Watu
wawili wamefariki dunia papo hapo na wengine 44 kujeruhiwa baada ya
basi la kampuni ya kidia one lililokuwa likitokea jijini Dar es Salaam
kuelekea jijini Mwanza kugongana uso kwa uso na lori la mizigo
lililokuwa likitoka Dodoma kwuelekea Morogoro katika kijiji cha vikonje
kata ya mtumba nje kidogo ya mji wa Dodoma.
ITV
ilifika eneo la ajali ambapo mashuhuda wa ajali hiyo akiwemo dereva
msaidizi wa basi aliyejitambulisha kwa jina moja la Makubeli akisema
chanzo cha ajali hiyo ni baada ya basi kuharibika mfumo wa breki na
kumshinda dereva mwenzake kauli inayopingana na mmoja kati ya abiria
aliyekuwemo kwenye basi hilo ambaye anadai chanzo ni mwendo kasi ambapo
dereva wa basi alikuwa akijaribu kulipita basi jingine lililokuwa mbele
yao bila tahadhari na ghafla akakutana uso kwa uso na lori.
Kamanda
wa polisi mkoa wa Dodoma Sasp David Misime amesema chanzo cha ajali
kimetokana na dereva wa basi hilo lenye namba za usajili T 663 AXL aina
ya Scania alipokuwa akijaribu kulipita gari lingine bila kuchukua
tahadhari na kukutana uso kwa uso na lori lenye namba za usajili T 496
CFG likiwa na tela namba T 576 AXZ ambapo watu wawili waliofahamika kwa
majina ya Fadhili Saidi dereva wa lori na Chogo Chigunda utingo wa basi
wakafariki dunia.
Kwa
upande wake mganga mkuu wa hospitali ya mkoa wa Dodoma Dk Nasoro Mzee
amethibitisha kupokea maiti hizo mbili na majeruhi 44 ambapo 16
wametibiwa na kuruhusiwa huku wengine 27 wakilazwa.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269