Mke wa Rais Mstaafu na Mwenyekiti
wa WAMA akisalimiana na Mama Othman Chande alipowasili katika Shule ya
Sekondari Tambaza kuhudhuriaWorld Thinking Day iliyoandaliwa na Tanzania
Girl Guide Association.
Wanachama wa Girl Guide
wakiwasili katika Shule ya Sekondari Tambaza katika kusherekea World
Thinking Day ambao walipokelewa na Mgeni Rasmi Mama Salma Kikwete.
Mama Salma Kikwete akiingia
katika ukumbi wa Tambaza Sekondari akiwa na viongozi wa Girl Guide
kushoto ni Mama Symphorosa Hangi, Kamishna Mkuu na kulia ni Mama
Matilda Balama na Mkuu wa Shule ya Tambaza.
Picha ya Pamoja na Mgeni Rasmi na baadhi ya wanafunzi Wanachama na viongozi wa Girl Guide
Mama Salma Kikwete akiangalia kazi za wakinamama wajasiriamali ambao walifanya maonyesho katika sherehe hizo
PICHA NA YUSUPH BADI
………………………………………………………………………………………………………………….
Na Philomena Marijani- Meneja Uraghbishi na Mawasiliano, WAMA
Chama cha Girl Guide Tanzania
kimetakiwa kuweka mikakati ya kuhakikisha inaongeza wanachama
watakaojiunga na chama hicho ili vijana wengi waweze kunufaika
Rai hiyo imetolewa mwishoni wa
wiki na Mke wa Rais Mstaafu na Mwenyekiti wa Taasisi ya WAMA, Mama
Salma Kikwete wakati wa maadhimisho ya kilele cha siku ya World
Thinking Day yenye kauli mbiu ya Ungana, Shirikiana, Sherekea
iliyoadhimishwa na Tanzania Girl Guides Association. Sherehe hizo
zilianza kwa maandamano ya wanafunzi Wanachama kutoka Upanga katika
Makao Makuu ya Girl Guide Tanzania na kumalizikia katika Shule ya
Sekondari Tambaza ambapo sherehe rasmi ilifanyika hapo.
Akiongea katika sherehe hizo Mama
Salma Kikwete alipongeza uongozi wa Girl Guide kwa kufikia mikoa 19
ambapo mpaka sasa chama kina wanachama 97,143 na aliongeza kuwa
changamoto kubwa waliyonayo ni kuongeza Wanachama zaidi kwani Tanzania
ina watu wengi sana.
“Wito wangu kwenu ni kuongeza
juhudi ya kuwafikia vijana wengi zaidi kwani sote tunajua umuhimu wa
TGGA katika kuwasaidia vijana kujiepusha na changamoto mbalimbali katika
makuzi yao. Ni lazima tuweke malengo ya muda mfupi, kati na mrefu ndani
ya miaka mitatu ili ifikapo mwaka 2018 tuwe tumeingiza wanachama zaidi
ya 100,000/= Tumieni vizuri shule za msingi na sekondari , nina hakika
mtafanikiwa kwa kiasi kikubwa sana. ” Alisema Mama Kikwete
Mama Kikwete pia alishauri
uongozi wa Girl Guide Tanzania kubuni mbinu za kukabiliana na changamoto
kwa kutumia rasilimali walizonazo.
“Kwa kuwa TGGA ni chama kikongwe,
chenye rasilimali kama ardhi ambazo ziko sehemu nzuri kibiashara
naamini kwamba ikitayarishwa mipango mizuri mnaweza kupata wabia wenye
tija au mkawekeza kama chama kwa kushirikiana na mabenki. Mtakusanya
kodi ambazo zitasaidia uendeshaji na kuongeza uwekezaji. ”Alisema Mama
Kikwete.
Akielezea maana ya World Thinking
Day Mkufunzi wa Taifa wa Tanzania Girl Guide Association, Mama Magreth
Olumbe alisema kuwa sherehe hii ilianza rasmi mwaka 1926 ambayo ni siku
ya; kuwakumbuka Girl Guide wote duniani na hasa wale walio kwenye
mazingira magumu;kuongelea mambo yanayowagusa wasichana kwa mfano mimba
za utotoni, kuolewa katika umri mdogo; na kukumbuka mwanzilishi wa Chama
Lord Baden Powell na mke wake Olave Baden Powell.
Akisoma risala kwa Mgeni Rasmi,
Kamishna Mkuu wa Tanzania Girl Guides Association, Mama Symphorosa
Hangi alisema kuwa katika kuadhimisha World Thinking Day walikuwa na
wiki mbili za kutoa huduma kwa jamii ikiwemo kuwatembelea wagonjwa
katika hospitali ya Ocean Road na kutoa chakula, mavazi na nauli za
kuwarudishwa makwao wale waliokuwa wameruhusiwa baada ya matibabu.
Aliongeza pia walitumia muda huo kuhamasisha wasichana wengine kujiunga
na chama cha Tanzania Girl Guides ili nao waweze kupata fursa ya
kujikwamua kifikra kwa kupitia mafunzo yanayotolewa na chama.
Chama cha Girl Guides Tanzania
(TGGA) kilianzishwa hapa nchini mwaka 1928. TGGA ni chama kisicho cha
serikali na ni cha kujitolea chenye lengo la kuwaendeleza watoto wa kike
na wanawake kwa ujumla kushiriki katika maswala ya kijamii na kiuchumi
kwa kupitia elimu na mafunzo yanayotolewa kwa kuzingatia kanuni za Girl
Guides pamoja na kuwajenga kimaadili.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269