Breaking News

Your Ad Spot

Jun 30, 2014

WAZIRI WA MALISILI NA UTALII AZINDUA MAONYESHO YA KIMATAIFA YA UTALII YA SWAHILI INTERNATIONAL TOURISM EXPO (SITE)

2a
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano Bw. Goefrey Tengenea wa pili kutoka kulia akiwa katika picha ya pamoja na maofiza wenzake wa TTB wakati wa hafla hiyo.
................................................................................................
(HOTUBA YA MH. WAZIRI RAZALO NYALANDU WAKATI WA UZINDUZI WA SITE)
Napenda kuchukua nafasi hii kutoa shukrani zangu za dhati, kwa wageni wote mliofika katika tukio hili muhimu ambapo nitatambulisha kwenu kuanzishwa kwa onesho jipya la utalii la kimataifa litakalojulikana kwa jina la Swahili International Tourism Expo (S!TE).
1. Sekta ya Utalii ni kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi hasa kwa kuchochea ukuaji wa sekta nyingine za kiuchumi kama vile usafirishaji, viwanda na biashara, kilimo, sanaa za mikono na kadhalika. Sekta ya utalii ina uwezo wa kuongeza ajira kwa haraka zaidi na inatambulika kwamba kila mtalii mmoja anapokuwa nchini huchangia takribani nafasi 12 za ajira za aina mbalimbali. Aidha, Utalii ni tasnia muhimu katika kuongeza kipato na kupunguza umasikini, kukuza mahusiano ya kijamii na vile vile katika kutunza na kuendeleza maeneo ya kihistoria na maliasili. Hapa nchini, katika kipindi cha kati ya mwaka 2002 na 2013, utalii wa kimataifa umekuwa kwa zaidi ya asilimia 50%, kutoka watalii 575,000 mwaka 2002 wambao waliliingizia taifa Dola za Marekani milioni 730 hadi kufikia watalii 1,135,884 mwaka 2013 ambao waliingizia taifa Dola za marekani Bilioni 1.81.
2. Tanzania imebarikiwa kwa kuwa na vivutio vya maliasili na utamaduni vya kipekee. Kutokana na kuwepo kwa vivutio hivi, taasisi ya Kimataifa ya World Economic Forum katika taarifa yake ya ushindani kwenye tasnia ya Utalii (Travel and Tourism) imeitaja Tanzania kuwa ni nchi ya pili (2) duniani ikiongozwa na Brazili kwa kuwa na mazingira asilia yenye Urithi asilia wa kimataifa, wingi wa wanyamapori na ardhi kubwa iliyo hifadhiwa. Hakika, ni ukweli usiopingika kwamba katika vivutio saba vya maajabu ya asili katika bara la Afrika, vitatu vinatoka Tanzania. Huu ni ushuhuda kwamba juhudi zetu za kuhifadhi mazingira zinazaa matunda. Hivi sasa Bonde la Ngorongoro; hifadhi ya Taifa ya Serengeti, na Mlima Kilimanjaro ni vivutio ambavyo vimeorodheshwa katika Maajabu saba ya asilia barani Africa.
3. Hata hivyo, hatuwezi kutegemea tu uwingi na ubora wa vivutio hivi vya utalii peke yake. Ni muhimu kuongeza juhudi zaidi kuliko wakati mwingine wowote, ili kujenga uelewa wa utajiri huu kidunia. Kama taifa, tunahitaji juhudi na mikakati zaidi ili kutangaza vivutio vyetu.
4. Kwa kuzingatia umuhimu wa kuendelea kutangaza utalii wetu na kuifaya Tanzania iweze kushindana kimataifa, mnamo mwezi Februari, 2013, Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), iliingia makubaliano na kampuni inayojulikana kama Pure Grit Project and Exhibition Management LTD, hapo mwanzo ilijukana kama Witch & Wizard Creative (Pty Ltd) ili kuanzisha maonyesho ya utalii ya kimataifa nchini Tanzania yajulikanayo kama Swahili International Tourism Expo -S!TE), ambayo yataanza rasmi Mwezi Oktoba, 2014. Pure Grit Project and Exhibition Management LTD ni kampuni inayoendesha maonesho ya utalii ya INDABA ambayo ni maonesho ya tatu kwa ukubwa duniani. Onesho la S!TE litafanyika hapa Dar es salaam, mwezi Oktoba kila mwaka katika ukumbi wa mikutano wa Mlimani City na kujikita zaidi katika kuvutia washiriki kutoka ndani nan je ya nchi.
5. Mkoa wa Dar es Salaam umechaguliwa mahsusi kuwa eneo la kufanyika kwa onesho la S!TE kutokana na sehemu ulipo Mkoa huo kijiografia, na uwepo wa miundombinu bora na huduma nzuri zinazofaa kwa kuendesha au kuanzisha maonyesho ya utalii ya kimataifa.
6. Hadi kufikia Juni 2014, hali ya maandalizi ya onesho hili ni kama ifuatavyo.
6.1 Mwenendo wa idadi ya washiriki hadi sasa: Zaidi ya asilimia 50% ya nafasi za maonesho hayo tayari zimejazwa kwa kuchuliwa na makampuni binafsi na Bodi za Utalii za nchi mbalimbali. Aidha, kuna idadi kubwa na ya kuridhisha ya maombi ya washiriki inayoendelea kuandaliwa. Lengo ni kwamba ifikapo katikati ya mwezi Agosti, 2014 tuwe tumetumefikia asilimia 100.
6.2 Programu maalum ya kuwaleta nchini wakati wa maonesho hayo mawakala wakubwa wa biashara ya Utalii: Katika kuhakikisha kuwa onesho hili linakuwa ni fursa ya kuwaunganisha wafanyibiashara ya Utalii wa Tanzania na masoko ya Utalii, S!TE itakuwa na programu maalum (Hosted buyer and travel writer programme) ya kuwaleta nchini wakati wa maonesho hayo mawakala wakubwa wa biashara ya Utalii na waandishi wa habari za utalii (Tour Operators, Wholesalers, Packagers and Travel Agents and Travel Writers) na kuwapangia ratiba maalum ya kuonana na washiriki wa maonesho hayo ili kuwawezesha kuanzisha uhusiano wa kibiashara. Mawakala hao wapatao ishirini na wandishi wa habari kumi watagharimiwa (hosted) na S!TE.Hadi kufikia Juni 2014,mawakala 13 kutoka Marekani, Australia, Ujerumani, Uholanzi, India, Mexico, Norway na China wamethibitisha ushiriki wao.
6.3 Utangazaji wa Onesho la S!TE: Onesho la S!TE lina tovuti ijulikanayo kama www.site.co.tz. Tovuti hii imeandaliwa ili kukidhi maudhui ya onesho lenyewe ambapo inataarifa nyingi zinazoweza kumfanya yeyote anayetembelea tovuti hiyo kupata taarifa zote muhimu kwa muda mfupi. Kwa mfano tovuti inatoa taarifa za ukumbi wa onesho, mabanda ya maonesho yatayojengwa na kumruhusu mteja kuchagua eneo kulingana na uwezo wake. Aidha, tovuti hii ambayo pia imeunganishwa na ukurasa wake wa Facebook, inapatikana kwa lugha mbalimbali
7. Pamoja na kuitangaza Tanzania kama kituo muhimu cha utalii katika ukanda wa Afrika ya Mashariki, S!TE ina lengo la kuunganisha wafanya biashara wa Utalii wadogo na wa kati wa Tanzania (Small and Medium Tourism Enterprises - SME’s), na masoko ya utalii ya kimataifa. Ni ukweli kwamba SME’s za kitanzania zina uwezo mdogo wa kimtaji wa kuweza kufikia masoko ya utalii ya kimataifa. Kupitia S!TE, hasa kupitia programu maalum ya kuwaleta nchini wakati wa maonesho hayo mawakala wakubwa wa biashara ya Utalii, itasaidia katika kutatua changamoto hii.
Naomba watanzania kuchangamkia fursa hii muhimu katika kukuza biashra ya Utalii nchini.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages