Breaking News

Your Ad Spot

Sep 13, 2013

WASHENZI WAZIDI KUCHAFUA AMANI ZANZIBAR, WAMMWAGIA TINDIKALI PADRI

 Padri Anselmo Mwang'amba akiwa kitandani kwenye wodi ya Mapinduzi Mpya, hospitali ya Mnazi mmoja mjini zanzibar, Padri Mwang'amba alimwagiwa tindi kali, Padri Anselmo Mwang'amba wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mpendae Jimbo la Zanzibar leo katika eneo la Mlandege mjini Zanzibar majira ya saa 10 jioni. Kufuatia tukio hilo, Natibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai amelaani kitendo  hicho alipofika hospitalini kumjulia hali Padri huyo. Picha na Martin Kabemba.
 ZANZIBAR, Tanzania
PADRI wa Kanisa Katoliki, Parokiya ya Mpendae Anselmo Mwan'gamba amemwagiwa tindikali usoni na watu wasiojulikana wakati akitoka kupata huduma za mawasiliano ya Intaneti, eneo la Mlandege.

Kamanda wa Polisi mkoa wa mjini Magharibi Unguja, Mkadam Khamis  alithibitisha kutokea kwa tukio hilo ambapo alisema uchunguzi wa kina umeanza.

'Tumepokea taarifa ya tukio lakini uchunguzi wa tukio hilo na kujuwa chanzo na mtandao wa wahalifu hawa umeanza'alisema.

Kwa mujibu wa taarifa za daktari wa hospitali ya Mnazi mmoja ambaye alimpokea padri huyo kwa ajili ya kupata matibabu ya kwanza Abdalla Haidari alisema ameumiya sehemu ya uso pamoja na kifua.

'Padri Mwan'gamba amejeruhiwa na maji ambayo baada ya kuyafanyia uchunguzi tumegunduwa kuwa ni tindikali katika sehemu za uso na kifua'alisema.

Kwa mujibu wa maelezo ya padri Mwan'gamba alisema alishambuliwa na watu ambao hawafahamu wakati akitoka katika duka linalotoa huduma za mtandao wa mawasiliano ya Intaneti hapo Sunshine Mlandege katika majira ya jioni saa kumi.

'Wakati natoka katika duka la kupata huduma za mawasiliano ya Intenate nilimwagiwa maji makali ambayo nilihisi kwamba ni tindikali na kuamuwa kwenda moja kwa moja katika hospitali ya Mnazi mmoja'alisema.

Mfanyakazi mmoja wa duka linalotoa huduma za mawasiliano ya Intenate aliyejitambulisha kwa jina la Salma alikiri kutokea kwa tukio hilo ambapo mteja wake alipata huduma hapo.

"Wakati anatoka baada ya kupata huduma mara namuona anarudi na kulalamika kwamba amemwagiwa tindikali katika sehemu za uso" alisema.

Hilo ni tukio la tano kwa watu mbali mbali kumwagiwa tindikali mjini hapa ambapo hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa kuhusika na ukatili huo, Padri mwangamba ni mkuu wa kituo cha malezi cha vijana kiliopo Cheju mkoa wa kusini Unguja ambacho hutunza vijana kwa ajili ya kuwapatia mafunzo mbali mbali.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages