Breaking News

Your Ad Spot

Nov 6, 2013

DK. NCHIMBI AWATAKA WENYEVITI WA CCM KUFANYA KAZI YA KUPANGA SAFU ZA USHAMBULIAJI KAMA KIPA UWANJANI

*ASEMA CHADEMA BADO WACHANGA KUIIWA WATANI WA JADI WA CCM

 Kada mahiri wa CCM, Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi, akisisitiza jambo, alipozungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya kikazi ya siku tatu kwa wenyeviti wa CCM wa kata 31 za wilaya ya Kinondoni, leo, Nov 5, mjini Dodoma. Kushoto ni Katibu wa CCM mkoa wa Dodoma Albert Mgumba na kulia ni Katibu wa CCM Wilaya ya Dodoma mjini, Saad Kusilawe na Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kinondoni, Salum Madenge.

DODOMA, Tanzania
WENYEVITI wa CCM, katika ngazi mbalimbali wameaswa kwamba pamoja na majukumu yao yote lazima wafanye kazi ya kupanga safu za kuimarisha Chama kama wafanyanyavyo magolikipa kuwapanga wacheji wa timu zao za soka wawapo uwanjani kupambana na adui.

Wametakiwa kutolitelekezajukumu hilo la kupanga safu na badala yake kwenda kwenye ushambuliaji na kwamba kufanya hivyo ni sawa na kosa la kipa kuliacha wazi goli na  kwenda kujiunga na washambuliaji.

Hayo yamesemwa na Kada wa CCM, Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi wakati akifungua semina ya mafunzo maalum ya kikazi kiwa Wenyeviti wa CCM Kata zote za Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, leo mjini Dodoma.

"Ndugu zanguni, kazi kubwa ya Mwenyekiti ni kukaa nyuma kabisa akipanga safu na kuangalia jinsi watendaji wanavyofanya kazi, kwa lengo la kuhakikisha yanafanyika marekebisho ya haraka pale utendaji unapokuwa unakwenda vibaya", alisema Dk. Rehema Nchimbi.

Alisema, moja ya uzimamizi huo ni kuhakikisha kila kiongozi wa CCM na watendaji serikalini wanatekeleza ilani ya CCM kwa umahiri mkubwa, na kuhakikisha hatua kali zinachukuliwaa kwa watendaji au kiongozi yeyote anayekwenda kinyume.

Ninyi wenyeviti wa CCM katika ngazi zote na wana CCM wote kwa jumla, ni lazima kuhakikisha kuwa mtendaji hata akiwa mwajiriwa katika serikali anatekeleza ilani ya Chama kwa kuwaa kazi aliyoomba au kukabidhiwa na serikali ndiyo hiyo.

"Inashangaza sana, unakuta mtendaji au mtumishi wa serikali, anasema yeye siyo mwana siasa,Kha! siyo mwanasiasa vipi, wakati aliyekupa kazi ni CCM iliyopewa dhamana ya kuunda serikali?", alisema, Dk. Rehema Nchimbi na kuhoji.

"Najua tupo viongozi, watendaji na watumishi wa umma, wenye tabia ya kujifanya wao hawana uhusiano kiabisa na CCM, sasa ninyi wenyeviti na viongozi wengine na wanachama wa CCM, hakikisheni watu wa aina hii mnashughulika nao bila kuwaonea haya", alisema Dk. Rehema na kuongeza;

"Ninyi mnapowaona watu wa aina hii shughulikieni nao papo hapo, msiwaache na kubaki mnalaumu serikali. Vinginevyo kama mnawaacha mambo yakienda kombo msilaumu serikali mjilaumu wenyewe kwa sababu mnakuwa mmeacha jukumu lenu la kusimamia utendaji na utekelezaji wa ialni ya Chama".

Aidha Dk. Rehema Nchimbi amewashangaa wanaovipa hadhi ya utani wa jadi na CCM, vyama vya upinzani kama Chadema, akisema, vyama hivyo husuasan Chadema bado ni vichanga sana na hivyo havina hadi hiyo ya kuwa mtani wa jadi wa CCM.

"Ukisikia watani wa jadi kama Simba na Yanga, lazima ujue kwamba wanaitwa hivyo kwa sababu zote ni timu za miaka mingi zenye nguvu karibu sawa katika soka", lakini sasa hawa Chadema wa juzi juzi utawatajaje kuwa ni watani wa CCM? huu ni mzaha wa ajabu kabisa", alisema, Dk. Rehema Nchimbi na kuongeza.

"Jamani CCM, siyo chama cha kulinganishwa au kuwekwa kwenye ushindani na vyama kama Chadema, ni chama kikongwe ingawa siyo kizee, ila kwa kuwepo miaka mingi, maana chama hakizeeki kama kiumbe hai chenyewe kinaendana na mabadiliko kila wakati".

Dk. Rehema alisema, amekuwa akitamba kuhusu uimara wa CCM kwa kuwa anaifahamu kwa muda mrefu na kutambua kwamba ni chama pekee cha wananchi kilichopo kwa maslahi ya wananchi.

Mkuu huyo wa mkoa wa Kada wa CCM, alipingana na wale wanaodhani kwamba CCM inaweza kufa kirahisi akisema kwamba, siyo rahisi chama hicho kufa kwa kuwa kifo chake kitakuwa sawa na kufa taifa la Tanzania.

Katika semina hiyo washiriki wanatarajiwa kupata ustadi mkubwa wa kiutendaji kutokana na mada zinatakzotolewa na wakufunzi mahiri katika muda wa semina hizo inayotarajiwa kumalizika Alhamisi wiki hii.

 Washiriki wakimsikiliza Dk. Rehema Nchimbi (kulia) walipokuwa akifungua mafunzo ya wenyeviti wa CCM wa Kata za wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, leo mjini Dodoma.

 Mwenyekiti wa CCM, wilaya ya Kinondoni, Salum Madenge, akimshukuru Dk. Rehema kwa kufungua mafunzo hayo.
Washiriki wakishangilia baada ya mafunzo hayo kufunguliwa rasmi na mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk. Reheme Nchimbi.
 Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo maalum kwa wenyekiviti wa CCM Kata za Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, baada ya kufungua mafunzo yao leo mjini Dodoma.
Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi akiagana na Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kinondoni, Salum Madenge baada ya kufungua semina ya Wenyeviti wa CCM Kata zote za wilaya ya Kinondoni, DSar es Salaam, leo mjini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages