Breaking News

Your Ad Spot

May 17, 2016

WABUNGE WA UPINZANI AFRIKA KUSINI WABURUZWA NJE YA BUNGE KWA KUZUIA HOTUBA YA ZUMA


Kwa mara nyingine tena, Bunge la Afrika Kusini limegeuka na kuwa ukumbi wa mieleka na malumbano kufuatia hatua ya wabunge wa upinzani kuzusha fujo kwa lengo la kuzuia hotuba ya Rais Jacob Zuma wa nchi hiyo.
Maafisa wa kusimamia usalama Bungeni wamewatoa nje kwa nguvu wabunge wa chama cha upinzani cha Economic Freedom Fighters kinachoongozwa na Julius Malema, kinara wa upinzani na mkosoaji mkubwa wa serikali ya Rais Zuma.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutolewa nje, Malema amesema Rais Zuma amepoteza haiba na itibari ya kuwa kiongozi wa nchi hiyo na kwa msingi huo, hawatamruhusu alihutubie bunge hilo kwa amani. Ameongeza na hapa tunanukuu: "Zuma hatawahi kupata amani katika Bunge hili, hatuwezi kuongozwa na mtu ambaye ameshindwa kutii, kutetea na kulinda katiba ya nchi."Mwisho wa kunuku.
Itakumbukwa kuwa, mapema mwezi huu, wabunge wa upinzani walizusha vurumai Bungeni kwa shabaha ya kuzuia hotuba ya Rais Jacob Zuma juu ya bajeti. Floyd Shivambu, Naibu Rais wa chama hicho aliliambia bunge hilo chini ya kiwingu cha vurumai kuwa: "Hatuwezi kumruhusu rais anayekabiliwa na tuhuma za ufisadi kuhutubia taifa kana kwamba hakuna chochote kilichofanyika."
Wapinzani nchini Afrika Kusini wanamtuhumu Zuma kuwa ni kiongozi fisadi, haswa baada ya Mahakama ya Katiba ya nchi hiyo kumpata na hatia ya kukiuka katiba na kumuagiza kulipa sehemu ya fedha zilizotumiwa katika ukarabati wa nyumba yake binafsi katika eneo la KwaZulu Natal, mradi ambao uligharimu zaidi ya dola milioni 16 za Marekani. Hata hivyo Rais Zuma alinusurika kura ya kutokuwa na imani naye bungeni kufuatia kashfa hiyo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages