Breaking News

Your Ad Spot

Jul 7, 2015

SAKATA LA WALIMU KUFANYIWA MAPENZI KWANJIA YA USHIRIKINA LACHUKUA SURA MPYA


SAKATA la walimu wa Shule ya Msingi Nambaza, katika Wilaya ya Bunda, mkoani Mara, kufanyiwa vitendo vya kishirikina na kutishiwa maisha, limeendelea kuumiza vichwa vya viongozi wilayani humo.

Viongozi hao, leo wanatarajia kukutana katika kikao ambacho kitamshirikisha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya, Ofisa Utumishi na Ofisa Elimu wa Wilaya hiyo ili kujadili hatima ya walimu wa shule hiyo ambao wote wamefungasha mizigo yao na kutoweka kijijini hapo wakihofia kuuawa na baadhi ya ndugu wa watuhumiwa.

Kaimu Ofisa Elimu wa Wilaya hiyo, Bw. Ruben Kaswamila, amesema kuwa kikao hicho pamoja na mambo mengine, pia kitajadili tukio zima la Nambaza ambalo ni la aibu na kushangaza ili kuangalia uwezekano wa kuwahamisha walimu wote wageni na kuwapangia vituo vingine.

"Kesho (leo) tutakuwa na kikao ambacho kitamhusisha Mkurugenzi, Ofisa Utumishi na mimi Kaimu Ofisa Elimu ili kujadili suala zima la Nambaza na hatima ya walimu wa shule hiyo waliodhalilishwa.
 
"Mwelekeo wa kikao ni kuwahamisha walimu wote wageni na kuwapangia vituo vingine vipya vya kazi kwani kuendelea kuwaacha hapo ni kuwahatarishia maisha maana hata kisaikolojia hawawezi kufundisha shuleni hapo kwa ufanisi," alisema.

Alisema uhamisho huo hautawahusu walimu watatu wa shule hiyo, Bw. Sospeter Mafuru ambaye ni Mwalimu Mkuu, Bw. Medard Munaku anayestaafu Juni, 2016 na Bw. Renatus Molla ambaye naye anastaafu Februari, 2016 ambao ni wazaliwa wa kijiji hicho ambao watabaki hapo shuleni kuwafundisha watoto.

Aliongeza kuwa, Serikali ya kijiji na wanakijiji kwa ujumla watatafuta wenyewe walimu ili waongeze nguvu shuleni hapo.

"Kwakuwa wanakijiji ndio waliosababisha hayo, watafute wenyewe walimu wa kuwafundishia watoto wao kama ni wanafunzi waliomaliza kidato cha nne na cha sita wakubaliane, mshahara wawalipe wao kwa sababu walimu walioletwa na Serikali, hawahitajiki kijijini," alisema.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, walimu wazawa kijijini hapo ambao inadaiwa ndio watabaki kufundisha watoto, walisema hawako tayari kurudi kufundisha shuleni hapo na kama mwajiri alikuwa na mpango wa kuwafukuza kazi afanye hivyo si kurudi Nambaza.

Bw. Mafuru alisema jana alifuatwa na watu ambao walimtukana, kumtemea mate na kutishia kumuua tukio ambalo ameliripoti polisi sasa kwanini aendelee kukaa kijijini hapo.

"Mimi ni mzawa wa kijiji hiki lakini ni mtumishi wa Serikali kama walivyo watumishi wengine, utumishi wangu ndio umesababisha nitendwe vibaya, nitishiwe kuuawa na kuonekana sifai na adui miongoni mwa wanakijiji, natishiwa sasa iweje niendelee kuwepo kijijini.

"Nambaza sitakiwi tena nitauawa, uhai wa maisha yangu ni bora kuliko kazi, kama mwajiri anataka kunifukuza kazi afanye hivyo lakini siwezi kurudi Nambaza kufundisha," alisema.

Kwa upande wake, Molla alisema, hawezi kurudi kufundisha Nambaza kwani amevumilia mengi pamoja na kumpoteza mtoto wake katika mazingira ya kishirikina lakini bado anatishiwa kuuawa hivyo ni bora afukuzwe kazi akafanye shughuli nyingine kama mwajiri anaona kumbakiza kijijini hapo atakuwa amemtendea haki kwa sheria za utumishi.

"Sitarudi Nambaza, nipo tayari kufukuzwa kazi, mizigo na familia yangu nimeitoa Nambaza baada ya kutendwa vibaya na wanakijiji, nimetishiwa kifo na hao hao wanakijiji, kurudi hapo ni kwenda kufa, siwezi kufuata kifo ninachokiona hadi Mwenyezi Mungu atakapoamua," alisema.

Aliongeza kuwa, mwaka 2014 mwanaye alikufa katika mazingira ya kutatanisha kishirikina kwani hakuugua bali alianguka njiani akitembea na kufa papo hapo.

Mwalimu Munaku, ambaye tayari amekwishajiondosha kijijini hapo akihofia kuuawa kutokana na vitisho kutoka kwa wanakijiji, hakuweza kupatikana ili kuzungumza kama yuko tayari kuendelea kufundisha shuleni hapo ama la.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages