Breaking News

Your Ad Spot

Mar 30, 2017

UWT WAKASIRIKA CHADEMA NA CUF KUTEUA MIDUME TU UBUNGE AFRIKA MASHARIKI

Dar es Salaam
Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) umekipongeza na kukishukuru Chama Cha Mapinduzi (CCM), kwa  uamuzi wake wa kuteua wagombea wa Ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki kwa uwiano ulio sawa baina ya wanaume na wanawake.

Akizungumza na waandishi wa habari, leo katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa UWT, Amina Makilagi, amesema, kwa uteuuzi huo umedhihirisha kuwa CCM ianatambua na kuthamini mchago wa wanawake katika maendeleo ya Jamii.

" Umoja wa wanawake Tanzania, tunaishukuru Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM iliyokutana jana tarehe 29/3/2017 chini ya Mwenyekiti Dk. John Pombe Magufuli kwa uamuzi wake wa kuteua wagombea wa Ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki kwa uwiano ulio sawa baina ya wanaume na wanawake {50/50}, wanawake 6 na wanaume 6. UWT inatoa shukrani na pongezi kwa uteuzi huo unaodhihirisha kuwa CCM inatambua na kuthamini mchango wa wanawake katika maendeleo ya jamii yetu", amesema  Makilagi.

Amesema wakati UWT iikiipongeza CCM,  haikufurahishwa na uteuzi uliofanywa na vyama vya CHADEMA na CUF katika uteuzi wao wa nafasi hizo, akisema haukuzingatia usawa wa kijinsia kwa kuteua wagombea wote wanaume.

"UWT unavitaka Vyama hivyo kujifunza na kuiga mfano wa CCM katika teuzi zake kwa kuzingatia uwiano sawa na kutambua nafasi ya wanawake, kwani UWT inaamini wapo wanawake wengi wenye uwezo, maarifa na sifa za kugombea katika vyama hivyo ambao wangeliweza kupewa nafasi", amesema.

Katika hatua nyingine, UWT imeihsukuru na kuipongeza CCM kwa uteuzi wa watendaji wake kwa nafasi ya Katibu wa Mkoa na Wilaya ambapo asilimia 30 ya Makatibu walioteuliwa ni wanawake na hivyo kuiomba CCM na Serikali yake kuendelea kuwateua wanawake katika nafasi mbalimbali za Uongozi na Uwakilishi kwenye vyombo vya Maamuzi.

Makilagi amesema UWT inawahamasisha wanachama wake na wanaCCM wenye sifa kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi wa ndani wa Chama na Jumuiya zake ambapo kwa UWT uchaguzi ngazi ya Tawi utaanza tarehe 1- 10/04/2017 hatua ya kuchukua na kurejesha fomu. 

"Natoa mwito kwa wanachama wenye sifa kuchukua fomu katika Ofisi zote za Matawi 24,770 ya UWT zilizopo Tanzania Bara na Zanzibar.

Aidha, nawasihi Viongozi, watendaji na wanachama wote wa UWT/CCM kutojihusisha na vitendo vya rushwa na ukiukaji wa Katiba, Kanuni na taratibu za uchaguzi katika kutafuta uongozi, kwani kufanya hivyo kutawaondolea sifa na atakayebainika atachukuliwa hatua kwa mujibu wa Kanuni za Maadili ya Chama na kwa sheria za Nchi", alisema.

Pia Makilagi amsema, UWT inaipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Dk. John Magufuli kwa utekelezaji nzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2015 – 2020 na kupongeza hatua ya Serikali kuzuia makontena yenye mchanga wa madini na kuunda Tume itakayobainisha kiwango cha madini kilichomo. Lengo likiwa kuhakikisha rasilimali zetu zinawanufaisha Watanzania wote.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages