Breaking News

Your Ad Spot

Mar 28, 2012

NI KOSA KURANDA RANDA VITUONI BAADA YA KUPIGA KURA:JAJI LUBUVA


Jaji Mstaafu Damian Lubuva

 USA RIVER
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imeonya kuwa ni kosa kisheria watu kuranda randa au kukaa makundi kwenye vituo vya uchaguzi baada ya kupiga kura.


Onyo hilo limetolewa leo na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Mstaafu, Damian Lubuva, katika mkutano wake na viongozi wa vyama vya siasa vinavyoshiriki katika uchaguzi mdogo jimbo la Arumeru Mashariki.


"Tumekuwa tukisisitiza kila mara kwamba ni kosa kisheria mtu au kundi la watu kuzagaa kwenye vituo baada ya kupiga kura. Ndugu viongozi sisitizieni sana wananchi kwamba ni vema baada ya kupiga kura kila mmoja arudi nyumbani kusubiri matokeo", alisema Jaji Lubuva.


Alisema, ni kufanya kosa lisilo la lazima wapiga kura kubaki vituoni au kuranda randa au kuweka vikundi kwenye vituo, kwa sababu wapo mawakala waliowekwa na vyama vyao ambao ndiyo wenye dhamana ya kulinda kura.


Jaji Lubuva alisema, vyama vyote vinapaswa kutaja mawakala wao mapema badala ya kuwaweka katika hatua za mwisho jambo ambalo alisema linaweza kusababisha uwezekano wa chama kukosa wakala.


Alisema, kila chama kina wajibu wa kuweka wakala wake ambaye kitamgharamia na kwamba kutokuwepo wakala kwa chama chochote hakutaathiri mwenendo wa upigaji kura au kuathiri kutangazwa matokeo.


Jaji Lubuva alisema, maandalizi ya uchaguzi huo ambao utafanyika Aprili Mosi mwaka huu, yamekamilika na TUme hiyo imejitahidi kuhakikisha hazitokei kasoro zisizo za lazima.


Katika uchaguzi huo, vyama vinane vimeweka wagombea kama ifuatavyo, majina ya vyama vyao yakiwa kwenye mabano,Mazengo Abdallah Adam (AFP),Sumari Sion Solomon (CCM),Nassari Joshua (CHADEMA), Muhammad Abdalla Mohammed (DP), Hamis Juma Kiemi(NRA),Kirita Shabani Moyo (SAU),Chipaka Abraham Moova (TLP) na Charles Mosses Msuya( UDP).


Uchaguzi huo unafanyika kufuatia aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM, Jeremia Sumari kufariki dunia mapema mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages