Breaking News

Your Ad Spot

Dec 17, 2013

SABA WASHIKILIWA NA POLISI KWA MAUAJI YA ALIYEKUWA MWENYEKITI WA CCM MKOA WA MWANZA

Marehemu Mabina alivyouawa
MWANZA, Tanzania 
Watu saba wanashikiliwa na Polisi mkoani Mwanza kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya kinyama ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Mwanza na Diwani wa Kata ya Kisesa, Clement Mabina.

Watuhumiwa hao wamekamatwa kwa nyakati tofati wakiwemo wakazi wa maeneo ya Kata ya Kanyama yalikofanyika mauaji hayo na kundi la watu kwa kile kilichoelezwa kuwa mgogoro wa mashamba.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Mwanza, Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Valentino Mulowola, akizungumza na waandishi wa habari kwa njia ya simu, alisema hadi sasa watu saba wanashikiliwa na jeshi hilo.

Alisema watuhumiwa hao walikamatwa juzi na jana na kwmba jeshi hilo linaendelea kuwatafuta watuhumiwa wengine wanaodaiwa kuhusika katika mauaji ya Mwenyekiti huyo wa Chama wa awamu iliyopita.

“Tunaendelea na upelelezi wa mauaji hayo ya kinyama nay a kujichuklulia sheria mkononi ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa wahusika na kuna maendeleo mazuri, tayari watu saba tunawashikilia kwa kuhusika na mauaji hayo,” alieleza Kamanda Mulowola

Katika tukio hilo la mauaji, Mabina aliuawa kwa kukatwa mapanga na kupigwa kwa mawe na mwili wake ulikutwa na majereha makubwa kichwani kisogoni.

Kabla ya kuawa na wananchi  hao, marehemu anadaiwa kumpiga risasi mtoto Temeli Malimi (12) kwa bahati mbaya wakati akijihami na mashambulizi ya wananchi hao.

Kamanda Mulowola alieleza jana kwamba, marehemu alikutwa akiwa na bunduki moja aina ya Shot Gun na bastola moja ambayo hakutaja aina yake.

Hata hivyo ndugu wa marehemu akiwemo msemaji wa familia Timoth Gregory, wanailaumu mitandao ya kijamii kwa kupotosha ukweli na kumpaka matope marehemu na hivyo kuomba waandishi wa habari waripoti ukweli na siki kuyafanya mauaji hayo kuwa mtaji wa kisiasa.

Habari kutoka katika eneo la tukio zimedai kuwa, mmoja wa watuhumiwa waliokamatwa alikutwa na simu ya mkononi ya marehemu Mabina.
  
Habari hizo zimedai kuwa, kundi linalosadikiwa kuhusika na mauaji hayo lilijiandaa kufanya kitendo hicho cha kinyama kutokana na mvutano wa eneo la mlima huo. 

Kamanda huyo wa polisi hakutaka kutaja majina ya watuhumiwa hao kwa madai ya kuwa kuyataja kungeweza kuvuruga upelelezi wa jeshi lake.  

 Gregory alisema jana kuwa, taratibu za mazishi bado zinaendelea ikiwa ni pamoja na kuwasubili watoto wawili wa marehemu walioko nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages