja huo wanaoishi na VVU  na kuongeza  bajeti katika masuala yanayohusiana na afya”, Alisema.
Akichangia mada katika mkutano huo Mke wa Rais ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya wanawake na Maendeleo (WAMA) Mama Salma Kikwete alisema kuwa ni jambo jema kwa wake wa viongozi wa SADC kuwa na mfumo mzuri wa utendaji kazi ambao  utawawezesha kufanya mambo  yatakayokuwa na tija katika kanda  na kuweza kuwasaidia wanawake  na watoto  ambao kwa kiasi kikubwa wameachwa nyuma kimaendeleo.
“Sisi kama wanachama tunatakiwa kutengeneza  mpango mkakati na kuona jinsi gani unaweza kujitoa  ili kuweza kutimiza  malengo tuliyojiwekea  ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto yanapungua  au kutokuwepo  kabisa katika  jamii inayotuzunguka”, alisema Mama Kikwete.
Aliendelea kusema kuwa pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo kuwasaidia rasilimali ambazo wanazifanyia kazi kila siku wao pia wanajukumu kubwa la kuhakikisha kuwa wanachangia  kwa kiasi kikubwa ili waweze kutimiza malengo waliyojiwekea.
 Kwa upande wake Mke wa Rais wa Zambia ambaye pia ni Mwenyekiti  wa Umoja wa wake wa  Marais wa Afrika wa Kupambana na Ugonjwa wa Ukimwi (OAFLA) Dkt. Christine Kaseba Sata alisema kuwa  hivi sasa nchi za SADC zinafanya jitihada kubwa ya kupunguza maambukizi ya ugonjwa huo kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto (MTCT) baada ya kugundua kuwa ugonjwa huo ni wa hatari si tu kwa watu wanaoishi na ugonjwa huo  bali hata kwa watoto wanaoupata kutoka kwa mama zao.
Dkt. Sata alisema kuwa Ugonjwa wa Ukimwi unatishia maisha ya watu  kwa kizazi kilichopo na  kijacho kwani watoto wengi wanaozaliwa kama watakuwa na maambukizi  hawataweza kuishi muda mrefu, ugonjwa huo unaharibu familia, kupunguza uzalishaji na uchumi  katika ngazi ya familia na kutokuwa  na kizazi kisichokuwa na urithi kwa kizazi kijacho.
“Licha ya kupambana na ugonjwa wa Ukimwi changamoto nyingine tunayokabiliana nayo  ni ya kuenea kwa kasi kwa ugonjwa wa shingo ya kansa ya kizazi na matiti kwa wanawake wengi katika nchi wanachama wa Umoja wa SADC, wanawake  hawa wanakufa kwa ugonjwa  ambao unaweza kuzuilika na kutibika kama mgonjwa atapata matibabu mapema” , Dkt.Banda alisema,
Aliendelea kusema kuwa wanawake wengi wanakufa kwa kukosa uelewa kuhusiana na ugonjwa huo , kutofanyiwa uchunguzi na kupata huduma za matibabu mapema  na kuwashauri wake hao wa viongozi kufanya kazi kwa ukaribu na Serikali ya nchi zao  jambo ambalo litawafanya  watu  wengi zaidi kuwa na ufahamu kuhusiana na ugonjwa huo.
Mkutano huo wa siku mbili  wenye kaulimbiu isemayo kuondoa maambukizi ya Ugonjwa wa ukimwi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto  inawezekana  unahudhuriwa na wake mbalimbali wa wakuu wa nchi wanachama wa SADC akiwemo mke wa Rais Mama Salma Kikwete

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages