Breaking News

Your Ad Spot

Jan 15, 2015

TANGO KUWA NA MKUTANO WA HADHARA MNAZI MMOJA LEO KUJADILI MALENGO YA SDGS

DSC_0589
Meneja wa sera na ushirikishaji wa TANGO, Zaa Twalangeti, akizungumza na Modewjiblog kwenye mahojiano maalum yaliyofanyika katika ofisi za TANGO jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mratibu wa kitaifa wa Mtandao wa Asasi zisizo za kiserikali za haki za binadamu kusini mwa Afrika(SAHRINGON), Bi. Martina Kabisama.
Na Mwandishi wetu
ASASI isiyokuwa ya kiserikali ya TANGO imezindua kampeni kubwa ya kuelimisha umma wa Tanzania kuhusu malengo 17 ya maendeleo endelevu kwa lengo la kuyafanya kumilikiwa na wananchi ili yapigane kuondoa umaskini na kuleta ustawi wa jamii.
Uzinduzi huo ulifanyika mjini Dar es salaam.
Aidha katika uzinduzi huo wamesema kwamba ili kutoa nafasi ya sauti za wananchi kusikika na kufikishwa kwa viongozi wa kimataifa ambao watakutana baadae mwaka huu, asasi zisizokuwa za kiserikali zitaitisha mkutano mkubwa ambapo watu wa kawaida wataambiwa wasema wanachohitaji, shughuli itakayofanyika viwanja vya Mnazi Mmoja Januari 15 mwaka huu kuanzia saa tatu asubuhi.
Kwa mujibu wa Meneja wa sera na ushirikishaji wa TANGO, Zaa Twalangeti,kuanzishwa kwa kampeni hiyo kabla ya kuanza kwa utekelezaji wake mwakani kwa miaka 15 kumefanyika baada ya kutambua kasoro zilizojitokeza katika kampeni ya malengo ya milenia (MDG) ambayo ushiriki wa wananchi haukulengwa na matokeo yake kuna kasoro katika utekelezaji.
Alisema ingawa malengo ya milenia yalikuwa manane, kasoro iliyoijitokeza ambayo inasababisha utekelezaji wake kuwa wa chini ni hali ya kuwatumia viongozi kuyazungumza na kuyatekeleza kiasi cha kufanya wananchi wasione kama ni mali yao.
Alisema haja ya kupata mafanikio katika malengo yaliyofikiriwa sasa ambayo ni 17 inatokana na kutaka wananchi kuyajua, na pia kusema wao katika malengo hayo 17, ambayo yatafanyiwa kazi na Umoja wa Mataifa Oktoba mwaka huu kabla ya kuanikwa wazi kwa jamii ya kimataifa, yapi wanayataka na kipaumbele chao nini.
Aidha alisema kwamba malengo hayo ni muongozo wa dunia wa kupunguza umaskini na kwamba wakati mataifa mengine yamefurahisha ushiriki wa wananchi kuanzia ngazi za chini hadi juu , watanzania wamejikuta hawajui wala kufikiria kuyatekeleza kutokana na ukweli kuwa hawakushirikishwa na hivyo malengo hayo hayakuwa yao bali ya viongozi.
Alisema kiukweli muongozo huo wa awali wa kukabili umaskini (MDGs) haukuweza kufikiwa na watanzania kwani hata upunguzaji wa umaskini umefanyika kwa asilimia 3 tu, huku tatizo la vifo vya wajawazito na watoto likiwa tatizo na elimu kubaki kuwa ya kubabia kutokana na matatizo lukuki yaliyozunguka elimu kufuatia kukosekana kwa tathmini.
DSC_0601
Mratibu wa kitaifa wa Mtandao wa Asasi zisizo za kiserikali za haki za binadamu kusini mwa Afrika(SAHRINGON), Bi. Martina Kabisama akifafanua jambo kwa mwandishi wa Modewjiblog wakati wa mahojiano maalum katika ofisi za TANGO jijini Dar es Salaam.
"umefikia lengo la kuandikisha, lakini mbona unazalisha watu wasiojua kuandika, kusoma na kuhesabu;mbona mdondoko ni mkubwa" alisema.
Alisema kampeni ya kuelewa malengo hayo ambayo wameiita Action 2015 yamelenga kuhakikisha kwamba malengo ya sasa ni vyema yakamilikiwa na wanananchi ili watafute dawa ya changamoto zinazowakabili.
Tawalangeti alisema kufikisha ujumbe kwa wananchi watatumia mikutano,makongamano, majadiliano, vipindi vya mazungumzo katika radio, televisheni na mitandao ya kijamii.
Sisi kama watanzania lazima tuupige vita umaskini, tunaupigaje vita? unasema pato limekua. limekuaje kama pengo kati ya matajiri na maskini linazidi kuongezeka? alisema Martina Kabisama ambaye aliongeza kwamba hata maisha yanaonesha kuongezeka kwa umaskini kwa sababu sasa kuna majengo ya bati vijijini lakini hakuna chakula.
Alisema zamani unakuta nyumba mbaya lakini kuna kuku , kuna maziwa kuna chakula cha kutosha tukasema kuna umaskini ulikithiri leo hii unaenda hukohuko vijijini kuna nyumba nzuri lakini nyumba hiyo haina mifugo wala akiba ya chakula.
Aidha kuonesha kutopea kwa umaskini pia alitolea mfano wa elimu ambapo alisema wakati zamani wakubwa wenye hela na viongozi walikuwa wakifanya kila hila kuhakikisha watoto wao wanaenda shule za serikali, siku hizi hawahangaiki kwa kuwa wanatumia uwezo wao kupeleka watoto katika shule za kulipia wakiacha shule za serikali magofu.
DSC_0578
Meneja wa sera na ushirikishaji wa TANGO, Zaa Twalangeti akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na mtandao wa habari wa Modewjiblog jijini Dar es Salaam.
Martina Kabisama, ambaye ni mratibu wa kitaifa wa Mtandao wa Asasi zisizo za kiserikali za haki za binadamu kusini mwa Afrika (SAHRINGON) alisema kampeni imelenga kuweka msingi imara wa mambo yanayotakiwa kufanywa huku wananchi wakiyaelewa.

Alisema miaka 15 ya malengo ya maendeleo endelevu kuanzia mwakani hadi mwaka 2030 bila kuwa na mipango madhubuti na wananchi kukumbatia malengo yenyewe kwa kuyafanya yao na kufuatilia utekelezaji wake kwa namna wanavyohitaji hasa kutokana na ukweli kuwa mwaka huu Tanzania imepata bahati ya kuwa na matukio mawili makubwa yanayoashiria maamuzi mazuri kusaidia msingi wa maendeleo.
Mambo hayo mawili ni katiba pendekezwa na pia uchaguzi mkuu.
Alisema matukio hayo mawili yatasaidia sana kujua nani wanawekwa madarakani ili kama maamuzi yalikuwa mazuri inakuwa rahisi kudai utekelezaji wa malengo hayo kama yalivyoeleweka.

Alisema ni muhimu kuelewa malengo endelevu ya maendeleo kwa kuwa hatima ya Watanzania ipo mikononi mwa watanzania wenyewe pamoja na maelekezo ya jumuiya ya kimataifa na viongozi waliopo nchini.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mwishoni mwa mwaka huu viongozi wa kimataifa watakutana kujadili malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) baada ya kukamilisha malengo ya milenia ambayo hata hivyo bado kuna mataifa yanahitaji kuendelea kutoka pale yalipoishia.

TANGO wamesema moja ya mambo muhimu ambayo wanafikiria yanastahili kufanyiwa kazi ni kuendelezwa kwa MDG1 ya kuondoa umaskini uliokithiri na njaa na MDG8 ya namna ya utekelezaji. Alisema malengo hayo, bado yapo kizani na ikizingatiwa kwamba malengo ya maendeleo endelevu yanatakiwa kushirikisha wananchi.

Pamoja na ushirikishaji wa wananchi TANGO imesema kwamba malengo ya SDGs yanahitaji serikali kuwa na dhamira ya kukabiliana na umaskini kwa kushirikisha wadau wote, huku bunge ambalo husimamia sera na utekelezaji wa sheria likiwezeshwa kutekekeza wajibu huo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages