Breaking News

Your Ad Spot

Jun 21, 2013

BUSH NA MKEWE KUJA TANZANIA MWEZI UJAO

GEORGE BUSH
DAR ES SALAAM, Tanzania
Rais mstaafu wa Marekani, George W. Bush na mkewe, Laura, wanatarajiwa kuwasili nchini mwezi ujao ambapo watahutubia kongamano litakalojadili wajibu wa wake za marais katika kuinua wanawake duniani.

Taasisi ya George Bush  ndiyo imeandaa kongamano  hilo litakalofanyika Dar es Salaam kuanzia Julai 2 hadi 3.

Taarifa iliyotolewa jana na taasisi hiyo kwa vyombo vya habari, ilisema kongamano hilo, litahudhuriwa pia na mke wa Rais Barack Obama wa Marekani, Michelle na  muasisi wa Taasisi ya Wanawake ya Cherie, Cherie Blair ambaye ni mke wa Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza, Tony Blair.

Wake wengine wa marais wa Afrika watakaohudhuria ni Mama Salma Kikwete, Chantal Campaore wa Burkina Faso, Roman Tesfaye wa Ethiopia, Maria da Luz Dai Guebuza (Msumbiji),  Penehupifo Pohamba (Namibia), Sia Nyama Koroma (Sierra Leone), Janet Museveni (Uganda) na Christine Kaseba wa Zambia.

Kongamano hilo litajikita zaidi katika kujadili masuala ya kuwekeza kwa wake, kuimarisha Afrika lakini pia wajibu wa wake za marais  kuhamasisha wanawake katika maeneo ya elimu, afya na kuwakwamua kiuchumi.

“Kongamano hili litakutanisha pamoja wake za marais, maofisa wa Serikali, mashirika binafsi, Asasi Zisizo za Serikali (AZISE) na wasomi kujadili mambo muhimu ya kuchukuliwa hatua ili kunufaisha wanawake,” ilisema taarifa hiyo.

Aidha, mada zitakazowasilishwa na kujadiliwa katika kongamano hilo ni kuinua wajasiriamali wanawake kiuchumi kupitia mafunzo na teknolojia, kupatia fursa wanawake wakulima kwa kupewa mafunzo ya kilimo cha kisasa, mafunzo kuhusu saratani ya matiti na umuhimu wa elimu kwa wanawake.

Kongamano hilo linafanyika sambamba na ujio wa Rais Obama anayetarajiwa kuwasili nchini mwanzoni mwa mwezi ujao.

Tanzania ni miongoni mwa nchi za Afrika ambazo kiongozi huyo atazuru katika ziara itakayoanza Juni 26 hadi Julai 2. Nchi nyingine ni Senegal na Afrika Kusini.

Ziara za kiongozi huyo na Bush, inafanya Tanzania mwaka huu kushuhudia ugeni wa watu mashuhuri mfululizo, baada ya Rais Xi Jiping wa China Machi 28, ambapo Tanzania ilikuwa nchi ya kwanza kutembelea Afrika tangu achaguliwe kuwa Rais Machi 14.
Amani, utulivu na uimara wa mfumo wa demokrasia  ni miongoni mwa mambo yanayotajwa kuvutia viongozi hao wa kimataifa kuja nchini.

Wapo  wengine ambao katika maoni yao juu ya ujio wa viongozi hao, wamekuwa wakisema ugunduzi wa rasilimali za asili kama vile gesi, mafuta na madini ya urani ni sababu nyingine ya Tanzania kutembelewa.

Hata hivyo, Balozi wa Marekani nchini, Alfonso Lenhardt alikaririwa hivi karibuni akifafanua, kwamba ziara ya Obama haina ajenda yoyote ya kuchukua rasilimali za Tanzania, bali ni ya uhusiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages