Breaking News

Your Ad Spot

Dec 20, 2011

AFRIKA YATAJA VIPAUMBELE MKUTANO WA RIO+20

 Mhe. Ombeni Sefue,

Na Mwandishi Maalum, New York
Wakati maandalizi ya mkutano wa kimataifa  kuhusu  Maendeleo Endelevu ( United Nations Conference on Sustainable Development) maarufu kama  RIO+20   yakiwa yanaendelea, Afrika imetoa vipaumbele vyake ambavyo inataka vizingatiwe wakati wa  mkutano  huo  unaotarajiwa kufanyika mwezi Juni,2012, Rio de Janairo,  Brazil.

Balozi  wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Mhe.Ombeni Sefue (pichani) akizungumza kwa niaba ya kundi la nchi za Afrika katika Umoja wa Mataifa. Amesema vipaumbele hivyo vinapashwa kuzingatiwa kwa kuwa ni muhimu katika kufikia malengo ya kuondoa umaskini hasa kwa   Afrika kupitia mkakati mpya wa  uchumi wa kijani.

 Anavitaja vipaumbele hivyo kuwa ni pamoja na,   uboreshaji wa uzalishaji wa kilimo na usalama wa chakula,  kupambana na kudhibiti  kuenea kwa jangwa na uharibifu wa ardhi,  usimamizi wa mazingira ya  bahari, uimarishaji wa matumizi endelevu ya maliasili ikiwa ni pamoja na  maji safi, misitu na viumbe hai. 

Vipaumbele vingine ni  kukuza matumizi  na uzalishaji  endelevu na maendeleo ya viwandani na kuhakikisha usimamiaji wa kemikali taka, kukuza utalii  endelevu na kuhakikisha upatikanaji wa nishati  salama na endelevu.

Kwa siku mbili wadau mbalimbali wakiwamo mabalozi walikutana katika majadiliano ya  ya siku mbili  hapa Umoja wa Mataifa ambapo pamoja na mambo mengine, walijadili maandalizi ya mkutano  huo muhimu  na ambao utawakutanisha wadau mbalimbali kutoka duniani kote, wakiwamo wakuu wa nchi na serikali,  wanadiplomasia, wanasiasa, wataalamu wa masuala ya maendeleo endelevu,   mazingira , tasisi binafsi na za kiraia.

Balozi Sefue anasema   ni matarajio ya Afrika kwamba, washiriki wa mkutano huo siyo tu watajituma bali pia wataonyesha utashi wa kisiasa katika kuhakikisha kwamba mkutano huo unafanikiwa na kutoka na malengo yanayotekelezeka na ambayo yatakuwa na manufaa kwa vizazi vijavyo.

“Kundi la afrika linatoa wito kwa jumuia ya kimataifa kuonyesha dhamira  na utashi wa kisiasa ili  katika mkutano  huo wa RIO+20 tuwezwe  kutoka na  habari yenye matumaini kwa vizazi vijavyo . 

Afrika pia  inapenda kukaribisha kuanzishwa kwa  mfumo ambao utasimamia na kufuatilia  makubaliano yatakayofikiwa na, pamoja na utekelezaje wake kama suala la dharura” akasema Balozi Sefue.

Akitilia mkazo wa vipaumbele vya Afrika katika suala zima la maendeleo endelevu, Balozi Ombeni  Sefue ambaye kwa  miezi miwili mfululizo, Tanzania   imekuwa Mwenyekiti wa Kundi la  Nchi za Afrika.

Anasema  mtizamo wa  Afrika ni kutaka kuona kwamba nguzo kuu tatu muhimu kwa  maendeleo endelevu zinapewa umuhimu unaolingana bila ya mmoja kupewa uzito wa kipekee.

Anasema “ Afrika inapenda kutoa  wito  na kusisitiza  umuhimu wa ushirikiano wa uwiano katika nguzo hizo tatu  hasa nguzo ya kuondoa umaskini, bila ya kuongeza mzigo wa ziada kwa nchi zinazoendelea au  kuwekwa vikwazo au kuhoji kuhusu matarajio yetu ya maendeleo”

Akaongeza  Afrika ingepeda kuona  pia kwamba harakati zozote za kubadili mifumo ya kiutendaji ya taasisi za Umoja wa Mataifa ikiwamo ile ya mazingira  UNEP inazingatia maslahi ya  Afrika. 

Wakati maandalizi ya mkutano huo yakiendelea, kumejitokeza   dalili za  waziwazi ambapo nchi zilizoendelea zimekuwa zikilipa uzito wa aina yake nguzo ya  mazingira na kutoa mkazo kidogo katika nguzo ya kuondoa umaskini na hasa ikizingatiwa kwamba nguzo ya mazingira inalenga kuwanufaisha zaidi  nchi zilizoendelea kuliko nchi zinazoendelea ambazo kwao nguzo ya muhimu zaidi  ni kuondokana na umaskini.

Nembo ya mkutano wa Rio+20
Mkutano wa RIO+20 utafanyika ikiwa ni miaka 20 kupita tangu mkutano mwingine kama huo  uliobeba ajenda ya Mazingira na Maendeleo maaruku kama  (Earth Summit) ulipofayika mwaka 1992 huko huko  Rio de Janairo.  Mkutano wa mwakani utatoa fursa ya kufanya tathmini ya makubaliano yaliyofikiwa mwaka 1992, kipi kimefanyika, wapi pameshindikana na kwa nini na hali kadhalika kutoa mwekeleo wa miaka 20 ijayo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages