Breaking News

Your Ad Spot

Aug 21, 2011

MAMA SALMA KIKWETE AWAPA CHANGAMOTO WALIMU

Mwalimu  Mama Salma Kikwete
Na Anna Nkinda – Maelezo
Ili kuboresha elimu na kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi hapa nchini walimu wametakiwa kuwa karibu na wanafunzi wao na kuwapenda kwa kufanya hivyo wanafunzi watayapenda masomo wanayoyafudhisha na kuwaheshimu.
Wito huo umetolewa na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati akiwaaga walimu wanafunzi kutoka chuo kikuu cha Mtakatifu Augustino tawi la Mtwara waliokuwa wanafanya mazoezi ya kufundisha katika shule za Sekondari za WAMA – NAKAYAMA na Nyamisati zilizopo wilayani Rufiji mkoani Pwani.
Hafla hiyo fupi ya kuwaaga wanafunzi hao ilifanyika jana katika ofisi za Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) zilizopo ikulu jijini Dar es Salaam.
Mama Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa WAMA alisema kuwa kama mwalimu hatakuwa karibu na wanafunzi wake ni vigumu kwa wanafunzi  kuyapenda masomo anayoyafundisha pamoja na kumpenda mwalimu huyo.
“Ninyi hapa ni walimu wanafunzi ipo siku mtakuwa walimu kamili na mtakuwa  walimu wa darasa au walimu wa zamu hivyo basi ni lazima muwe karibu na wanafunzi , msikae nao mbali na kuwachukia kwa kufanya hivyo hawatawapenda hata kama  mtakuwa mnafundisha vizuri kiasi gani”, alisema.
Aidha Mama Kikwete  aliwataka walimu hao kufuata maadili yao ya kazi  ikiwa ni pamoja na kuvaa mavazi ya heshima jambo ambalo litawafanya wafanye kazi zao vizuri huku wakipata heshima kutoka kwa wanafunzi pamoja na jamii inayowazunguka.
Wakiongea kwa niaba ya wenzao Hango Tatu na Magoa Kaiza walisema kuwa licha ya wao kwenda kujifunza kufundisha katika shule hizo pia wamejifunza mambo mengi zaidi ambayo yatawasaidia katika kazi yao ya ualimu na maisha yao kwa ujumla.
Walisema, “Tumeona jinsi walimu wanavyofundishana namna ya kuwafundhisha wanafunzi jambo ambalo hatujawahi  kuliona , wanaandaa program, namna ya kuandaa somo na kutengeneza skimu ya kazi hakika inapendeza.
Sisi kama walimu shida kubwa inayotusumbua ni lugha ya kiingereza na somo la hesabu tulipata bahati ya kuhudhuria mafunzo ya Peaceful start ambayo yametusaidia sana,  tunahakika kuwa mafunzo haya licha ya kutusaidia katika kazi yetu ya ualimu pia yatatusaidia katika maisha yetu ya baadaye”.
Kwa upande wa wanafunzi waliokuwa wanawafundisha walisema kuwa wanafunzi hao wananidhamu , hawahitaji kusukumwa huku wakifuata ratiba wanayopangiwa  ukilinganisha na wanafunzi wa shule zingine ambazo wamewahi kufundisha kwani mwanafunzi bila kuwa na nidhamu hawezi kusoma vizuri.
Kutokana na utaratibu wa vyuo kuwapa fursa wanafunzi wake kwenda kufundisha kwa vitendo katika shule mbalimbali hapa nchini shule hizo zilipokea walimu wanafunzi saba kutoka chuo kikuu cha Mtakatifu Augustine tawi la Mtwara  ambao walifundisha  kwa kipindi cha mwezi mmoja.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages