Breaking News

Your Ad Spot

Nov 23, 2010

MATAKWA YA WANANCHI YAZINGATIWE KURA YA MAONI SUDANI KUSINI

KATIBU MKUU WA UMOJA WA MATAIFA, BAN KI MOON AKIBADILISHANA MAWAZO NA WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA UINGEREZA BW. WILLIAM HAGUE MUDA MFUPI KABLA YA KUANZA KWA MKUTANO WA BARAZA KUU LA USALAMA LILILOKUWA LIKIJADILI HALI YA SUDANI HUSUSANI MCHAKATO WA UPIGAJI KURA YA MAONI UTAKAOFANYIKA SUDANI YA KUSINI NA ENEO YA ABYEI JANUARI TISA MWAKANI.

PICHANI NI WAJUMBE WA BARAZA KUU LA USALAMA WA UMOJA WA MATAIFA WAKIWA KATIKA MKUTANO WA KUJADILI HALI YA SUDANI NA MCHAKATO WA UPIGAJI WA KURA ZA MAONI. MKUTANO HUO ULIOKUWA KATIKA NGAZI YA MAWAZIRI ULIHUDHURIWA PIA NA WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA MAREKANI BI HILARY CLINTON NA WAWAKILISHI WA PANDE MBILI ZINAZOHUSIKA NA MCHAKATO HUO YAANI SERIKALI YA SUDANI KUSINI INAYOONGOZWA NA KIKUNDI CHA SPLM NA SERIKALI KUU YA KHARTOUM 
NA MWANDISHI MAALUM
NEW YORK
Wakati wananchi wa Sudani ya Kusini wakiendelea na zoezi la kujiandikisha kwa ajili ya kupiga kura ya maoni itakayoamua mstakabali wao wa kujitenga, Baraza kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa limezihimiza pande zote zinazohusika na mchakato huo kuheshimu matakwa ya wananchi.

Aidha Baraza hilo pia limezitaka pande zinazohusika kuchukua hatua muhimu na za haraka kuhakikisha kura hiyo inapigiwa katika muda waliokubaliana.

Wananchi wa Sudani ya Kusini watapiga kura Januari tisa mwakani kuamua kama wajitenge na serikali Kuu ya Khartoum. Ili hali wananchi wa eneo la Abyei wao lenye utajiri mkubwa wa mafuta wao watapiga kura ya kuamua waende upande upi.

Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, katika mkutano wake uliofanyika katika ngazi ya mawaziri, lilikutana siku ya jumanne chini ya Urais wa Uingereza kwa mwezi Novemba kujadili hali ya Sudani.

Katika taarifa yake kwa Baraza hilo, Waziri Uingereza anayehusika na Mambo ya Nje na masualaya Jumuia ya Madola, wa Mambo ya N Bw. William Hague amesema “ Baraza linazitaka pande zote zinazohusika na mkataba wa amani wa mwaka 2005 kuchukua hatua haraka , kuhakikisha kunakuwapo na amani, na kura ya maoni inapigwa kwa wakati na katika mazingira huru na kwa kuzingatia matakwa ya wananchi wa Sudani ya Kusini na Abyei.

Katika Mkutano huo, wajumbe walipokea taarifa za kuanza kwa zoezi la uandikishaji wapiga kura. Zoezi hilo lilianza siku ya jumatatu na litaendelea hadi Desemba Mosi.

Wajumbe hao pia wamezungumzia haja ya kukamilishwa kwa baadhi ya vipengele vilivyomo katika Mkataba wa amani, baadhi ya vipengele hivyo ni suala la mipaka, mali asili, uraia, sarafu na suala zima la amani.

Aidha Baraza hilo pia limezitaka pande husika kushirikiana kwa karibu na jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa nchini Sudani ( UNAMIS) katika kipindi chote na utekelezaji wa majukumu yake.

Ushirikiano ambao pande hizo zinatakiwa kulipatia jeshi hilo ni pamoja na uhuru wa kwenda wanakotaka, uhuru wa kusafirisha vifaa na watu na usafirishaji wa vifaa vya kupigia kura.

Akizungumza katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon, amesema ingawa jumuia ya kimataifa inatoa misaada na ushirikiano mkubwa kuhakikisha upigaji kura ya maoni unafanyika na kwa wakati. Lakini anabainisha kuwa wajibu huo hauwezi kuchukua nafasi au kuwa mbadala wa utayari wa pande zinazohusika kutimiza wajibu wao.

Amesisitiza kuwa Umoja wa Mataifa unafanya kazi na pande zote mbili ili kuhakikisha kwamba kunakuwa na hali ya amani na utulivu wakati wa kipindi cha upigaji kura na baada ya kupiga kura.’

Hata hivyo ametahadharisha kwamba majeshi ya Umoja wa Mataifa yanaweza yasiwe na uwezo wa kutosha wa kuzuia kurejea kwa vita endapo ghasia kati ya pande hizo mbili zitaibuka tena

Wakati huo huo timu ya watu watatu inayoongozwa na Rais Mstaafu wa Tanzania Benjamin Mkapa, tayari iko nchini Sudani kuangalia zoezi la uandikishaji wapiga kura linavyoendelea.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolwa na Idara ya Habari ya Umoja wa Mataifa, Rais Mstaafu Mkapa na timu yake waliwasili nchini humo muda mfupi kabla ya zoezi hilo halijaanza.

Akiwa nchini humo, Mkapa amenukuliwa akisema kuwa uandikishwaji wa wapiga kura ni hatua moja muhimu sana ya kuelekea mchakato wa upigaji wa kura yenyewe

Akabinisha kuwa timu yake inalifuatilia kwa makini sana zoezi hilo wakati wote watakapo kuwapo nchi humo ili kuona linakwendaje.

Mkapa pia amesema ni matumaini ya timu yake kuwa wananchi wote wa Sudani ya Kusini kokote kule walipo watajitokea kwa amani na kujiandikisha.

Akongeza kuwa timu yake iliyoteuliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Mwezi Septemba, inatambua wazi kwamba uratibu mzima wa maandalizi ya daftari la wapiga kura halikuwa jambo rahisi na hasa kwa kuzingatia ukubwa wa eneo lenyewe na kasi ya maandalizi lakini wana matumaini kwamba kazi hiyo itamalizika kwa mafanikio.



============================================================

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages