Na Jumia Travel Tanzania
Miongoni
mwa maeneo ya kitalii ambayo hayapewi kipaumbele au kutokuwa maarufu ni
pamoja na Kusini mwa Tanzania. Tofauti na vivutio vya kitalii vya kanda
ya Kaskazini kuwa maarufu kama vile Mlima Kilimanjaro, Hifadhi za
Serengeti na Ngorongoro, kuna uwezekano mkubwa kwamba Kusini mwa
Tanzania kuna hazina kubwa ya vivutio kwa watalii ambavyo havitangazwi
au kuvumbuliwa na wengi.
Miongoni
mwa sababu ambazo zimekuwa zikikwamisha shughuli za kitalii kwa ukanda
wa Kusini ni pamoja na miundominu hafifu kama vile barabara, viwanja vya
ndege ambavyo hupelekea maeneo hayo kufikika kwa ugumu pamoja na
upungufu wa malazi kama vile hoteli za kisasa na zinazokidhi vigezo.
Kwa
kutambua umuhimu wa ukanda huu, serikali ya awamu ya tano imekuwa
ikifanya jitihada za makusudi ambazo zitakuwa ni chachu katika kukuza
utalii. Jitihada hizo ni pamoja na kuzinduliwa kwa mpango wa uwekezaji
katika miundombinu ya mradi wa kuendeleza utalii ukanda wa Kusini mwa
Tanzania (REGROW) eneo la Kihesa, Kilolo mkoani Iringa. Mradi huo
ulizinduliwa hivi karibuni na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mh. Bi. Samia Suluhu na kuhudhuriwa na Waziri wa Maliasili na
Utalii, Mh. Dkt. Hamisi Kigwangala.
Pamoja
na jitihada hizo watalii na watanzania kwa ujumla wanahitaji kujua
vivutio vinavyopatikana katika eneo hilo. Kwa kutambua umuhimu wa kutoa
elimu juu ya vivutio mbalimbali nchini Tanzania, Jumia Travel
imekukusanyia vivutio na shughuli zifuatazo za kitalii pindi utembeleapo
eneo la Kusini mwa Tanzania.
Iringa.
Mkoa wa Iringa ni kivutio tosha kutokana na historia yake ndefu tangu
enzi za utawala wa kikoloni wa Wajerumani. Ni eneo ambalo Wajerumani
walijenga ngome yao kwa ajili ya kupambana na vuguvugu za harakati za
kukataa kutawaliwa kutoka kwa kabila la Wahehe ambazo ziliongozwa na
Chifu Mkwawa. Mji huu ambao ulijengwa tangu karne ya 19 una mambo mengi
ya kujifunza na kujionea pindi utembeleapo ambayo hayapatikani sehemu
yoyote nchini.
Isimila.
Mbali na harakati za wazi za kupinga ukoloni wa Wajerumani, eneo la
Kusini linasifika kwa kupatikana kwa mabaki ya historia za kale. Eneo
hili limegundulika kuwa na masalia ya kutosha ya zana za kale za Zama za
Chuma kuliko eneo lolote duniani, ambapo inasemekana ni maeneo ya
mwanzo kabisa kuzalisha zana za viwandani na vichwa vya mishale.
Bonde
la Kilombero. Ukubwa wa bonde hili ambalo hujaa maji kwa msimu
umelifanya kuwa ndilo kubwa katika ukanda wa Afrika ya Mashariki. Kuna
shughuli nyingi za kufanya kama mtalii na mambo kadhaa ya kujifunza
pindi utembeleapo eneo hili linalopatikana mkoani Morogoro. Miongoni mwa
shughuli za kufurahia ni pamoja na kujionea ndege wa aina mbalimbali wa
kuvutia pamoja na shughuli za kijadi za wakazi wa eneo hilo kama vile
uvuvi.
Hifadhi
ya Taifa ya Mikumi. Kama unaishi Dar es Salaam itakuchukua mwendo wa
nusu siku kwa gari ili kufika kwenye mbuga hiyo. Ikiwa imezungukwa na
safu ya milima, hifadhi hiyo ya taifa inatoa mandhari nzuri ya mawio na
machweo. Mikumi ni mahali pazuri kwa kujionea wanyama wa aina mbalimbali
wanaoonekana kwa urahisi na ndani ya muda mfupi. Lakini pia ni sehemu
ambayo unaweza kuvinjari aina tofauti za ndege.
Hifadhi
ya Taifa ya Ruaha. Mbuga hii ni maarufu kwa kujionea wanyama mbalimbali
ambao watalii wengi hupendelea kuwaona. Ukiwa kwenye hifadhi hii
wanyama kama vile chui, duma, simba na mbwa mwitu ni jambo la kawaida
kuwaona.
Selous.
Hii ndiyo hifadhi inayoshikilia rekodi ya ukubwa duniani kama ulikuwa
haufahamu. Kutokana na ukubwa huo hutoa fursa ya kuwatazama wanyama kwa
utulivu zaidi kwani watalii sio wengi tofauti na ukanda wa Kaskazini.
Hifadhi ya mbuga ya Selous ni nyumbani kwa wanyama wakubwa kama vile
simba, chui, mbwa mwitu, viboko na makumi ya maelfu ya tembo.
Milima
ya Udzungwa. Hifadhi ya Taifa ya milima ya Udzungwa ni hifadhi ya
misitu ambapo hurusiwa kutembea pekee. Miongoni mwa vivutio ukiwa hapa
ni pamoja na kuvinjari matembezi katikati ya msitu wenye miti mirefu
yenye urefu wa takribani mita 60 na kujionea maporomoko marefu ya maji
yanayotiririka kutoka milimani. Safu ya milima ya Udzungwa ina utajiri
wa takribani 40% ya misitu na wanyama wa aina mbalimbali.
Milima
ya Uluguru. Badala ya kufunga safari kwenda mikoa ya Kaskazini unaweza
kutembelea safu ya milima ya Uluguru ambayo ipo umbali mchache kutokea
mji wa Morogoro. Ikiwa na urefu wa takribani mita 2300, milima hii
itakupatia wasaa mzuri wa kuepuka pilikapilika za jiji la Dar es Salaam.
Kama kupanda milima hiyo haitoshi, eneo hili pia limepakana na Hifadhi
za Taifa za Selous na Mikumi.
Zipo
shughuli nyingi za kufanya na mambo ya kuvutia pindi utembeleapo
vivutio vilivyopo eneo la mikoa ya Kusini. Lakini ni karibu zaidi na
hivyo kuokoa gharama za usafiri kwani hakuna umbali mrefu. Faida
nyingine ni kwamba kutokana na watalii wengi kumininika ukanda wa
Kaskazini, maeneo ya Kusini hutoa fursa ya kujionea vivutio vingi zaidi
kwa utulivu bila ya kuwa na msongamano mkubwa.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269