Breaking News

Your Ad Spot

May 24, 2014

TAARIFA KWA UMMA KUHUSU UPOTOSHWAJI WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA AFYA NA USTAWI WA JAMII

TAARIFA KWA UMMA KUHUSU UPOTOSHWAJI WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE.

Wizara ya Afya na Ustawi wa jamii inapenda kutoa ufafanuzi kuhusu taarifa mbalimbali za upotoshaji unaofanywa kupitia baadhi ya mitandao ya kijamii, simu za mikononi na mikusanyiko ya watu kuwa ugonjwa wa Dengue haupo nchini Tanzania.

Wizara inapenda kusisitiza kwamba, ugonjwa huo upo nchini na serikali kwa kushirikiana na wananchi inaendelea kutekeleza hatua mbalimbali za kukabiliana nao. Ikumbukwe ugonjwa huu unapatikana pia katika nchi nyingi duniani zilizoko katika ukanda wa joto na unaathiri takribani asilimia 40 ya watu duniani.Takwimu za Shirika la Afya Duniani zinathibitisha kuwa takribani watu milioni 5 wanaripotiwa kuugua ugonjwa wa kila mwaka.

Wizara inasisitiza na kuikumbusha jamii kwamba hakuna dawa maalumu ya ugonjwa wala chanjo bali mgonjwa anatibiwa kutokana na dalili zitakazo ambatana na ugonjwa huu kama vile homa, kupungukiwa maji au damu.

Jinsi ya kujikinga na ugonjwa wa homa ya Dengue
o   Kuangamiza mazalio ya mbu
ü Fukia madimbwi ya maji yaliyotuama  au nyunyuzia viuatilifu vya kuua viluwiluwi  vya mbu kwenye madimbwi hayo
ü Ondoa vitu vyote vinavyoweza kuweka mazalio ya mbu kama vile: vifuu vya nazi, makopo, magurudumu ya magari yaliyotupwa hovyo, nk.
ü Fyeka vichaka vilivyo karibu na makazi ya watu
ü Hakikisha maua yanayo pandwa kwenye makopo au ndoo hayaruhusu maji kutuama
ü Funika mashimo ya maji taka  kwa mfuniko imara
ü Safisha gata za paa la nyumba ili kutoruhusu maji kutuama

o   Kujikinga na kuumwa na mbu
ü Tumia viuatilifu vya kufukuza mbu “mosquito repellants”
ü Vaa nguo ndefu kujikinga na kuumwa na mbu
ü Tumia vyandarua vilivyosindikwa viuatilifu (kwa wale wanaolala majira ya mchana na hasa kwa watoto)
ü Weka nyavu kwenye madirisha na milango ya nyumba za kuishi

Wizara inawakumbusha wananchi wa Tanzania kuwa, huu ni muda muafaka wa kuzingatia utunzaji bora wa mazingira yetu. Tukitunza mazingira yetu, nayo yatatutunza na kutuepusha na maradhi yanayoambatana na mazingira machafu.


Nsachris Mwamwaja
Msemaji wa wizara
23 mei 2014

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages