Breaking News

Your Ad Spot

Nov 16, 2017

TAASISI YA MOYO JAKAYA KIKWETE KWA KUSHIRIKIANA NA TAASISI YA KIMATAIFA YA KIISLAMU YA MISAADA (IIRO) YA NCHINI SAUD ARABIA KWA MARA YA KWANZA WAFANYA UPASUAJI WA KUZIBUA MISHIPA YA MOYO KUPITIA MSHIPA WA DAMU WA MKONO (CATHETERIZATION) BADALA YA MSHIPA WA DAMU WA PAJA KWA KUTUMIA MTAMBO WA CATHLAB.

Zoezi la kumfanyia mgonjwa upasuaji wa kuzibua mishipa ya moyo kupitia mshipa wa damu wa mkono (Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab likiendelea.
 (Picha na JKCI)

Na Mwandishi wetu
Leo Novemba 16, 2017 jumla ya wagonjwa 20 wamefanyiwa upasuaji wa kuzibua mishipa ya moyo kupitia mshipa wa damu wa mkono (Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab hii ikiwa ni mara ya kwanza kwa upasuaji wa aina hiyo kufanyika hapa nchini.
Akiongea na Waandishi wa Habari leo jijini Dar Salaam Daktari bingwa wa magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Peter Kisenge alisema upasuaji huo unafanyika  katika kambi ya matibabu ya Moyo inayofanywa na Taasisi hiyo kwa kushirikiana na madakatari kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini Saudi  Arabia.
Dkt. Kisenge alisema kuwa kambi hiyo inaenda sambamba na utoaji wa elimu na kubadilishana ujuzi wa kazi  kati ya wafanyakazi wa Taasisi hizo mbili ikiwemo aina mpya ya upasuaji wanaoufanya kitu ambacho kinawajengea uwezo zaidi. ”
“Faida ya upasuaji huu ni kumwezesha mgonjwa kutoka chumba cha upasuaji akiwa  anatembea na baada ya masaa manne kama hali yake inaendelea vizuri anaweza kuruhusiwa.
“Tofauti na upasuaji wa kutumia mshipa wa paja ambao tulikuwa tunaufanya, baada ya upasuaji mgonjwa ni lazima akae Hospitali kwa zaidi ya masaa 24 ili kuangalia maendeleo ya afya yake”, alisema Dkt. Kisenge.
Kwa upande wake  Daktari bingwa wa magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya IIRO Ali Al Masoud   alisema kambi hiyo inaendelea vizuri kwani kwa siku wanatibu wagonjwa 10 na baada ya matibabu afya zao zinaimarika tofauti na ilivyokuwa  kabla ya matibabu.
Dkt. Masoud aliongeza kuwa  wamekuja na utaalam mpya wa kuzibua mishipa ya moyo kupitia mshipa wa damu wa mkono ambapo kabla ya hapo matibabu yaliyokuwa yanafanyika ni ya kutumia mshipa wa damu wa kwenye paja.
Alifafanua, “Hivi sasa tunafanya upasuaji wa Moyo wa bila kufungua kifua  kitu ambacho wenzetu hawa walikuwa wanakifanya. Sisi tumewaongeza utaalam mpya wa kutumia  mshipa ya mkononi badala ya mshipa wa  paja.
Naye Bader Alanezi ambaye ni Mtaalamu wa magonjwa ya Moyo na mishipa ya damu kutoka IIRO alimalizia kwa kusema kuwa  wamepata muda wa kujifunza vitu vingi na kupata uzoefu mpya  wa baadhi ya magonjwa na mambo ya kiteknolojia ambayo katika nchi yao hakuna.
Jumla ya wagonjwa  40 wanatarajiwa kufanyiwa upasuaji katika kambi hiyo ya siku tano ambayo imeanza tarehe 14 hadi tarehe 18 mwezi huu. 

 Madaktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Peter Kisenge na mwenzake wa Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini Saud Arabia Ali Al Masoud wakimfanyia mgonjwa upasuaji wa kuzibua mishipa ya moyo kupitia mshipa wa damu wa mkono (Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab katika kambi ya matibabu ya moyo inayoendelea kwenye Taasisi hiyo. Jumla ya wagonjwa 40 wanatarajiwa kufanyiwa upasuaji katika kambi hiyo ya siku tano.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages