Breaking News

Your Ad Spot

Dec 5, 2012

WENYE ULEMAVU WAKUMBUKWA


Na Mwandishi Maalum, New York
 Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, ametaka kuwapo kwa msukumo mpya wenye lengo la kujenga jamii inayothamini utofauti  baina ya watu na ushirikishwaji.
Ban Ki Moon ameyasema  hayo katika  k salamu zake wakati wa maadhimisho ya  siku ya Kimataifa ya watu wenye ulemavu. Maadhisho hayo hufanyika kila desemba tatu.
Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa  ameeleza kuwa, kwa kutambua nafasi  na mchango wa watu wenye ulemavu katika sekta mbalimbali, ndiyo maana Umoja wa Mataifa umeandaa  mkutano wa kilele wa wakuu wa  nchi na serikali,  mkutano ambao utajadili kwa kina masuala ya watu wenye ulemavu na maendeleo.
 “Maadhamisho haya ya leo “. Akasema   Ban Ki Moon,  “ Ni mwanzo wa maandalizi ya mkutano huo wa kilele  kwa lengo hasa la kuchochea  na kuhakikisha kwamba haki, mahitaji na mchango wa watu wenye ulemavu vinazingatiwa kwa ukamilifu.
Mkutano huo utafanyika   Septemba 23  mwaka 2013 ikiwa ni sehemu ya  Mjadala Mkuu wa Baraza Kuu la 68 la Umoja wa Mataifa.  kufanyika kwake kunatokana na mchango na msukumo mkubwa  uliofanywa na  Balozi za Tanzania na Ufilipioo katika Umoja wa Mataifa wa kuandaa na kusimamia majadiliano yaliyozaa maazimio mbalimbali ambayo hatimaye yalijenga ushawishi mkubwa wa kuwa na mkutano huo katika ngazi ya viongozi wakuu wa nchi na serikali.
Maazimio hayo   likiwamo lililopitishwa hivi karibuni, yanahimiza pamoja na mambo mengine, ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu katika shughuli  na maamuzi  yanayohusu masuala ya maendeleo ikiwamo utekelezaji wa malengo ya maendeleo ya millennia.
Aidha maamizio hayo yanazihimiza serikali na taasisi za kimataifa    kuwa na mipango madhubuti na endelevu ya ukusanyaji wa raslimali zitakazohakikisha ushiriki wa  kundi hilo la jamii  na  halikadhalika maazimio hayo yanaisisitiza pia haja na umuhimu  wa kuwa na taarifa na takwimu sahihi za watu wenye ulemavu.
Katika maadhimisho yaliyofanyika hapa Makao Makuu   yakiambatana pia na mijadala mbalimbali, Ban Ki Moon anasema  watu wenye ulemavu wana mchango mkubwa katika jamii. Na kwamba wanaweza kufanya vizuri zaidi ikiwa vikwazo vinavyokwamisha ushiriki wao vitaondolewa.
Aidha Ban Ki moon  ameeleza kwamba  changamoto kubwa ni katika utoaji wa fursa  sawa na ukidhi wa mahitajio  ya msingi ya watu wenye ulemavu.
“ kwa umoja wetu lazima tuhakikishe kwamba tunajitahidi kutekeleza  malengo ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Watu wenye Ulemavu.  Kuondoa ubaguzi na kutoshirikishwa, na kujenga jamii ambayo inathamini na kuhimiza ushirikishwaji” akasema Ban Ki Moon.
Inakadiriwa kwamba watu bilioni moja sawa na  asilimi 15 ya  idadi ya watu wote  duniani wanaishi na aina moja ama nyingine ya ulemavu.
Umoja wa Mataifa umekuwa ukiadhimisha siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu tangu mwaka 1992, na   mwaka 2007 ulipitishwa  Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa  Haki za Watu wenye  Ulemavu na ukaanza kufanya kazi mwaka 2008.
Mkataba huo pamoja na mambo mengine unatambua vikwazo  vinavyowakabili watu wenye ulemavu   kwa sababu tu ya ulemavu wao, na kwa sababu hiyo Mkataba  unatamka  kwamba watu wenye ulemavu wana haki ya msingi ya kupata elimu  jumuishi.
Hadi kufikia mwezi Novemba mwaka huu nchi 126  sawa na theluthi mbili   ya wanachama 193 wa Umoja wa Mataifa zilikuwa zimeuridhia  Mkataba huo. 

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages