Breaking News

Your Ad Spot

Sep 25, 2015

MO AMPIKU DANGOTE MFANYABISHARA BORA AFRIKA

 MO dewji
Vinara wa biashara Afrika walipewa tuzo mbalimbali za African Business katika picha ya pamoja. Kuanzia kushoto ni Daphne Mashile Nkosi, Strive Masiyiwa, Helen Hai na Mohammed Dewji . hafla ya utoaji wa tuzo hizo ilifanyika hoteli ya Four Seasons Hotel mjini New York.(Picha na African Business).


Na Mwandishi wetu, New York
MTANZANIA Bilionea Mohamed Dewji amepata tuzo ya Mfanyabiashara Bora wa Afrika wa mwaka 2015, katika kinyang’anyiro cha tuzo za wafanyabiashara bora wa Afrika (African Business Awards 2015).
Dewji maarufu kama Mo alikabidhiwa tuzo hizo usiku wa kuamkia jana mjini New York.
Katika hafla hiyo iliyofanyika katika hoteli ya Four Season mkabala na jengo la Umoja wa Mataifa (Baraza Kuu) watu wengine waliopata tuzo ni Aliko Dangote, Daphne Mashile Nkosi, Strive Masiyiwa na Helen Hai.
MO alimshinda Aliko Dangote ambao walikuwa kwenye Kategori moja wakiwania tuzo hiyo ya mfanyabiashara bora wa Afrika, huku wengine walioshindanishwa kwenye kategori hiyo ni CEO wa Paramount Group, Ivor Ichikowitz, CEO wa Groupe Loukil, Groupe UADH, Bassem Loukil, na Oscar Onyema DG wa Nigerian Stock Exchange.
Tuzo hizo zimeandaliwa na jarida la African Business .
Pia katika tuzo hizo taasisi kadhaa zinazofanya vyema bara la Afrika zilitambulika. Taasisi hizo ni pamoja na kiwanda cha sementi cha Dangote , Guaranty Trust Bank, Abellon Clean Energy, Nigerian Stock Exchange na taasisi ya bima kwa masoko yanayochipukia ya BIMA.
Akielezwa wasifu wake katika hafla hiyo, Mo ameelezwa kama mfanyabiashara aliyefanikiwa kutokana na kuongeza kipato na ukubwa wa kampuni ya Mohammed Enterprise toka aitwae kutoka kwa baba yake.
Akiwa mtendaji wa kampuni hiyo, akiwa katika miaka ya 40 amefanya mabadiliko makubwa katika makampuni mbalimbali ya umma yaliyoshindwa kujiendesha katika sekta ya kilimo, viwanda na maeneo ya makazi na viwanda.
Uongozi wake uliwezesha kampuni hiyo ya MeTL kufanya makubwa kiasi cha kumfanya aingie katika jarida la Forbes la matajiri wa Afrika.
Majaji waliompa tuzo kwa mwaka huu walisema kwamba uongozi wake umewezesha biashara katika kampuni hiyo kuchupa kutoka dola za Marekani milioni 30 hadi bilioni 3.
Akipokea tuzo hizo Dewji alisema kwamba tuzo hiyo ni ishara muhimu kwa waafrika wote na uwakilishi wa uhakika wa vijana katika masuala ya ujasirimali.
DSC_0310
Afisa Mtendaji Mkuu wa Makampuni ya MeTL Group, Mohammed Dewji.
Tuzo ya Biashara ya Mwaka ilienda kwa kiwanda cha saruji cha Dangote kinachoongozwa na bilionea wa Afrika, Aliko Dangote.
Kiwanda hiki kilichopo Nigeria kimejipanga kusambaza uzalishaji katika nchi nyingine za Afrika, hatua ambayo imeifanya tuzo hiyo kuwa ya kwao.
Akipokea tuzo hiyo Aliko alisema amefurahishwa sana na tuzo hiyo ya thamani kubwa na kwamba imetolewa wakati ambapo kiwanda hicho kinatanua shughuli zake kuhakikisha ukombozi wa uchumi kwa nchi za Afrika unafanyika kwa dhati.
“Tunaamini katika Afrika. Tunaamini kwamba katika kuhakikisha kuna uwekezaji mkubwa wa miundombinu Afrika itaweza kusonga mbele katika uchumi wake”.
Daphne Mashile Nkosi, Mwenyekiti Mtendaji wa kampuni ya manganisi ya Kalagadi ya Afrika Kusini alipokea tuzo mwanamke bora katika biashara. Majaji walimpa tuzo hiyo kwa kuwa ameonesha mafanikio makubwa katika sekta ambayo kwa kawaida huendeshwa na wanaume.
Mdada huyo anatambulika kwa kuwezesha kupatikana kwa ajira 30,000 huko Northern Cape, na ni muasisi wa mgodi wa aina yake katika kipindi cha miaka 30.
Mfanyabiashara wa Zimbabwe, mjasiriamali, anayependa kusaidia watu wenye mahitaji Strive Masiyiwa alipata tuzo ya mafanikio katika maisha.
CPoF_XCWcAAyCO6
Afisa Mtendaji Mkuu wa Makampuni ya MeTL Group, Mohammed Dewji akipokea tuzo yake.
Strive ambaye ni mmoja wa waanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji kwa kampuni ya kimataifa ya mawasiliano ya simu Econet Wireless amepewa tuzo hiyo kwa mafanikio yake na pia kwa misaada mingi aliyotoa kwa vijana.
Masiyiwa ametumia utajiri wake kusomesha vijana zaidi ya laki moja wa Afrika katika kipindi cha miaka 20.
“Ni heshima kuu kupata nafasi ya kuthaminiwa na jarida lako, Ni heshima kuwa miongoni mwa marafiki… tafadhali endelezeni kazi hii njema,” alisema akizungumza kwa njia ya video.
Tuzo ya mfanyabiashara wa Mfano imeenda kwa Helen Hai, Mtendaji mkuu wa Made in Africa Initiative.
Tuzo hii kwa kawaida hutolewa kwa mtu aliyetoa mchango mkubwa katika kuboresha hali ya ufanyaji biashara barani Afrika.
Helen ambaye ana asili ya China amewezesha mabadiliko makubwa katika biashara ya viatu ya Ethiopia baada ya kuanzisha kiwanda cha viatu cha Huajian Oktoba 2011 baada ya kuwa na mkutano na rais wa nchi hiyo Meles Zenawi mwaka huo huo.
Imeelezwa kuwa kiwanda hicho mara baada ya kuanzisha katika kipindi cha miezi sita tu waliweza kuongeza pato la mauzo ya nje ya nchi hiyo kwa mara mbili na katika kipindi cha miaka miwili kiliajiri waethiopia 4000.
Sasa hivi mdada huyo amefungua kiwanda cha nguo nchini Rwanda.
“Sekta binafsi haikuja Afrika kutoa msaada, tumekuja afrika kufanyabiashara. KLakini katika biashara tunatekeleza maelengo ya maendeleo. Nina imani kubwa na Afrika, naamini kupitia simulizi za mafanikio tunashawishi wengine kujiamini kutwaa uongozi na kuliwezesha bara hili kutambua fursa zake,” alisema Helen.
Guaranty Trust Bank, iliwashinda wengine kadhaa waliotajwa na kushinda tuzo ya utawala bora wakati Abellon Clean Energy ilipata tuzio ya ubinifu wakati Nigerian Stock Exchange ilipata tuzo ya urejeshaji kwa jamii faida ikiwa ni huduma bora za jamii.
Akizungumzia tuzo hizo ambazo ni za sab, Omar Ben Yedder alisema hafla hiyo imwezeshwa na Zenith Bank, GTBank, Agility na Cofina .
Washindi wa 2015
AFRICAN BUSINESS OF THE YEAR
-Dangote, Nigeria
BUSINESS LEADER OF THE YEAR
-Mohammed Dewji, CEO, Mohammed Enterprise, Tanzania
MOST OUTSTANDING WOMAN IN BUSINESS
-Daphne Mashile Nkosi, Executive Chairperson, Kalagadi Manganese, South Africa
AWARD FOR GOOD CORPORATE GOVERNANCE
-Guaranty Trust Bank, Nigeria
AWARD FOR BEST CORPORATE SOCIAL RESPONSIBILITY
-The Nigerian Stock Exchange, Nigeria
AWARD FOR INNOVATION
-Abellon Clean Energy, Ghana
INSURANCE COMPANY & INITIATIVE OF THE YEAR
-BIMA ( bimamobile.com )
LIFETIME ACHIEVEMENT AWARD
-Strive Masiyiwa
AFRICAN BUSINESS ICON
-Helen Hai

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages