Breaking News

Your Ad Spot

Jul 16, 2011

SUDANI YA KUSINI YAWA MWANACHAMA WA 193 WA UMOJA WA MATAIFA

Na Mwandishi Maalum
New York
Mkutano Mkuu wa 65 wa Umoja wa Mataifa, jana julai 14 umeipitisha  kwa kauli moja Jamhuri ya Sudani ya Kusini kuwa mwanachama    mpya wa 193 wa Umoja wa Mataifa.
Tukio hilo la kihistoria lililokuwa na msisimko wa aina yake, lilitanguliwa kwanza kwa   kusomwa kwa tamko maalum lililoandaliwa na    Kundi la nchi za Afrika  katika Umoja wa Mataifa, tamko  liloinadi Sudani ya Kusini ili iweze kuingizwa kuwa mwanachama wa UM.
Bw. Jeffrey Thamsanqa Rabede, Waziri wa     Sheria na Katiba kutoka Afrika ya Kusini, ndiye aliyesoma Tamko  hilo ambalo baadaye lilipitishwa kwa kauli mmoja na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa.
Akizungumza  mara baada ya Jamhuri ya Sudani ya Kusini kukubaliwa rasmi kuwa mwanachama  wa 193 wa Umoja wa Mataifa,  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon alisema.
“ Katika muda huu na mahali hapa, dunia imekusanyika na kutamka kwa kauli moja,  karibu Sudani ya Kusini. Karibu katika Jumuia ya Umoja wa Mataifa”  .
 Akaendelea kusema “ kwa  pamoja hebu na tuwaambie wananchi wa taifa hili jipya. Sasa mnakaa  miongoni mwetu na tunasimama pamoja nanyi”
Naye Rais wa Mkutano wa Mkuu wa 65 Bw. Joseph Deiss amesema, siku ya julai 14 ilikuwa ni siku muhimu sana kwa  Afrika na  kwa Jumuia ya  Kimataifa
Akaelezea matumaini yake kwamba Sudani ya Kusini itaendeleza juhudi za kuhimiza amani, ulinzi, maendeleo , urafiki na ushiriiano  baina ya mataifa mbalimbali.
Akizungumza kwa niaba ya serikali mpya ya Jamhuri ya Sudani ya Kusini ambayo ilijipatia uhuru wake rasmi julai  tisa, makamu wa Rais wa nchi hiyo  Bw.   Riek Machar,ambaye ndiye aliyeongoza ujumbe wa chini yake, katika tukio hilo alikuwa na haya ya kusema.
“Ninajisikia mwenye heshima na  fahari kubwa  kusimama mbele yenu na kuwasilisha salamu za serikali yangu na watu wake.  Kwa kukubali kwenu kulikaribisha  taifa hili jipya kuwa  Mwanachama wa Umoja wa Mataifa.
Akiongea kwa hisia , Makamu hiyo wa Rais alisema, harakati za nchi yake za kudai uhuru wake zimegharimu maisha ya mamilioni  ya watu ya, na kwamba kujitoa kwao mhanga hakutasahaulika kamwe.
“ Tulipoanza safari yetu hatukujua, licha  ya matumaini makubwa tuliyokuwa nayo wakatu ule,  kama  tungefikia hatua hii ya leo. Tunachotakiwa sasa ni kusonga mbele ili tuweze kutimiza mataratijo ya watu wetu”
Makamu huyo wa Rais alitoa wito kwa  nchi za Eritrea, Ethiopia na Somalia kutumia njia za majadiliano ili kumaliza migogoro inayoendelea katika nchi hizo. Aidha aliitaka  jumuia ya kimataifa  kukishughulikia kikundi cha Lord’s Resistance Army , kikundi ambacho kimekuwa kikiendesha mapigano na vitendo vya kikatili  nchi Uganda na katika baadhi ya nchi nyingine.
 Aidha  wawakilishi wa makundi ya nchi za Afrika, Asia, Ulaya Mashariki,  Amerika ya Latini,  Ulaya ya Magharibi na nchi nyingine,  pamoja na nchi mwenyeji Marekani nao walitoa hotuba za kulikaribisha taifa hilo jipya.
Baada ya Mkutano Mkuu kukamilisha shughuli  hiyo  kulifuatiwa shughuli ya kupandisha bendara ya  Taifa ya Jamhuri ya  Sudani ya Kusini.
Nchi ya mwisho kujiunga na  kuwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa ilikuwa ni Montenegro iliyojiunga  June 28 mwaka  2006 na kuwa nchi ya 192 baada ya kupata uhuru wake kutoka Serbia
Ujumbe wa  taifa jipya la Jamhuri ya Sudani ya Kusini, ukiwa umekaa rasmi katika sehemu yake ndani ya ukumbi Mkuu wa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa, baada ya kupitishwa kwa kauli moja kuwa mwanachama wa 193 wa Umoja wa Mataifa.
Walinzi wa Usalama wa Umoja wa Mataifa  wakijiandaa kuipandisha rasmi bendara ya  Jamhuri ya  Sudani ya Kusini. 
Viongozi wakuu wakiwa katika picha ya pamoja  mara baada ya  Bendara ya Jamhuri ya Sudani ya Kusini kupandishwa rasmi katika Umoja wa Mataifa. Kutoka Kushoto ni Rais wa Mkutano Mkuu wa  65 Bw. Joseph Deiss, Makamu wa Rais wa Sudani ya Kusini, Bw. Riek Machar, Ban Ki Moon, Katibu Mkuu  Umoja wa Mataifa na Dkt. Asha-Rose Migiro, Naibu Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa. 
Mjumbe  huyu wa Serikali ya Sudani ya Kusini, alishindwa kabisa kujizuia, akaamua kuserebuka kivyake vyake, akifurahia kupandishwa rasmi kwa bendera ya nchi yake, na kuwa bendara ya 193.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages