Breaking News

Your Ad Spot

Jun 2, 2015

TUWALINDE ALBINO WETU KWA KUWAAJIRI

download (6)
*Azim Dewji aanza kuajiri, kujenga kituo maalumu Mwanza
*Kwa kuanzia atenga sh milioni 100 kulea watoto albino
WATANZANIA wenye ulemavu wa ngozi (albino) wapatao 76 wameuawa, na wengine wanaokaridiwa kufikia 34 wameachwa na ulemavu wa kudumu kutokana na viungo vyao mbalimbali kukatwa katika mashambulizi yanayoashiria ushirikina uliokithiri.
Mauaji na mashambulizi hayo yamefanyika kwa wingi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa, kati ya kipindi cha kuanzia mwaka 2005/2006 mpaka  mwaka huu. Yalitulia kidogo kati ya mwaka 2012 na 2013, lakini mwaka huu yameibuka upya. Mikoa inayotajwa sana kwa matukio haya ni Mwanza, Tabora, Kagera, Mara na Geita.
Kuanzia mwaka 2006 mpaka mwaka huu, jumla ya mashauri 35 yanayohusu mauaji na mashamnbulizi hayo yamefikishwa katika mahakama ambako watuhumiwa 139 walishitakiwa, 15 wakapatikana na hatia huku 73 wakiachiwa huru kutokana na ushiriki wao kukosa ushahidi wa kutosha.
Hatua kadhaa zimechukuliwa kujaribu kuwalinda ndugu zetu albino. Katika Kanda ya Ziwa pekee, Polisi imewatia nguvuni waganga wa kienyeji 225 ikiwatuhumu kuhusika katika matukio ya mauaji hayo. Kadhalika wigo wa kusaka watuhumiwa umepanuliwa hadi kufika katika mikoa ya Simiyu, Shinyanga, Katavi na Rukwa.
Viongozi wetu, wa kila nyanja, akiwamo Rais Jakaya Kikwete, wamejitokeza kukemea uovu huu. Rais amekaririwa akisema kwamba hataachwa mtu yeyote anayeshiriki katika mauaji haya.   
Desemba 14, mwaka jana mjini Dar es Salaam, akizungumza katika Harambee ya Kusaidia Watoto Wenye Ulemavu wa Ngozi wa Kituo cha Buhangija, Shinyanga,  Waziri Mkuu Mizengo Pinda, alieleza kwamba takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zilikuwa zinaonesha kwamba Tanzania ina walemavu wa ngozi wapatao 170, 000.
Lakini akaongeza kwamba ni vigumu sana kupata takwimu za hakika za walemavu hawa kwa vile wengine hufichwa wanapozaliwa, na wengine wanazaliwa katika maeneo ya mbali ambako taarifa zao haziwezi kufahamika kwa urahisi.
Pinda amekuwa mara kwa mara akishiriki kuelimisha jamii iwalinde albino. Yeye mwenyewe analea albino kadhaa. Huko  nyuma alipata kutoa machozi bungeni, akielezea kusikitishwa kwake na mauaji hayo.
Tayari Jaji Mkuu, Othman Chande, ameahidi kwamba mahakama itatoa kipaumbele kwa kesi zinazohusu na mauaji ya albino akieleza kwamba mauaji hayo yanakiuka haki za binadamu.
Sasa kila Mtanzania mwenye mapenzi na nchi yetu anafahamu ni kwa jinsi gani mauaji haya yalivyolipaka matope Taifa. Anafahamu aibu ambayo imelifika Taifa kutokana na vitendo vya baadhi yetu kufikiri kwamba viungo vya albino vinaweza kuwafanya wawe matajiri!
Hizo si fikra za kweli. Hakuna njia ya mkato kuelekea kwenye utajiri. Hatuna matajiri wengi hapa Taazania, na hao wachache tunaowaona, mali zao zimetokana na jasho na jitihada zao kubwa. Wengine tumo kwenye biashara kwa zaidi ya miaka 30 sasa, na bado hatuwezi kujiita matajiri.
Mauaji haya, yana sababu nyingi, lakini mimi naona kwamba sababu kubwa ni elimu ndogo. Hakika kama mtu uelewa wake ni mdogo kiasi cha kufikiri kwamba kiungo cha albino kinaweza kumpa utajiri, hata akiweza kupata hiyo mali hataweza kudumu nayo kwa sababu hiyohiyo ya elimu duni.
Nimeomba nikutane na waandishi wa habari ili kwa pamoja tujaribu kutafuta suluhisho la mauaji haya ya albino. Njia ya kuanzia, kwa maoni yangu, ni kuwajua wako wapi.
Mimi, familia na kampuni yangu ya Simba Trailer Manufacturers Ltd tumejaribu. Tumeajiri mmoja wa hawa ndugu zetu. Yeye sasa ni sehemu ya familia yetu pana kama kampuni. Nimekuja naye hapa. Anaweza baadaye kutoa ushuhuda. Lakini mipango yetu kama kampuni ni kuajiri walau wawili wengine.
Maoni yetu ni kuwa kama kila mtu mwenye kampuni, si lazima iwe kampuni kubwa, angeajiri walau albino watatu, tungekuwa nao karibu.
Natoa mwito kwa Watanzania wote wenye uwezo wa kuajiri watu watatu na zaidi, kuwaajiri ndugu zetu albino. Kwa kufanya hivyo tutakuwa tumepunguza sana uwezekano wa wao kuwindwa kama vile si binadamu. Makampuni 350 yakiajiri kila moja angalau albino watatu, tutakuwa na uhakika wa kuingiza albino zaidi ya 1000 katika ajira rasmi, hii ni kwa kuanzia.
Kadhalika  nina mpango wa kujenga  kituo mkoani Mwanza ambacho kitaweza kuhifadhi albino 100  kwa wakati mmoja pia tutakuwa tunawahudumia chakula na mavazi.vile vile tutaomba serekali ya mkoa kuwapatie shule na sisi upande wetu tuta wapa usafiri.
Kutokana na dhamira hiyo ambayo nimeitengea sh milioni 100 kwa kuanzia, namuomba Mkuu wa Mkoa wa Mwanza atutengee angalau ekari kumi za ardhi kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho. Itapendeza zaidi kama kitakuwa karibu na eneo la barabara kuu na pia karibu na huduma muhimu zikiwemo za maji na umeme.
Shime Watanzania, hasa wafanyabiashara tuungane katika hili. Tumevuka mengi, hakika hata hili la mauaji ya albino tutalishinda.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages