Breaking News

Your Ad Spot

Jul 23, 2013

UNESCO YAWATAKA WATENDAJI WA REDIO ZA KIJAMII WILAYANI KARAGWE KUFANYA KAZI KWA KUFUATA MAADILI

IMG_0093
Mshauri Mwelekezi masuala ya utawala bora Bw. Wilbert Kitima akiendesha mafunzo kwa washiriki wa Redio Jamii yaliyofanyika mjini Kayanza, wilayani Karagwe mkoa wa Kagera na kumalizika mwishoni mwa Juma. Kushoto ni Mshauri wa Radio Jamii kutoka UNESCO Rose Haji Mwalimu
IMG_0549
Afisa Mipango Taifa wa Kitengo cha Mawasiliano na Habari UNESCO Yusuph Al Amin akizungumzia mahitaji muhimu kiuwezeshaji utoaji wa taarifa na kufafanua kuwa mradi huo utasaidia kutoa fursa kwa jamii kujadili masuala ya maendeleo kupitia redio za kijamii hivyo kuwezesha na kurahisisha upatikanaji wa habari kupitia redio hizo.
IMG_0477
Mkurugenzi wa Radio Jamii visiwani Zanzibar Hamad Shapandu (aliyesimama) akiwasilisha changamoto zinazoikabili kituo chake kwenye kikao cha kitaifa cha kujadili mradi wa Sida kutathmini kazi za mwaka uliopita kuona mafanikio yaliopatikana, kuzichanganua kero zilizojitokeza katika utekelezaji na mpango kazi kwa mwaka ujao kwa Afisa Mipango Taifa Kitengo cha Mawasiliano na Habari UNESCO Yusuph Al Amin (aliyeketi) wilayani Karagwe mkoa wa Kagera.
IMG_0528
Usia Nkhoma Ledama kutoka Kitengo cha habari cha Umoja wa Mataifa (UNIC) akitoa somo kwa viongozi wa redio jamii kuhusu umuhimu wa kuwepo uwazi wa taarifa na habari zao katika mitandao ya kijamii ili kuongeza ufanisi na soko la kazi zao kujulikana Kimataifa na kuongeza nafasi ya kujipatia matangazo katika redio zao za kijamii.
IMG_0495
Mshauri wa Radio Jamii kutoka UNESCO Mama Rose Haji Mwalimu amesema kupitia mradi huo watendaji wa vyombo vya habari katika jamii wana nafasi kubwa ya kuhamasisha jamii katika mijadala ya maendeleo na kudumisha amani katika taifa. Kushoto aliyeketi ni Afisa Mipango Taifa wa Kitengo cha Mawasiliano na Habari UNESCO Yusuph Al Amin.
IMG_0480
Meneja wa Kituo cha redio ya Jamii FADECO ya Wilayani Karagwe Adeline Lweramula akitoa maoni namna ya kuboresha utekelezaji wa mradi wa SIDA unaofadhili mafunzo ya redio za Jamii wakati wa kikao cha kitaifa cha kujadili mradi wa huo kutathmini kazi za mwaka uliopita kuona mafanikio yaliopatikana, kuzichanganua kero zilizojitokeza katika utekelezaji na mpango kazi kwa mwaka ujao.

NA MWANDISHI WETU, KARAGWE
Watanzania wenye nafasi mbalimbali za kutoa huduma kwa jamii, wameshauriwa kuondoa tabia ya kuogopana na kuoneana haya katika utendaji wa majukumu yao, ili mchango wao usaidie katika utendaji wenye tija katika sekta wanazozisimamia.

Akizungumza na mameneja na wajumbe wa bodi za redio za jamii Tanzania katika mkutano maalum wa wiki moja ulioandaliwa na Unesco wilaya ya Karagwe mkoa wa Kagera, Mshauri Mwelekezi masuala ya utawala bora Bw. Wilbert Kitima amesema kuwa maeneo mengi yamekosa ufanisi kwa kuwa na watendaji wasio na sifa.

Amewaagiza watendaji hao kufanya kazi kwa kufuata sheria wakifahamu kuwa vituo wanavyosimamia ni vya jamii, hivyo havinabudi kuendeshwa ipasavyo, wakifahamu uajibikaji sio kufanya kazi tu za kiofisi bali matokeo mazuri ndio kigenzo cha ufanisi, badala ya kukumbatia nafasi zote za kiutendaji.

Amefahamisha kuwa vyombo vya jamii vinakabiliwa na changamoto nyingi za kiutendaji kutokana na vianzio vya ukusanyaji wa mapato, hivyo hawanabudi kuwa wabunifu, waadilifu na waaminifu, wenye msimamo thabiti wa kusimamia kazi zao kwa maslahi ya jamii na kuacha tabia yakuishi kwa udalali ambayo haina maslahi katika kuziendesha redio zao na kufanya kila linalowezekana kuepusha majungu katika kuendesha vituo hivyo.

Mshauri wa Radio Jamii kutoka UNESCO Rose Haji Mwalimu amesema pamoja na mafunzo ya ujasiriamali katika kuendesha vituo hivyo pia watawezeshwa kufanyakazi na washauri waelekezi wa serikali za mitaa na halmashauri za wilaya.

Amesema kutafanyika uzinduzi wa ushirikiano wa redio FADECO na Shirika la simu la Airtel katika kufanyakazi kwa ushirikiano baada ya shirika hilo kuruhusu transmita ya redio Fadeco, kuwekwa katika mnara wa Airtel kuongeza wigo kwa wasikilizaji wa redio hiyo ambao walikuwa hawajapata huduma ya matangazo watanufaika baada ya matangazo kwenda mbali zaidi.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Meneja wa Redio Fadeco Adeline Lweramula , pia kutafanyika uzinduzi wa mtandao wa taarifa za wanahabari watoto, wanaoandaa vipindi vya watoto na redio Fadeco chini ya shirika la Umoja wa Mataifa la Unicef.

Aidha kutafanyika uzinduzi wa kampeni ya mwaka mmoja kupiga vita unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto wa wilaya ya Karagwe.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages