Breaking News

Your Ad Spot

Feb 26, 2014

NEW YORK YAMJADILI TENA TEMBO. MJADALA WAONGOZWA NA CHELSEA CLINTON, TANZANIA YASHIRIKI

Na Mwandishi Maalum, New York
 Zikiwa zimepita  wiki  chache tangu  kufanyika kwa  Mkutano  uliojadili kwa kina  kuhusu  ujangili dhidi ya tembo na biashara haramu ya pembe za  tembo  uliofanyika Jijini London,  Uingereza, Jana Jumanne, hapa Jijini New York, Marekani, palifanyika majadiliano mengine yakihusu pia sifa na uzuri wa mnyama tembo na hatari inayomkabili.
      Majadiliano hayo na ambayo yaliwavutia washiriki  wengi, yaliandaliwa kwa ushirikiano kati ya National Geograpy na  ABC na yalifanyika katika jengo lijulikanalo kama  ABC HOME lilipo Broadway, jijini New York.
     Balozi Tuvako Manongi, Muwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, alikuwa kati ya wanajopo wanne walioalikwa kushiriki majadaliano hayo ambayo yaliongozwa na Chelsea Clinton, Makamu Mwenyekiti wa Clinton Foudantion.
     Wanajopo wengine walikuwa ni Bw. Josh Ginsberg  kutoka Wildlife Conservation Society, Bw. John Heminway mwandishi na mtengeneza filamu ambaye pamoja na mwanajopo mwingine Bryan Christy wameshiriki katika kutengeneza filamu ijulikanayo kama “The  Battle for Elephants” filamu hii inatarajiwa kuonyeshwa february  27 kupitia Channel ya National Geograpy.
      Wanajopo hao wakiongozwa na Chelsea Clinton, walipata fursa ya kila mmoja wao kuelezea nini yeyé  kama mtu binafsi au kupitia taasisi anayoiwakilisha ametoa mchango  gani katika suala zima la uhifadhi wa Tembo na uthibiti wa  mauaji holela ya  Tembo na  biashara haramu   ya pembe za tembo.
       Balozi  Manongi kwa upande  wake, alielezea  juhudi mbalimbali ambazo serikali inafanya katika  kukabiliana na  ujangili dhidi ya tembo, pamoja na biashara haramu  ya pembe , aidha alielezea dhamira na nia ya serikali  ya  kuendeleza  mapambano  ya kuwanusuru tembo kupitia awamu ya pili ya  Operesheni Tokomeza.
      Balozi pia alijibu maswali mbalimbali na kutolea ufafanuzi hoja zikiwamo  kuhusu  kwanini operesheni tokomeza ilisitishwa,  na  je serikali  ilikuwa na mpango gani kuhusu shehena ya pembe za ndovu ambayo iko katika maghala.
       Kwa ujumla wanajopo wote walikubaliana kwamba, mapambano dhidi ya  ujangili na biashara haramu ya pembe za ndovu ni vita  ngumu  hasa ikizingatiwa kwamba mtandao unaohusika na biashara ya pembe za  tembo ni mpana sana na unaohusisha watu wengi.
        Na kwa sababu hiyo wamehimiza mambo kadhaa  yakiwamo,  ushiriki wa wadau kutoka makundi mbalimbali ya  kijamii kitaifa na kimataifa,  udhibiti wa soko na  hitajio la pembe za ndovu, utoaji wa elimu kwa umma, uwezeshwaji wa watendaji katika ngazi mbalimbali,  na uimarishaji wa sheria.

Muwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa  Mataifa, Balozi Manongi, akielezea jambo wakati  wa majadiliano kuhusu tembo na changamoto  zinazomkabili. Balozi Manongi alitumia fursa hiyo kuelezea juhudi mbalimbali zinazofanywa na Serikali katika kukabiliana na vitendo vya ujangili na udhibiti wa biashara haramu ya pembe za tembo. Kwa picha zaidi Bofya Hapa

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages