Breaking News

Your Ad Spot

Aug 20, 2016

DUNIA YAENDELEA KUKOSOA UKIUKWAJI WA HAKI ZA BINADAMU WA SAUDIA

Ukiukaji wa haki za binadamu unaofanywa na Serikali ya Saudi Arabia umeendelea kukosolewa vikali katika duru mbalimbali za kikanda na kimataifa.
Saudi Arabia inayotambuliwa kuwa husuni na ngome ya udikteta ni miongoni mwa wakiukaji wakubwa wa haki za  binadamu duniani. Watawala wa kifalme wa nchi hiyo hawaheshimu haki za binadamu si ndani ya Saudia pekee bali hata katika kanda hii ya Asia. 
Ndani ya Saudi Arabia kwenyewe wanawake na Waislamu wa madhehebu ya Shia ndio wahanga wakubwa zaidi siasa za kikandamizaji wa Aal Saud. Wanawake nchini humo hawana hata haki ya kuendesha magari yao wenyewe na hata haki ya kupiga kura waliyopewa hivi karibuni bado haijaanza kutekelezwa. 
Msomi wa Kishia, Sheikh Nimr alinyongwa kwa sababu ya kukosoa serikali Saudia
Vyombo vyote vya habari vya Saudi Arabia vinamilikiwa na watu wa kizazi tawala na ni kosa la jinai kukosoa wanamfalme na viongozi wa nchi hiyo. Ubaguzi wa kijamii hususan dhidi ya Waislamu wa madhehebu ya Shia unaonekana kila mahala. Nchini Saudi Arabia wananchi hawana haki yoyote isipokuwa kutii amri za utawala wa kifalme. 
Watawala wa kizazi cha Aal Saud hususan katika kipindi cha miaka mitano ya hivi karibuni wamekuwa miongoni mwa wakiukaji wakubwa wa haki za binadamu katika nchi nyingine. Serikali ya nchi hiyo inawaunga mkono na kuwafadhili kwa hali na mali magaidi nchini Syria ambako maelfu ya raia wasio na hatia wanauawa kila siku.
Machi mwaka 2015 utawala wa kifalme wa Saudi Arabia ulianzisha mashambulizi ya kinyama dhidi ya nchi maskini zaidi ya Kiarabu katika eneo la Mashariki ya Kati yaani Yemen, na mashambulizi hayo bado yanaendelea. Matokeo ya mashambulizi hayo ni kuuawa maelfu ya Waislamu wasio na hatia, kuharibiwa asilimia 80 ya miundombinu ya nchi hiyo, kuwafanya Wayemeni milioni 3 kuwa wakimbizi, kuharibu umoja wa kitaifa wa nchi hiyo na kuwapa magaidi fursa ya kudhibiti baadhi ya maeneo ya Yemen.
Watoto wa Yemen wanaendelea kuuawa na jeshi la Saudia
Huko Iraq pia watawala wa Saudi Arabia wanawaunga mkono magaidi wa kundi la kiwahabi la Daesh na wanafanya kila wawezalo kudhoofisha serikali ya nchi hiyo kupitia njia ya kuzusha mivutano ya kikaumu na kimadhehebu. 
Licha ya hayo yote lakini tawala zinazodai kutetea demokrasia na haki za binadamu za Magharibi hususan Marekani si tu kwamba hazijachukua hatua yoyote dhidi ya Saudia bali zinaiunga mkono na kuisaidia. Miongoni mwa vielelezo vya uungaji mkono wa nchi za Magharibi kwa utawala katili wa Saudi Arabia ni kuchaguliwa nchi hiyo kama Mwenyeliti wa Baraza la Haki za Binadamu katika Umoja wa Mataifa, suala ambalo limetambuliwa na wachambuzi wengi wa mambo kuwa ni sawa na nchezo mchungu wa kuigiza wa kisiasa. Suala hilo linakosolewa sana na taasisi za kiraia na jumuiya za kimataifa za kutetea haki za binadamu.
Katika uwanja huo jana Ijumaa katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Ubinadamu wanaharakati wa masuala ya kiraia nchini Uingereza walimtaka Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Theresa May kupinga suala la kuchaguliwa tena Saudi Arabia kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Haki za Binadamu.
Magaidi wa kundi la Daesh wanaoungwa mkono na Saudia wanavyokata vichwa vya watu Iraq na Syria
Wakati huo huo Belkis Wille ambaye ni mhakiki mkuu wa shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch (HRW) ametoa taarifa akilitaka Bunge la Marekani kupinga mauzo ya silaha zenye thamani ya dola bilioni 1.15 kwa serikali ya Saudi Arabia. Sababu ya ombi hilo ni kwamba HRW inaamini Saudia inatumia silaha hizo kuua watu wa Yemen. Awali shirika hilo la kutetea haki za binadamu lilitoa wito wa kufanyika uchunguzi huru kuhusu jinai za kivita zilizofanywa na Saudi Arabia nchini Yemen.
Nchi na mashirika mengine ya kimataifa ya kutetea haki za binadamu kama Amnesty International pia yametaka kufanyike uchunguzi kuhusu ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu, mauaji na jinai zinazoendelea kufanywa na Saudi Arabia na washirika wake dhidi ya raia wa Yemen.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages