Breaking News

Your Ad Spot

Oct 2, 2014

UZINDUZI WA REDIO JAMII UVINZA: MKUU WA MKOA AHIMIZA WELEDI, UADILIFU NA AMANI


DSC_0177
Mkuu wa Wilaya ya Uvinza Mwalimu Hadijah Nyembo (kulia) akitoa nasaha zake kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya (wa pili kulia) kuzungumza na wakazi wa wilaya ya Uvinza kwenye sherehe za uzinduzi wa kituo cha redio jamii Uvinza FM mkoani Kigoma. Kutoka kushoto ni Meneja wa huduma za kijamii wa Airtel Tanzania, Hawa Bayumi, Mshauri na Mkufunzi kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) ambao ndio wadhamini wakuu wa redio Uvinza FM, Bi. Rose Haji Mwalimu na Mkurugenzi Mtendaji wa Uvinza FM Radio Bi. Nuru Kalufya.(Picha na Zainul Mzige wa MOblog).
Na Mwandishi wetu, Uvinza - Kigoma
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya amesisitiza uadilifu katika vyombo vya habari jamii kwa kutangaza habari zisizoumiza hisia kwa wananchi wengine na kuepuka migogoro.
Akizindua kituo cha redio jamii cha Uvinza FM, Luteni Kanali Mstaafu Machibya alisema kuwa vyombo vina wakati mgumu hasa katika kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu mwaka 2015.
“Changamoto hii inaweza kuepukika kwa kuhakikisha habari zinazotolewa zinalenga kuendeleza utamaduni wa amani, upendo, utulivu na uvumilivu na kuepuka viashiria vinavyoweza kusambaza chuki kwa lengo la kufanikisha chaguzi salama.
Mkuu wa Mkoa huyo amesisitiza umuhimu wa kuutumia uhuru wa kutoa na kupata habari vizuri kwa kusema kwamba uhuru huo usitumike kutoa habari zinazopendelea upande mmoja na kukandamiza mwingine kwa kuwa hali kama hiyo husababisha machafuko.
“Kwa mujibu wa Ibara ya 18 (b) ya Katiba ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, kila mtu anayo haki ya kutafuta, kupokea na kutoa habari bila ya kujali mipaka ya nchi, lakini haki hiyo iende sambamba kwa kuzingatia Sheria za nchi na kuhakikisha habari hizo haziumizi hisia za wananchi wengine,”
DSC_0206
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya akisoma risala wakati wa uzinduzi wa kituo cha redio jamii Uvinza FM ambapo alilipongeza shirika la UNESCO kwa juhudi kuwaweka karibu wananchi na serikali kupitia mawasiliano ya redio.
Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya ameitaka redio jamii Uvinza kuonyesha uwezo wao ili waweze kujitangaza na kujijengea imani kwa wanajamii wao kuwa wanaweza. “Ni kwa hali hiyo tu mtaweza kujulikana, kutambulika na kupata udhamini na matangazo ya kutosha.”
Amewataka wanajamii kukitumia vyema kituo chao cha redio ili kiwe chachu ya kuleta na kukuza maendeleo katika vijiji, wilaya, mkoa na taifa kwa ujumla.
Wakati huo huo Mkuu wa Mkoa ameitaka redio jamii ya Uvinza kutangaza habari zenye kuonyesha madhara ya mila potofu na kujenga uelewa wa jamii kuhusu mila hizo hususan mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), kufichua wagonjwa wanaohofia kuwa na dalili za ugonjwa wa ebola na uharibifu wa mazingira.
Amelipongeza shirika la umoja wa mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kwa kutoa msaada wa vifaa vya kituo hicho na kuendesha mafunzo ya kuwajengea uwezo wanahabari jamii, Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel kwa kuruhusu matangazo ya Uvinza FM Redio yarushwe kupitia mnara wake na waanzilishi wa kituo hicho.
DSC_0120
Mwalikishi wa Shirika la Kimataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) ambaye pia ni mshauri na mkufunzi wa redio jamii, Bi. Rose Haji Mwalimu akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkazi wa UNESCO Tanzania, Zulmira Rodrigues kwenye sherehe za uzinduzi wa kituo hicho cha redio jamii Uvinza FM uliofanyika wilayani Uvinza mkoani Kigoma.
“Ninayapongeza mashirika hayo ya Umoja wa Mataifa na Airtel kwa ufadhili wao, Ruchugi Salt Works na Asasi za kiraia (EHENA) kwa ushirikiano wao kwa jambo hili”
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza Mwalimu Hadijah Nyembo amewakumbusha waandishi wa habari kuepuka kutangaza habari zinazoleta hofu katika jamii kwa kutangaza habari zinazotoa maelezo ya ufafanuzi kutoka chombo husika.
Amekemea matumizi ya lugha isiyo sahihi na kutoeleweka kwa wasikilizaji kwa kusema kwamba redio inalenga makundi yote ya umri kwa hiyo Matangazo yalenge wananchi wote.
“Redio Uvinza isiwe chombo cha propaganda, zingatieni mojawapo ya madhumuni ya kuanzishwa kwa redio zenu ambayo yanalenga kuhamasisha mshikamano, Amani, upendo, utulivu, umoja na utaifa, alisema Mwalimu Nyembo.”
Chombo cha habari jamii Uvinza FM Redio ni cha kwanza kuanzishwa mkoani Kigoma katika halmashauri mpya ya Uvinza.
DSC_0153
"Hongereni sana UNESCO serikali inatambua mchango wenu",...... Ni maneno ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya akimpongeza Mshauri na Mkufunzi kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) ambao ndio wadhamini wakuu wa redio jamii Uvinza FM, Bi. Rose Haji Mwalimu kwa niaba ya UNESCO. Katikati ni Mkurugenzi Mtendaji wa Uvinza FM Radio Bi. Nuru Kalufya.
Chombo hicho kimetakiwa kutumika kuwaunganisha wanajamii, kuepuka kutangaza hisia au uvumi kwa kueleza ukweli na kuwatunzia heshima wasikilizaji wao kwa kuwa wana haki ya kuheshimiwa na kutoumbuliwa masuala yao binafsi.
Uzinduzi huo umeshuhudiwa pia na Mkuu wa wilaya ya Uvinza Mheshimiwa Mwalimu Hadijah Nyembo, viongozi wa chama na serikali, viongozi wa dini, Shirika la Umoja wa Mataifa (UNESCO), Kampuni ya simu za mkononi AIRTEL, wanakijiji na wananchi wa halmashauri ya Uvinza.
Wengine ni wanahabari 30 wanaohudhuria mafunzo ya maadili, jinsia na habari za migogoro kijijini Uvinza, kutoka redio jamii za wilaya 8 ambazo ni Karagwe, Bunda, Mwanza, Kahama, Sengerema, Maswa, Simanjiro, Loliondo, Mpanda, Ngara. Kutoka Zanzibar ni Unguja North, na Southern Pemba (Pemba).
DSC_0082
Meneja wa huduma za kijamii wa Airtel Tanzania, Hawa Bayumi, akitoa salamu kwa wakazi wa wilaya ya Uvinza kutoka kampuni ya simu za mkononi ya Airtel ambao wametoa udhamini wa mnara wao kurusha matangazo ya kituo cha redio jamii Uvinza FM ili kupanua wigo wa usikivu kwa redio hiyo.
DSC_0257
Mkurugenzi Mtendaji wa Uvinza FM Radio Bi. Nuru Kalufya akitoa neno la shukrani kwa mkuu wa mkoa na wadhamini wa kituo hicho cha redio jamii Uvinza FM.
DSC_0054
Meneja wa huduma za kijamii wa Airtel Tanzania, Hawa Bayumi akishiriki kutoa burudani na kikundi cha wakinamama wachimba chumvi Uvinza.
DSC_0164
Baadhi ya viongozi wa dini na jeshi la polisi waliohudhiria uzinduzi huo...Kutoka kulia ni Sheikh Mkuu wa wilaya ya Uvinza Hassan Hamisi, OCD wa Wilaya ya Uvinza S.P Nobert Mahala, Mchungaji wa SDA, Pius Mutani, Mchungaji wa EAG Uvinza, Daniel Magunge na Diwani wa kata ya Ngumka, Abdallah Masanga.
DSC_0333
Baadhi ya waandishi wa habari kutoka redio mbalimbali za jamii waliokuwa wakihudhuria warsha ya siku nane iliyokuwa ikiendelea kwenye kituo cha redio jamii Uvinza FM na wakazi wa wilaya hiyo waliohdhuria sherehe za uzinduzi wa kituo hicho.
DSC_0231
DSC_0226
DSC_0264
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa kituo cha redio jamii Uvinza FM chini ya ufadhili wa Shirika la UNESCO na kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania. Wanaoshuhudia tukio hilo kutoka kulia ni Meneja wa huduma za kijamii wa Airtel Tanzania, Hawa Bayumi, Mwalikishi wa Shirika la Kimataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) ambaye pia ni mshauri na mkufunzi wa redio jamii Bi Rose Haji Mwalimu pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Uvinza FM Radio Bi. Nuru Kalufya.
DSC_0267
Sasa kimezinduliwa rasmi.
DSC_0285
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya akifanyiwa mahojiano mafupi ndani ya studio za redio jamii Uvinza FM na Mtangazaji wa kituo hicho, Kadisilaus Simon mara baada ya kuzindua rasmi redio hiyo.
DSC_0304
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya akisaini kitabi cha wageni ndani ya studio za redio jamii Uvinza FM.
DSC_0308
Mtangazaji wa kituo cha redio jamii Uvinza FM, Kadisilaus Simon akitekeleza majukumu yake kwa furaha kabisa mara baada ya kupewa baraka na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Luteni Kanali Mstaafu Issa Machibya.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages