Breaking News

Your Ad Spot

Aug 30, 2016

MAKAMU WA RAIS MHE. SAMIA SULUHU AHUDHURIA UFUNGUZI WA MKUTANO WA 36 WA SADC MJINI MBABANE SWAZILAND

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisaini ubao wa kumbukumbu kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli wenye majina ya viongozi waliohudhuria mkutano wa 36 wa SADC uliofanyika Lozitha, Mbabane Swaziland.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan (katikati) akiwa kwenye mkutano wa 36 wa Wakuu wa Nchi na Serikali za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) uliofunguliwa leo kwenye ukumbi wa Mandvulo uliopo Lozitha, Swaziland.
Mfalme Mswati wa III (kushoto) akihutubia kwenye ufunguzi wa mkutano wa 36 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC kwenye ukumbi wa Mandvulo, Lozitha Swaziland.
Binti akionyesha bendera ya Tanzania wakati wa kuimba shairi maalum ya ufunguzi wa mkutano wa 36 wa SADC
Wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya ufunguzi wa mkutano wa 36, Lozitha Swaziland.
  ....................................... 

Mwenyekiti anayemaliza muda wake wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika -SADC- ambaye pia ni Rais wa Botswana Luteni Jenerali Dkt. Seretse Khama Ian Khama amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa kwake kwa kishindo katika uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka jana.

Rais huyo wa Botswana ametoa kauli hiyo ya pongezi katika hotuba yake kwenye ufunguzi wa Mkutano wa 36 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC unaofanyika Mbabane- Swaziland ambapo Katika Mkutano huo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dakta JOHN POMBE MAGUFULI anawakilishwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Rais huyo wa Botswana amesema ukuaji wa demokrasia katika nchi wanachama wa jumuiya ya SADC unaendelea kuimarika hivyo ni muhimu jitihada hizo zikaendelezwa zaidi.

Amesema ana Imani kubwa na Viongozi waliochaguliwa kwa njia ya amani,uhuru na haki katika ukanda wa SADC akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Jamhuri ya Visiwa shelisheli kwamba watafanya kazi kwa bidii ili kuharakisha maendeleo kwa wananchi wao.

Wakuu wa nchi na Serikali wa SADC katika mkutano huo wameshuhudia utoaji wa zawadi mbalimbali kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika utunzi wa insha na kwa wanahabari ambao wameandika habari mbalimbali kuhusu SADC ikiwemo masuala ya huduma ya maji.

Aidha Katika Mkutano huo wa 36 wa SADC viongozi wanaohudhuria watafanya uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa SADC na Uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Asasi ya SADC ya Siasa, Ulinzi na Usalama ( SADC Troika)

Katika mkutano huo Wakuu wa nchi na serikali pia watapokea rasimu za maboresho ya mikataba mbalimbali kutoka kwenye Baraza la Mawaziri kwa ajili ya kutia saini. Miongoni mwa rasimu hizo ni mkataba wa kuboresha itifaki ya SADC dhidi ya rushwa, maboresho ya itifaki ya ushirikiano wa siasa, ulinzi na usalama ya SADC na maboresho ya itifaki ya biashara.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages