Breaking News

Your Ad Spot

Feb 18, 2015

Mapigano ya Magaidi na Polisi Mapango ya Amboni Tanga Hii ndio Full Story

NI kama kumekucha! Siku chache tu baada ya Gazeti la Ijumaa (ndugu na hili) kuandika ukurasa wake wa mbele habari yenye kichwa; Kiongozi wa kikundi cha kigaidi kinachoua polisi na kuiba silaha kwenye vituo nchini...NI HUYU, kundi jingine limeibuka na kuandika mkanda wa video wakizungumzia uhalifu....


Cha ajabu, sanjari na kundi hilo linalodai liko Tanga, Tanga hukohuko kwenye Kitongoji cha Amboni, Ijumaa iliyopita kulizuka mapigano kati ya polisi, askari wa JWTZ wakipambana na kundi lililodhaniwa ni la kigaidi likiwa limepiga makazi ndani ya mapango ya kihistoria ya  Amboni, Uwazi lina full story.
Katika mapigano hayo hadi juzi Jumapili, askari mmoja wa JWTZ aliuawa huku wanajeshi watatu na askari polisi wawili wakijeruhiwa na kulazwa Hospitali ya Mkoa wa Tanga, Bombo.



MASHUHUDA WA MAPIGANO 
Kabla Uwazi halijatiririka na video hiyo, lilizungumza na wananchi wenye makazi yao kwenye Kitongoji cha Amboni ambako mapigano ya askari na wahalifu yalitokea.
Mzee Ibrahimu Ally, yeye anasema: “Siku ya tukio (Ijumaa asubuhi) mimi nilikuwa nimepumzika ndani kwangu lakini ghafla nikasikia mlio wa risasi kama mara mbili hivi.

“Mke wangu alikuwa anafua, akaja mbio ndani akisema ni majambazi. Nilimwambia funga mlango haraka sana, akaufunga. Lakini cha ajabu milio ya risasi ikawa inaongezeka kadiri muda ulivyokwenda.
“Ilifika mahali nikajua si majambazi bali tumevamiwa na majeshi ya nje ya nchi. Kwani sasa risasi zilikuwa zikirindima kila muda. Hali ikawa tete kwa kweli. Hata hapa ninapoongea na wewe siamini kama ile milio ya risasi haitajirudia tena.”

WAZIKIMBIA NYUMBA 
Mwanahawa Mudale yeye alisema: “Ilibidi tuhame majumba kwenda kujificha, tatizo ni ile milio ya mabomu na risasi na baadaye tukaona chopa (helikopta) ikitembea angani. Awali tulijua ni vita ya nchi na nchi, kumbe walikuwa askari wetu.”



SIKU MBILI HAKUNA KULALA 
Baadhi ya mashuhuda wanasema kutokana na milio ya risasi kwa siku ya Ijumaa hadi Jumamosi asubuhi, hakuna mwananchi aliyepata usingizi.

“Mimi na familia yangu hatujalala jamani. Risasi na mabomu yasikieni hivihivi tu. Kuna wakati tulikuwa tukiona miale ya moto kutokea kwenye eneo la mapango. Wakati mwingine badala ya moto tuliona moshi mkubwa. 
“Kumbe wanajeshi wetu nao walishafika kupambana na hao watu,” alisema Simeon Patrick, mkazi wa Kitongoji cha Karasha, Amboni.

INAVYODAIWA 
Habari zilizosambaa juzi, zinadaiwa kundi hilo lililopambana na askari ni la kigaidi ambapo safari yao kubwa ilikuwa kwenda kufanya ugaidi wa kumwaga damu nchi jirani ya Kenya.

Wale jamaa nasikia walikuwa wakipeleka vifaa nchini Kenya eneo la mwambao ili waje wafanye uhalifu baadaye.
“Sasa wakiwa katika hatua za mwisho mwisho baada ya kupeleka silaha za kivita, wakashtukiwa. Ikabidi waache silala zao eneo walipozificha na wao waje Tanga kujificha kwenye mapango.

“Lengo lao, watulie mpaka hali kule Kenya itakapokuwa imepoa ndipo wajitokeze. Sasa kilichotokea ni kwamba, wakati wanaishi mapangoni ilibidi waanze kutoka kutafuta chakula kwa kufanya uhalifu mdogomdogo ndipo siku moja jamaa yao mmoja akakamatwa kwa uhalifu.

“Yule jamaa ndiye aliyewapeleka polisi walipo wenzake na kutokea kwa mapigano makali kama yale,” alisema mtoa habari mmoja huku akiomba jina lake lihifadhiwe.

WANACHOAMINI WANANCHI, TOFAUTI NA POLISI
Uwazi lilibahatika kuzungumza na baadhi ya wananchi wa jijini Tanga ambapo karibu wote walikuwa na mtazamo mmoja tu.

“Kutuambia wale ni majambazi si sawasawa. Majambazi wetu tunawajua, polisi wanawatosha sana, sasa hawa wametokea wapi mpaka JWTZ washirikishwe?” alihoji Paulina Mathias, mkazi wa Chumbageni, Tanga.

Kusema ukweli serikali ituambie moja. Lakini wale si majambazi. Kwanza mpaka leo hii (juzi) hawajamkamata hata mmoja zaidi ya kujeruhi askari wetu na kumuua mmoja. Wale ni magaidi, lazima tuwe makini sana,” alisema Ally, mkazi wa Duga Maforoni, Tanga.

KUHUSU VIDEO MPYA
Tukiachana na mapigano ya Amboni, sasa turudi kwenye video mpya ya watu waliojiita ni watetezi wa haki dhidi ya udhalimu.
Video hii ipo ndani ya mitandao mbalimbali ya kijamii ambapo wanaonekana watu wawili wakiwa wamevaa mavazi ya kininja ili wasijulikane.

Watu hao wanasema wanapinga jamii yao kukamatwa na kuuawa mara kwa mara wakidai jeshi linawaonea hivyo kutangaza kupambana na askari.

Video hiyo haipishani sana na ile iliyotangulia kuandikwa kwenye gazeti ndugu na hili la Ijumaa.

KAULI YA JESHI LA POLISI
Akizungumza na Uwazi jijini Tanga muda mfupi baada ya kutulia kwa mapambano ya Amboni, Kamishna wa Polisi-Operesheni na Mafunzo, Paul Chagonja aliwataka wananchi kutulia na kuendelea na shughuli zao za kawaida huku akisisitiza:
“Askari walifika mapangoni, kundi lile ni la majambazi. Lilianza kufanya mashambulizi ya risasi na katika majibizano,  askari sita walijeruhiwa na kuwahishwa katika Hospitali ya Mkoa wa Tanga ya Bombo,” amesema Kamishna Chagonja.    
~GPL

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages