Breaking News

Your Ad Spot

Jul 31, 2017

MAMA NAMAINGO ‘AWAFUNDA’ AKINAMAMA WA GREEN VOICES KILIMOBIASHARA NA UJASIRIAMALI

Mkurugenzi wa Namaingo, Biubwa Ibrahim
Mratibu wa Mradi wa Green Voices kutoka Hispania, Alicia Cedaba, akiwapa majukumu washiriki wa warsha hiyo.

MKURUGENZI Mtendaji wa kampuni ya Namaingo Business Agency, Biubwa Ibrahim, amewataka akinamama wanatekeleza mradi wa Green Voices Tanzania kuwa wabunifu na kutokata tamaa katika shughuli wanazozifanya.

Akizungumza wakati wa kufunga semina ya siku sita ya mafunzo yaliyowashirikisha akinamama 15, Biubwa alisema kwamba, ubunifu, jitihada na kutokata tamaa ndiyo silaha kubwa katika mafanikio, huku akiwahimiza watafute fedha bila kuchoka.

“Lazima muwe wabunifu, halafu ni dhambi kubwa kukata tamaa bali mnatakiwa kuongeza jitihada katika mradi yenu,” aliwahimiza.

Aidha, alisema kwamba, mafanikio yoyote hayawezi kuja kwa siku moja, hivyo wanapaswa kuwa wavumilivu daima ili waweze kufanikiwa.

Akinamama hao wa Green Voices wanatekeleza miradi mbalimbali ya kilimo inayoendana na mapambano dhidi ya uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi, ambayo inadhaminiwa na taasisi ya Women for Africa Foundation ya Hispania inayoongozwa na makamu wa rais mstaafu wa nchi hiyo, Bi. Maria Tereza Fernandes de la Vega.

Biubwa alisema, wajasiriamali wengi wanaposhindwa kuona faida ya shughuli wanazozifanya huvunjika moyo mapema, lakini hilo lisiwe kikwazo kwao kwani wanapaswa kukaa chini na kutafakari njia mpya ya kuendesha biashara ama miradi yao.

“Inabidi kujiuliza wewe mwenyewe kama hapo ulipo ndipo mahali sahihi, vinginevyo usife moyo unapoona mambo hayaendi, bali angalia wapi ulipokosea na ujipange upya halafu utaona matokeo yake,” alisema.

Akaongeza: “Mimi nilianza na mtaji wa shilingi elfu nne tu, nimepitia changamoto nyingi ikiwemo kudhulumiwa fedha, lakini katu sikukata tamaa nimeendelea kupambana na mpaka sasa kupitia kampuni yangu nimeweza kusajili wakulima 400,000 nchi nzima.”
Mwanahabari mshiriki wa mradi wa Green Voices, Farida Hamisi, akipokea cheti kutoka kwa Alicia Cedaba, Mratibu wa Green Voices kutoka Hispania. Katikati ni muwezeshaji wa mafunzo hayo, Dkt. Olomi kutoka taasisi ya IMED.

Mradi wa Green Voices unatekelezwa nchini Tanzania pekee, ambapo akinamama 10 kati ya 15 wanaendesha miradi mbalimbali ya kilimo, ufugaji wa nyuki, ukaushaji wa mboga na matunda pamoja na utengenezaji wa majiko rafiki katika jitihada za kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

Akinamama walioanzisha miradi hiyo – miradi na mikoa watokayo vikiwa kwenye mabano –ni Regina Kamuli (Mkuranga, Pwani – Majiko Banifu), Abiah Magembe (Kisarawe, Pwani – Usindikaji wa Muhogo na Mtama), Magdalena Bukuku (Kinondoni, Dar es Salaam – Kilimo cha Uyoga), Mariam Bigambo (Dakawa, Morogoro – Ufugaji wa Nyuki), na Esther Muffui (Morogoro – Ukaushaji wa Mboga na Matunda).

Wengine ni Farida Makame (Kilimanjaro – Majiko ya Umeme-Jua), Leocadia Vedastus (Ukerewe, Mwanza – Kilimo na Usindikaji wa Viazi Lishe), Monica Kagya (Kisarawe, Pwani – Ufugaji wa Nyuki), Dkt. Sophia Mlote (Kinyerezi, Dar es Salaam – Kilimo Hai cha Nyanya na Mbogamboga), na Evelyn Kahembe (Uvinza, Kigoma – Kilimo cha Matunda).

Mradi huu wa Green Voices ambao mwaka huu uko katika awamu ya pili, ulizinduliwa Julai mwaka 2016 na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Samia Suluhu Hassan.

Katika awamu ya pili kinamama hawa wameendelea kuboresha kilimo cha mazao yao kinachozingatia uhifadhi wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi katika mikoa sita nchini. 

“Pamoja na kilimo, Mradi wa Green Voices umaeandaa mafunz mbalimbali ya kuongeza ujuzi katika kilimo (climate smart agricultura) pamoja na mafunzo ya jinsi ya kuandaa mazao au bidhaa wanazozalisha kupitia kilimo,” alisema Mratibu wa Green Voices nchini Tanzania Secelela Balisidya.

Katika kutekekelza hilo, Green Voices kupitia mfadhili wake, Women for Africa Foundation, walishiriki katika mafunzo mbalimbali ya Mbinu bora za kuweka nembo na kufungasha bidhaa za vyakula, Viwango vya Ubora, na Kanuni za uchakataji wa vyakula.

Mafunzo hayo ambayo yalifanyika Julai 16 -22, 2017 yalizinduliwa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Selemani Jaffo, ambaye aliahidi kuwapa ushirikiano akina mama hao.

Utengenezaji bidhaa na ufungashaji
Kwa siku sita baada ya kuzinduliwa kwa mafunzo, akinamama hao walijifunza kuhusu Mchango wa kilimo katika mabadiliko ya tabianchi, Jinsi ya kuweka mazingira bora ya umwagiliaji, Mikakati ya biashara katika ujasiriamali wa kilimo, Utafutaji wa rasilimali na mkakati wa kuongeza mtaji, Ukuzaji wa mtaji kupitia Vicoba, na Mbinu za uongozi.


Akinamama hao walipata fursa ya kutembelea Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) ambapo ilikutana na wajasiriamali walio katika hatua za juu za kufungasha na kuuza bidhaa zao, ambapo walipata nafasi ya kubadilishana nao mawazo ili kuongeza ujuzi wao.

Katika mafunzo hayo, Linus Gedi ambaye ni mtaalam wa ubora wa chakula na viwango kabla ya kuvipeleka sokoni, aliwaeleza washiriki kwamba ni muhimu kufungasha na kuweka nembo kwani inasaidia kuhifadhi bidhaa na inarahisisha  mteja kutambua hiyo ni bidhaa ya aina gani, imetengenezwa wapi na ina mchanganyiko gani.
Akinamama wanaotekeleza mradi wa Green Voices walipotembelea Ofisi za SIDO jijini Dar es Salaam.

“Ni muhimu sana kuhakikisha chakula hakisababishi maradhi, lakini pia kinafikia malengo ya walaji, hii huepusha sumu kwenye chakula, mchanganyiko usiofaa, upotevu wa chakula, kupoteza bidhaa na kuepukana na masuala ya kisheria,” alisema Linus.
Alisema uzalishaji wa chakula unatakiwa kuzingatia mbinu bora za uzalishaji na pamoja na usafi.

Aidha, aliwataka kuzingatia ubora, usafi na viwango vya chakula wanachozalisha ili kifikia malengo ya walaji.
Kwa upande wake, Richard Jackson akielezea umhimu wa kunadi bidhaa, alisema ni lazima kuwa na mikakati imara ya masoko ili kuhakikisha mjasiriamali anapata faida.
Alisema ni vizuri kujua wateja maalum na wateja wa ujumla na nini hasa wanahitaji ikiwa ni pamoja na namna ya kuwafikia.

“Ni lazima kujua kati ya wanaohitaji bidhaa zako, ni nani ambao siyo wateja wako walengwa na kwa nini wateja wanunue bidhaa zako na siyo kwa washindani wako? Lazima ujue tabia zao na ukubwa wa soko lako,” alisema Jackson.

Aidha, alisema ni muhimu kuwajua wateja wako ili kuelewa mahitaji yao na kwa nini wananunua bidhaa wanazonunua pamoja na kutambua mambo yanayowaudhi ili usiwakwaze.

Kwa upande wa uchangishaji fedha na kutafuta mitaji kwa biashara na kilimo, Rais wa VICOBA Endelevu Tanzania, Devota Likokola, alieleza jinsi mfumo wa VICOBA Endelevu unavyoweza kuwasaidia kinamama wa Green Voices kupata mitaji ya kuendeleza miradi yao.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages