Breaking News

Your Ad Spot

Jan 3, 2017

WAZIRI HAMADI RASHID: VYAMA VYA UPINZANI VINAO WAJIBU WA KUISHAURI SERIKALI

Na Idara ya Habari - MAELEZO
Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Chama cha siasa cha Alliance for Democraytic Party – ADC, Wziri Hamad Rashid Mohamed amesema, vyama vya upinzani hapa nchini vinao wajibu na  nafasi kubwa kuishauri Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoongozwa na Rais Dk. Ali Mohamed Shein katika masuala mbalimbali ya maendeleo visiwani Zanzibar ili kwa kuwa kufanya hivyo ndiyo moja ya sababu ya kuwepo vyama hivyo.

Waziri Hamad Rashid Mohamed amesema hayo alipohojiwa na Idara ya Habari (MAELEZO) leo kuhusiana na mafanikio yaliyopatikana tangu mapinduzi ya Zanzibar yalipofanyika miaka 53 iliyopita. Amesema, Dkt. Shein amekuwa akivitaka Vyama vya Upindani Visiwani Zanzibar kushiriki katika masuala ya maendeleo kwa njia mbalimbali. Alitolea mfano, yeye kabla ya kuteuliwa kuwa Waziri, Chama chake cha ADC kwa kushirikiana na Wananchi wamejenga uwanja wa mpira wa Gombani, Pemba kwa msaada kutoka Serikali ya Korea.

Waziri huyo pekee kutoka Chama cha Upinzani amewabeza Wanasiasa wanaodai kuwa Dkt. Shein hatoi nafasi kwa Vyama vingine katika kutoa michango yake katika masuala ya maendeleo. “Mimi mwenyewe nimepewa dhamana ya Uwaziri kupitia chama changu cha ADC na katika vikao tunavyokaa kila mtu anatoa mawazo yake kuhusiana na masuala ya maendeleo ya Zanzibar na kama hoja unayotoa ni ya msingi lazima itakubalika. Inapofikia suala la maendeleo Dkt. Shein haangalii Chama, anaangalia maslahi ya Zanzibar kwanza.”

Akizungumizia maadhimisho ya miaka 53 ya Maapinduzi ya Zanzibar Waziri Hamad amesema, Wazanzibar na Watanzania kwa ujumla wana kila sababu ya kuenzi Mapinduzi hayo ambayo yalikuwa chachu cha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Muungano wetu ulizingatia uwepo wa umoja kwani Serikali ya Kikoloni ilipandikiza mbegu ya kubaguana hata Waafrika kwa Waafrika wenyewe.

Alifafanua kuwa, mapinduzi hayo yaliifanya nchi iwe huru zaidi na Wananchi wake waishi kwa amani, umoja na mshikamano. Chini ya uongozi wa Rais wa Awamu ya kwanza wa Zanzibar marehemu Sheikh Abeid Aman Karume, Zanzibar ilipata maendeleo makubwa ambapo zilijengwa nyumba bora za makazi za Wananchi, elimu ilitolewa bure, huduma za afya, maji na hivyo kufuta kabisa aina zote za ubaguzi uliokuwa umeota mizizi kabla ya mapinduzi.

Akijibu swali kuhusiana na masimamo Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli juu ya mageuzi ya kuekelea kwenye uchumi wa Viwanda amesema, kukua kwa uchumi ndio kigezo cha maendeleo katika Taifa lolote duniani. “Rais anaposema anataka Taifa liondokane na umasikini inawezekana iwapo tutakuwa na viwanda vidogo vidogo, vya kati na vikubwa.

Ameeleza kuwa, kutokana na viwanda Watu watapata ajira, Wakulima watapata soko la uhakika la mazao wanayozalisha na bidhaa zitakazozalishwa zitauzwa ndani na nje ya nchi kwa kuwa zimeongezwa thamani. Hivyo katika kufikia malengo hayo lazima tukubali mageuzi hayo na Wananchi lazima wafanye kazi.

Mwisho alimalizia kwa kutoa wito wa Zanzibar lazima iwe salama na ibaki salama kwa kusisitiza nchi ni lazima iwe na Amani, Mshikamano na Utulivu. Inapotetereka ni vema kushirikisha viongozi wa dini na Wazee wenye busara ili kutanzua matatizokuliko amani kutoweka. kwa Wazanzibar, kila mmoja ajiiulize ameifanyia nini Zanzibar ili kuleta maendeleo.
Kwa wanasiasa alitoa wito kwa kusema njia za kurekebisha makosa zipo kukubali kukaa chini na kuzungumza kutoa lawana sio suluhisho. Vyama vya siasa vishiriki kikamilifu katika utekelezaji wa maendeleo ya Zanzibar.  

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages