Breaking News

Your Ad Spot

Sep 10, 2016

RAIS WA GABON KUKUBALI KUHESABIWA KURA UPYA

Rais Ali Bongo Ondimba wa Gabon amekubaliana na ushauri wa kuhesabiwa upya kura za uchaguzi wa hivi karibuni uliozusha machafuko nchini humo. Hata hivyo amesema, uamuzi wa mwisho kuhusu suala hilo umo mikononi mwa Mahakama ya Katiba ya Gabon.
Kwa upande wake, Jean Ping, mpinzani mkuu wa Rais Ali Bongo na ambaye alikuwa mgombea wa muungano wa vyama vya upinzani katika uchaguzi wa rais wa Oktoba 27 amesema kuwa, hana imani na majaji wa Gabon kwani wote wanadhibitiwa na Rais Ali Bongo.
Pamoja na hayo, Jean Ping amewasilisha mashtaka katika mahakama hiyo akitaka kuhesabiwa upya kura za mkoa wa Houto Ogooue. Kwa mujibu wa tume ya uchaguzi ya Gabon, asilimia 99 ya wapiga kura wa mkoa huo walishiriki kwenye uchaguzi huo na matokeo yaliyotangazwa ya kura za mkoa huo zinaonesha kuwa Ali Bongo amepata ushindi wa zaidi ya asilimia 95 ya kura za mkoa huo ambayo ni ngome yake.
Tume ya taifa ya uchaguzi ya Gabon inadai kuwa ushiriki wa wapiga kura katika mikoa mingine ya nchi hiyo ni asilimia 60, sasa suala hilo limewatia wasiwasi mkubwa wapinzani na kutilia shaka uwezekano wa kushiriki asilimia 99 ya wapiga kura katika mkoa huo. Mkoa wa Houto Ogooue ni wa kabila la Tek la Rais Ali Bongo, hivyo wachambuzi wa mambo wanasema si jambo la kushangaza kuona kuwa Ali Bongo amepata ushindi mkubwa kwenye mkoa huo.
Machafuko nchini Gabon baada ya kutangazwa matokeo ya uchaguzi na kupingwa na wapinzani 

Hii ni kusema kuwa, majaji wa Mahakama ya Katiba ya Gabon wana muda wa siku 15 kutoa uamuzi wa mwisho kuhusu mgogoro wa matokeo ya uchaguzi ulioikumba  nchi hiyo. Wafuasi wa Jean Ping wameonya kuwa, kupeleka mashtaka kwa Mahakama ya Katiba ambayo majaji wake 9 ni wafuasi wa Rais Ali Bongo ni kujitia kitanzi cha kisheria, na itakuwa ni madhara kwa wapinzani na kunaweza kushadidisha machafuko nchini humo.
Ikumbukwe kuwa watu karibu 800 wametiwa mbaroni kwa kuhusika na machafuko yaliyotokea hivi karibuni baada ya kutangazwa matokeo ya uchaguzi. Wafuasi wa Jean Ping wanasema kuwa watu baina ya 50 hadi 100 wameuawa katika machafuko, lakini duru za serikali zinasema ni watu watatu tu waliopoteza maisha yao kwenye machafuko hayo. Kwa kweli hali ya kiusalama huko Libreville, mji mkuu wa Gabon ni mbaya na hali hiyo imeulazimisha Umoja wa Afrika AU kuingilia kati ili kumaliza mgogoro wa kisiasa wa nchi hiyo.  
Ujumbe wa AU unaoundwa na baadhi ya viongozi wa nchi za Afrika ukiongozwa na Rais Idris Deby wa Chad ambaye ndiye mwenyekiti wa hivi sasa wa Umoja wa Afrika, ulitarajiwa kuwasili mjini Libreville jana Ijumaa tarehe 9 Septemba, hata hivyo ujumbe huo umeakhrisha safari yake hiyo kwa sababu zisizojulikana.
Hivi sasa kuna wasiwasi kwamba wafuasi wa Jean Ping wataitikia mwito wake wa kufanya mgomo wa nchi nchi nzima, na hivyo kuifanya hali kuwa tete zaidi ya ilivyo hivi sasa nchini humo.
Jambo jengine ambalo linaonekana hivi sasa ni kuwa, tofauti na miongo ya huko nyuma, sasa hivi Ufaransa imejizuia kuingilia mgogoro wa nchi hiyo inayozungumza lugha ya Kifaransa. Msemaji wa serikali ya Ufaransa amesisitiza kuwa, hivi sasa ni wakati wa mabadiliko na Ufaransa inaunga mkono uamuzi wowote utakaochukuliwa na Umoja wa Afrika kuhusiana na Gabon.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages