Breaking News

Your Ad Spot

Mar 12, 2016

BABU SEYA, PAPII, MAPOKEZI YA KIFALME!

babuseyarufaa2
Nguza Vicking ‘Babu Seya’ na mwanaye, Johnson Nguza ‘Papii Kocha’
NA MWANDISHI WETU Risasi Jumamosi
DAR ES SALAAM! Inawezekana ikawa habari njema kwa mashabiki wao kusikia kwamba familia ya mwanamuziki aliyefungwa maisha jela kwa kosa la kuwanajisi watoto 9, Nguza Vicking ‘Babu Seya’ na mwanaye, Johnson Nguza ‘Papii Kocha’, ipo katika maandalizi makubwa ya kuwapokea kifalme wawili hao mara watakapotoka gerezani, Risasi Jumamosi lina habari kamili.
babu seya na papii (1)
Nguza Vicking ‘Babu Seya’ na bendi yake wakitumbuiza.
KWA MUJIBU WA CHANZO
Chanzo kilichozungumza na gazeti hili katikati ya wiki hii kilisema kuwa familia hiyo imejipanga kwa ujio wa wapendwa wao hao kwa vile inaamini mambo sasa yamefikia mwisho na watatoka jela.
“Jamani kuna ishu ipo chini kwa chini ndani ya familia ya Babu Seya, nimepata habari kwamba wameanza maandalizi ya kumpokea yeye na mwanaye, Papii watakapotoka jela.
“Kinachoonekana ni kwamba wanajua siku yoyote ile watatoka. Sasa sijajua nini kitawatoa, maana hivi karibuni nimesoma kwenye vyombo vya habari kwamba shauri lao limetua kwenye Mahakama ya Haki za Binadamu Afrika (AfCHPR). Nadhani kuna mwanga wameuona kule,” kilisema chanzo hicho.
babu seya na papii (2)
Babu Seya akicharaza gitaa.
WATAPIGA MUZIKI?
Chanzo hicho kilisema kuwa miongoni mwa mambo yatakayofanywa na wawili hao baada ya kutoka ni kufanya shoo kwa kupiga muziki kuzunguka nchi nzima kwa lengo la kuwashukuru Watanzania kwa kuwaombea katika kipindi chote cha mapito yao.
“Lakini hili la kupiga shoo mnaweza kufuatilia zaidi kwa ndugu, kama wataona hakuna haja ya kulificha watawaambia, kama wameamua kulihifadhi basi lakini ndiyo ninachojua mimi.”
babu seya na papii (3)
Papii Kocha akiimba (Picha zote na maktaba).
FAMILIA HAIJAWAHI KUKATA TAMAA Chanzo: “Mnajua tangu walipofungwa wale wote, wakiwemo wale walioachiwa huru, Francis na Mbangu, familia haijawahi kukata tamaa hata siku moja.
“Wamekuwa bega kwa bega kila wakati gerezani, mara kukata rufaa mpaka ikafika mahali rufaa zikaisha. Lakini nadhani huko kwenye mahakama walikoenda kupeleka malalamiko yao, kuna matumaini makubwa ndiyo maana familia imeanza kujipanga kuwapokea.”
RISASI NA MBANGU NGUZA Baada ya kusikia kutoka kwa chanzo hicho, Risasi Jumamosi lilimsaka Mbangu Nguza, kaka wa Papii Kocha ili kumsikia anasemaje kuhusu kuwepo kwa madai ya baba yake na mdogo wake kutoka jela na kuwepo kwa maandalizi ya mapokezi makubwa. Risasi Jumamosi: “Mbangu habari za leo?” Mbangu: “Njema bwana, nani mwenzangu?”
Risasi Jumamosi: (likajitambulisha). Mbangu: “Ooo! Za siku bwana? Upo?” Risasi Jumamosi likasema lipo kisha likaanza na mahojiano moja kwa moja ili kuokoa muda… “Nilitaka kujua, kuna madai kwamba mzee na Papii wanatoka jela hivi karibuni. Unasema nini kuhusu hilo?”
Mbangu: “Kwanza wamechelewa sana kutoka, ilitakiwa wawe nje siku nyingi sana, yaani wamechelewa ndugu yangu.” Risasi Jumamosi: “We unadhani watatokaje? Ni kwa vile wamepeleka rufani yao Mahakama ya Haki za Binadamu Afrika au kuna njia nyingine?”
Mbangu: “Huko mimi siingilii, lakini najua watatoka. Kwa kuwa familia imekuwa ikiomba usiku na mchana watoke, sasa wanakaribia kutoka na wamechelewa.” Risasi Jumamosi: “Wewe una uhakika kwa asilimia ngapi kwamba watatoka?” Mbangu: “Mia moja! Mungu wangu ninayemwabudu mimi akijibu maombi hatoi asilimia chache, ni mia moja nakuhakikishia wanatoka.”
Risasi Jumamosi: “Chanzo chetu kimesema familia imeandaa mapokezi ya kifalme, ni kweli?” Mbangu: “Siku hiyo itakuwa ya kipekee kwa familia. Lakini nini kimeandaliwa hilo jukumu lipo kwa familia mimi silisemei. Kuna watu wanashughulikia kila kitu. Unajua siku hizi nimejikita kwenye huduma ya Mungu kwa hiyo kuna watu wanashughulikia masuala yao.”
Risasi Jumamosi: “Huwa unakwenda kuwaona gerezani?” Mbangu: “Yeah! Huwa nakwenda mara kwa mara, lazima si baba yangu na mdogo wangu bwana, lazima kwenda.”
Risasi Jumamosi: “Nakushukuru sana bwana Mbangu.” Mbangu: “Haya bwana, kazi njema.”
RUFAA YAO IMEPITIWA JANA Jana, Mahakama ya Haki za Binadamu Afrika katika kikao chake cha 40 kilichoanza jijini Arusha, ilitarajiwa kupitia maombi ya rufaa ya Babu Seya na Papii dhidi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (JMT).
SIRI KUTAWALA Kwa mujibu wa taarifa ya mahakama hiyo kwa vyombo vya habari, rufaa hiyo Namba 006/2015 ilipangwa kusikilizwa kwa siri na si kwenye mahakama ya wazi (open court).
KESI MBILI TU Mahakama hiyo ilitarajiwa kusikiliza rufani 50 lakini katika hizo, ni mbili tu ndizo zitakazosikilizwa kwenye mahakama ya wazi na kutolewa hukumu Machi 18.
KUMBUKUMBU MUHIMU Juni 25, 2004, Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam, Addy Lyamuya aliwatia hatiani Babu Seya na wanaye watatu, Papii Kocha, Mbangu na Francis. Januari 27, 2005, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Thomas Mihayo alitupilia mbali rufaa yao iliyokuwa ikipinga hukumu hiyo. Wakili wao, Mabere Nyaucho Marando akapeleka suala hilo Mahakama ya Rufaa Tanzania ambako Mbangu na Francis waliachiwa huru, Babu Seya na Papii wakaonekana bado wana hatia. Babu Seya na wanaye walidaiwa kutenda makosa 10 ya kubaka na kulawiti watoto hao kati ya Aprili na Oktoba, 2003 katika maeneo ya Sinza ya Palestina, Dar es Salaam. Mpaka sasa wana miaka 12 gerezani.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages