Breaking News

Your Ad Spot

Oct 28, 2013

RAIS KIKWETE AMPONGEZA RAIS JAMAL MALINZI WA TFF

Rais Jakaya Kikwete
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameupongeza uongozi mpya wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) chini ya Rais wake, Bwana Jamal Malinzi, uliochanguliwa usiku wa jana, Jumapili, Oktoba 27, 2013.

Katika salamu za pongezi ambazo Rais Kikwete amemtumia Bwana Malinzi, Rais Kikwete ameutakia mafanikio uongozi huo akisisitiza kuwa ni muhimu kwa uongozi mpya kuwekeza ipasavyo katika soka badala ya kuwekeza katika migogoro na kufanya jitihada za kujiendeleza binafsi.

Amesema Rais Kikwete kwa Bwana Malinzi na uongozi mzima wa TFF: “Nimefurahi kupata taarifa ya kuchaguliwa kwenu kuongoza Shirikisho la Soka Tanzania (TFF). Nakupongeza wewe binafsi Bwana Jamal Malinzi kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa TFF na kupitia kwako nawapongeza viongozi wenzako ambao umechaguliwa nao.”

“Hii ni heshima kwenu. Hakuna shaka kuwa mmepata ridhaa ya wananchi wetu kusimamia shughuli za mchezo unaopendwa na wananchi wengi nchini. Wananchi hawa wana matarajio makubwa kwenu kuwa mtatumia muda mwingi katika kuwekeza katika soka badala ya kuwekeza katika migogoro isiyoisha. Migogoro imekwamisha sana maendeleo ya soka katika nchi yetu na kuwanyima watu wetu raha ambayo wanaitaraji kutoka kwenye mchezo huo na hasa pale timu zetu zinapopata ushindi.”

Amesisitiza Rais Kikwete: “Aidha ni matarajio na matumaini ya wananchi, na hasa mamilioni ya wapenda soka katika nchi yetu, kuwa mtawekeza ipasavyo katika maendeleo ya mchezo huo badala ya kuwekeza katika maendeleo binafsi na kujiendeleza binafsi.”

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages