Breaking News

Your Ad Spot

Apr 19, 2011

MKAZO UTILIWE KATIKA KUTAMBUA MAPEMA DALILI ZA MALARIA: TANZANIA

Na Mwandishi Maalum, New York
Baraza kuu la  Umoja wa Mataifa limepitisha kwa kauli moja azimio linalohimiza  Kuimarisha faida na Kuongeza kasi katika jitihada za kuuthibiti na  hatimaye kuutokomeza  Ugonjwa wa Malaria ifikapo mwaka 2015.
Mchakato wa majadiliano  ya Azimio hilo yalihusisha nchi za Afrika kwa upande mmoja  na   nchi zilizoendelea kwa upande mwingine.  Tanzania kupitia Ubalozi wake katika Umoja wa Mataifa, ndiyo iliyosimamia na kuendesha majadiliano hayo hadi kupatikana kwa Azimio hilo.
Akiwasilisha Azimio hilo mbele  ya Baraza Kuu la 65 la Umoja wa Mataifa, Mwakilishi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa,  Balozi Ombeni Sefue amesema kwamba   nchini nyingi zinazoendelea zikiwamo za Afrika zimeonyesha kufanikiwa katika kuudhibiti ugonjwa wa malaria.
Anasema   mafanikio  hayo ambayo kwa kiasi kikubwa yametokana   dhamira ya kisiasa iliyoonyeshwa na viongozi wa nchi hizo, upatikanaji wa misaada kama vile fedha na madawa, pamoja na  utambuzi wa haraka wa homa zitokanazo na malaria  ukiwa umechangia sana.
Anasisitiza kuwa   Suala la  utambuzi wa haraka wa kutofautisha baina ya homa zitokanazo  na vimelea vya   malaria na  homa ambazo hazisababishwi na vimelea vya malaria ni  jambo la muhimu  sana katika kuutibu na kuudhibiti ugonjwa huo.
Mwakilishi huyo wa Tanzania katika UM, amebainisha  kuwa   nchi nyingi zimefanikiwa  katika  upimaji na utambuzi wa homa zitokanazo na malaria,kutokana na ufadhili mkubwa  katika eno hilo. Takwimu zinaonyesha kuwa  kupitia ufadhili huo, utambuzi wa homa za malaria umeongezeka kutoka asilimia tano mwanzoni mwa mwongo  huu hadi kufikia asilima 35 mwak 2009.
kwa namna yoyote ile anasema Balozi Sefue haya ni mafanikio tosha, ingawa bado kunahitajika uimarishaji na   upanuzi wa   uwezo  huo wa kutambua ugonjwa wa malaria kutokana na ukweli kwamba matukio  mengi ya malaria hayachunguzwi ipasavyo
Akielezea zaidi  mafaniko katika kuudhibiti ugonjwa huo katika Afrika na nchi nyingine,  Balozi Sefue anasema  matumizi ya vyandarua vilivyotiwa viatilifu  yameongezeka sana.
Kwa mfano anasema  kati ya mwaka  2008 na 2010  zaidi ya vyandarua 289 milioni vyenyeviatilifu, vilikuwa zimesambazwa Kusini mwa Jangwa la  Sahara.
Aidha inakadiriwa kuwa  asilima 45 ya  kaya katika Afrika zilikuwa zinamiliki  angalau chandarua kimoja  chenye viatilifu.
Kama hiyo haitoshi, asilimia 35 ya watoto chini ya miaka mitano wanalala kwenye vyandarua hivyo. “ haya ni mafanikio,lakini  lengo letu la pamoja ni kuhakikisha kila mtu anapata chandarua    kwa maana hiyo  bado tunasafari ndefu”.
Aidha  Tanzania kupitia Balozi Sefue  imetaka kuwapo kwa uratatibu maalum utakaohakikisha kwamba ubadilishaji wa vyandarua ambavyo vimekwisha muda wake unafanyika kwa umakini bila ya kuathiri zoezi  hilo.
Amesema uhai wa vyandarua vyenye viatilifu ni miaka mitatu na baada ya hapo nguvu ya dawa hiyo inakuwa imekwisha, sasa kama hapakuwapo  na  utaratibu mzuri wa kuvibadili kwa wakati kunahatari ya  kurudhisha nyuma  kazi nzuri ambayo imekwisha kufanyika hadi sasa.
Kuhusu matumizi ya dawa za mseto za  malaria  ( ACTs), Balozi  Sefue anasema  kutokana na  nchi nyingi kubadilisha sera zake   pamoja na kuongeza  bajeti, nchi 11 za Afrika zimeweza kutoa dawa mseto kwa asilima 100 kwa  wagonjwa waliokwenda kupata huduma katika  sekta za umma hadi  mwishoni mwa  2009.
Pamoja na mambo mengine Azimio hilo linasisitiza umuhimu wa kuimarisha miundombinu ya udhibiti na  utokomezaji wa malaria ili kufikia malengo yakimataifa yaliyokubaliwa.
Aidha Azimio hilo inahimiza  Jumuia  ya Kimataifa, Umoja wa Mataifa na wadau wengine wote kushiriki kikamilifu katika ufadhili na utekelezaji wa  mapango wa malaria duniani.
Wakati huo huo Msemaji wa  Mpango wa Ushirikiano kuhusu Malaria ( Roll Back Malaria Partineship). Amesema  Baraza Kuu  kupitisha Azimio  hilo,   ni kielelezo kipya cha juhudi za nchi wanachama za  kutekeleza malengo ya ushirikiano kuhusu udhibiti wa ugonjwa wa malaria na utekelezaji wa malengo ya maendeleo  ya millennia.
Msemaji wa Ushirikiano huo, Bw Herve Verthoosel ameyasema hayo mara baada ya Baraza kupitisha  Azimio hilo,  huku  akimpongeza Rais Jakaya Kikwete  kwa kuonyesha dhamira  ya kisiasa katika kukabiliana na Malaria   na Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, kwa kusimamia azimio hilo na kuhakikisha kwamba linapita kwa kauli  moja.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages