Breaking News

Your Ad Spot

Jul 19, 2012

CCM YATOA POLE AJALI YA MELI ZANZIBAR

Nape

DODOMA, TANZANIA
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetoa pole kwa wale wote ambao wamepatwa na msiba katika ajali ya meli iliyotokea jana, Zanzibar.
Pamoja na pole, CCM  imeitaka serikali kuipitia upya taarifa ya Tume iliyoundwa kuchunguza ajali ya kwanza ya meli ya Mv. Spice Islander na kuitaka  serikali kuchukua hatua za haraka pale itakapobainika kuwepo kwa uzembe kwa watendaji wowote bila kujali nyadhifa zao.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi CCM,  Nape Nnauye, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa leo kuhusu ajali hiyo.
Nape alisema kuna umuhimu mkubwa wa kuipitia upya kwa taarifa hiyo kwani inawezekana kuna baadhi ya mambo hayakufuatiliwa kwa kina na au kuna uzembe unafanyika.
Alisema endapo kutabainika kuwepo kwa uzembe basi wale wote wanaohusika na uzembe huo wawajibike wenyewe kwani haiwezekani watumie fedha za wananchi lakini hakuna linalofanyika.
“Ni Muhimu tufike wakati wewe kama kiongozi unapoona jambo limekushinda au limetokea kutokana na uzembe na wewe kiongozi upo tujenge tabia ya kujudhuru hii itasaidia kuleta heshima zaidi’’ alisema Nape.
Alisema hali hiyo inatokana na ukweli kuwa mara kwa mara tukio la kuzama kwa meli au ajali mambo mbalimbali hujitokeza ikiwemo uzito wa mizigo au idadi kubwa kuliko uwezo wa meli au uchakavu.
Nape alisema vyombo vinavyohusika ni lazima kuwa makini na watendaji wake kama wameshindwa kufanya kazi ni bora wawajibike wenyewe au wawajibishwe na mamlaka  za juu.
“Sasa meli inaondokaje bandarini ikiwa imebeba abiria zaidi au mizigo zaidi ya uwezo wake wakati kuna watu wanaohusika na kazi hiyo, hii inatia shaka kidogo na huko ni kuwaibia wananchi kwa kutowajibika ’’
Kwa mujibu wa Katibu huyo alisema hivi sasa inaonekana kuwa usafiri wa ndege umekuwa ni wa uhakika zaidi lakini hilo linatokana na ukweli kuwa watendaji wake wamekuwa makini kila wakati.
Aidha Nape alisema kutokana na msiba huo ulitokea CCM imehairisha Mkutano wake wa hadhara ambao walipanga kufanyika Kigoma jana .
Alisema sasa mkutano huo utafanyika siku ya Jumapili  baada ya kumalizika kwa siku za maombolezo zilizowekwa na serikali.
“Tunatoa pole kwa wale wote waliofikwa na msiba na kwa wale ambao bado wanaugua kutokana na jail hiyo tunamuomba Mungu awaeze kuwasaidia waweze kupona haraka.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages