Breaking News

Your Ad Spot

Oct 14, 2016

MAMA JANETH: MUENZINI MWALIMU NYERERE KWA KUWAHUDUMIA WAZEE



Na Hassan Silayo-MAELEZO
Mke wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Janeth Magufuli, (pichani), amewataka watanzania kumuenzi kwa vitendo Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa kuwahudumia Wazee nchini kwa kuwapatia mahitaji ya muhimu kwa ajili ya ustawi wa maisha yao.
Akiongea na Wazee katika Kambi ya kulea wazee ya Chazi iliyopo Wilayani Mvomero Mkoani Morogoro Mama Janeth amesema kuwa watanzania wanapaswa kutambua Wazee ni kundi muhimu kwa ustawi wa nchi kwani miongoni mwao walishiriki katika ukombozi wa taifa leo hivyo tuitumie Siku kama ya leo na nyingine kumuenzi Hayati mwalimu Julius Nyerere akiwa kama mzee aliyetangulia mbele za haki.

"Leo ni siku muhimu sana katika taifa letu siku ambayo tunaenzi siku aliyofariki muasisi awa Taifa letu Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, hivyo ni rai yangu kwa watanzania kwa ujumla kumuenzi kwa kushiriki kwa pamoja katika kuwahudumia wazee na kuwapatia mahitaji yao muhimu" Alisema Mama Janeth.

Aidha, Mama Janeth alisema kuwa amesikia changamoto zinazokabili Makazi hayo na ameahidi kuendelea kushirikiana na wadau kwa kadri iwezekanavyo ili kuhakikisha wanapunguza na kuondoa kabisa changamoto hizo iwe makazi ya wazee Chazi na yote nchini yawe sehemu salama ya kuwahudumia wazee.
Katika kutembelea kituo hicho Mamam Janeth Magufuli ametoa zawadi ya mchele, Maharagwe,unga na mafuta ya kupikia kwa ajili ya wazee na watu wasiojiwezakatika kituo hicho.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Stephen Kebwe amesema kuwa serikali ya mkoa wake inatekeleza kwa vitendo maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. john Pombe Magufuli  ya kuwahudumia wazee na kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ndani mkoa wameshaanza kutatua baadhi ya kero na wataendelea kufanya hivyo ili kuyaimarisha makazi ya wazee mkoani humo.

Pia Dkt. Kebwe amewataka watu wote waliovamia makazi ya wazee kuondoka mara moja na kutafuta maeneo mengine na atakayekiuka agizo hilo serikali itamchukulia hatua kali za kisheria.

Akiwasilisha Risala ya Makazi ya Ya wazee ya Chazi kwa Mama Janeth Magufuli Kaimu Afisa Mfawidhi wa Makazi hayo Bw. Richard Kamwana amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa misaada aliyoitoa kwa wazee wa kituo hicho wakati wa sikukuu ya Eid.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero Bw. Florent Kiombo amemuhakikishia Mama Janeth Magufuli wataendelea kushirikiana na taasisi nyingine katika kukiendeleza kituo hicho ikiwamo kuwapatia wazee wote kadi za CHF kwa ajili ya kuwasaidia wazee hao kupata huduma ya Afya popote waendapo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages