Imeelezwa kuwa wastani wa
unyonyeshaji kwa watoto walio chini ya miezi sita nchini sio mzuri na
hivyo kuwa na uwezekano wa watoto kudhoofika kwa kukosa maziwa ya mama
ambayo yanakuwa na virutibisho muhimu kwa ukuaji ya mtoto.
Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe, Dkt. Joyceline Kaganda katika
warsha iliyoandaliwa na UNICEF ili kujadili jinsi uwekezaji mkubwa zaidi
katika kunyonyesha maziwa ya mama kunaweza kusaidia maendeleo kiuchumi
na kuokoa maisha ya watoto nchini.
Dkt. Kaganda amesema wastani wa
unyonyeshaji kwa watoto walio chini ya miezi sita ni asilimia 42 na
wastani huo ni mdogo hivyo kuashiria kuwa hali sio njema kwa watoto
ambao hawapati maziwa ya mama.
Amesema kiafya inatakiwa mtoto aanze
kunyonya nusu saa baada ya kuzaliwa na mtoto anyonye maziwa ya mama
yake kwa kipindi kisichopungua miezi sita na baada ya hapo anaweza
kuanza kuwa anachanganya na vyakula vingine kama uji na maji.
“Hali sio nzuri ukiangalia wastani
wa wamama ambao wanawapa watoto wao maziwa ya kunyonya ni wachache na
labda inawezekana wengi wakawa hawatambui matatizo yanayoweza kutokea
kama hawatawanyonyesha watoto wao,” amesema Dkt. Kaganda.
Aidha Dkt. Kaganda amesema kazi
zinachangia kina mama wengi kushindwa kuwanyonyesha watoto wao lakini
wanaweza kuweka utaratibu wa kuwa wanakamua maziwa yao na kuyahifadhi
sehemu nzuri ili hata kama wanapokuwa mbali na watoto wao, msimamizi
anayemuangalia mtoto aweze kumpa mtoto ili kumfanya apate virutubisho
muhimu kutoka kwenye maziwa ya mama yake.
Nae Mwakilisha wa Shirika la
Kimataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) nchini, Bi. Maniza Zaman amesema
katika kusaidia Tanzania kuongeza wastani wa watoto ambao wananyonya
wamekuwa wakitoa elimu kwa kina mama wanaonyonyesha pamoja na familia
zao ili wajue umuhimu wa mtoto kunyonya maziwa ya mama.
Alisema watoto wengi wamekuwa
wakipoteza maisha kwa matatizo ambayo yanatokana na kukosa maziwa ya
mama zao na hivyo ili kuzidi kushughulikia tatizo hilo wanataraji kuanza
kutoa elimu kwa watumishi wa afya katika mikoa ya Mbeya, Iringa na
Njombe na wanataraji kutembelea zaidi maeneo ya vijijini kutokana maeneo
hayo kuonekana kutokuwa na elimu hiyo zaidi.
“Watoto wamekuwa wakipata matatizo
na kupoteza maisha na hiyo inachangiwa na kutokunyonya kwa mama …
tumeshirikiana na serikali tunataraji kutoa elimu katika vijiji zaidi ya
15,000 kwenye mikoa ya Njombe, Iringa na Mbeya na tutafundisha pia mama
na familia umuhimu wa mtoto kunyonya,” alisema Bi. Zaman.
Alisema baada ya kumalizika kwa
mikoa hiyo wataendeleza utoaji wa elimu nchi nzima ili jamii ya Tanzania
itambue umuhimu wa watoto kunyonya maziwa ya mama na pia kuwaomba
waandishi wa habari kutumia nafasi yao katika jamii ili kuwaelimisha
watanzania kuhusu tatizo hilo.
Katika makala zilizoandikwa katika
jarida la habari za afya la The Lancet linaonyesha kuwa uboreshaji wa
kunyonyesha maziwa ya mama kunaweza kuokoa maisha zaidi ya watoto
820,000 kila mwaka duniani na Dola za Kimarekani Bilioni 302 kila mwaka.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269